1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

KHARTOUM : Sudan yakubali rasmi uwekaji vikosi Dafur

1 Agosti 2007
https://p.dw.com/p/CBdA

Sudan leo imesema imekubali rasmi Azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye kuidhinisha uwekaji wa kikosi mchanganyiko cha kulinda amani katika jimbo la Dafur nchini Sudan.

Waziri wa mambo ya nje wa Sudan Lam Akol amewaambia waandishi wa habari kwamba wanatangaza kukubali kwao azimio hilo ikiwa ni siku moja baada ya baraza la usalama kuidhinisha kikosi hicho mchanganyikko cha Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa kulinda amani huko Dafur ambapo watu wanaokadiriwa kufikia 200,000 wameuwawa kutokana na vita na njaa tokea mwaka 2003 na wengine milioni mbili kupotezewa makaazi yao.

Serikali ya Ujerumani imeukaribisha uamuzi huo wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wa kuweka wanajeshi 26,000 kulinda amani Dafur hata hivyo imesema haiyumkiniki kutuma wanajeshi wake zaidi huko Dafur kwa ajili ya shughuli za kulinda amani.

Msemaji wa serikali ya Ujerumani Thomas Steg amesema Ujerumani itaendelea kutekeleza ahadi yake ya kuwa na wanajeshi 200 kusaidia kuvisafirisha vikosi vya Umoja wa Afrika.

Walinda amani wa Umoja wa Mataiafa watakuwa na mamlaka ya kutumia nguvu ikibidi katika kuwalinda raia na wafanyakazi wa misaada huko Dafur.

Vikosi vya kwanza vinatazamiwa kuwasili Dafur hapo mwezi wa Oktoba.