1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kifo cha Rabbani ni pigo kwa amani Afghanistan

21 Septemba 2011

Rais wa zamani wa Afghanistan, Burhanuddin Rabbani ameuawa katika shambulio la kujitoa mhanga lililofanywa nyumbani kwake hapo jana mjini Kabul.

https://p.dw.com/p/Rmv1
Burhannudin Rabbani alieongoza jitahada za amaniPicha: dapd

Kifo cha Rabbani aliekuwa akiongoza jitahada za amani nchini Afghanistan, kimezusha wasiwasi mpya huku wengine wakiuliza iwapo nchi hiyo itarejea kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe. Bila shaka kifo hicho ni pigo kubwa kwa jitahada za kupatana na waasi nchini Afghanistan. Kwani yeye, alikuwa mwenyekiti wa Baraza Kuu la Amani linaloongoza jitahada za kujadiliana na Wataliban. Hiyo jana, Rabbani aliekuwa na miaka 71, alipanga kukutana na wanachama wawili wa Taliban nyumbani kwake. Mwanachama wa baraza hilo la amani, Fazel Karim Aymaq amesema, wageni wawili waliodai kuwa na ujumbe muhimu kutoka kwa Wataliban, walikaribishwa ndani ya nyumba. Mmoja wao alimkumbatia Rabbani na akaripua miripuko iliyofichwa ndani ya kilemba chake. Viongozi wa kimataifa wamelaani vikali mauaji hayo. Rais wa Marekani Barack Obama amesema:

"Tumepokea habari za huzuni hii leo kuwa rais wa zamani Rabbani aliekuwa akiongoza mchakato wa upatanisho ameuawa katika shambulio la kujitoa mhanga. Alikuwa mtu aliejitolea kwa Afghanistan na alithaminiwa kama mshauri wa Rais Karzai. Vile vile ametoa mchango mkubwa kuijenga upya nchi. Kwa hivyo ni msiba mkubwa."

Afghanistan President Hamid Karzai seen during a meeting with his Turkish counterpart Abdullah Gul in Istanbul, Turkey, Monday, Jan. 25, 2010. Turkish, Afghan and Pakistani presidents meet in Istanbul for Turkish-sponsored talks aimed at reducing tensions between Afghanistan and Pakistan. (AP Photo/Osman Orsal, Pool)
Rais wa Afghanistan Hamid Karzai amevunja ziara yake MarekaniPicha: AP

Na Rais wa Afghanistan, Hamid Karzai aliekwenda Marekani kuhudhuria mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York, ameamua kurejea nyumbani. Alipozungumza kwenye mkutano wake na Rais Obama, pembezoni mwa mikutano ya Umoja wa Mataifa, alisema ni siku ya uchungu mkubwa lakini pia ni siku ya umoja na ya kuendeleza jitahada za amani. Amesema, itakuwa shida kuziba pengo aliloliacha. Akaongezea:

„Ameyatoa mhanga maisha yake kwa ajili ya Afghanistan na amani ya nchi. Alijibebesha jukumu lililo muhimu kwa watu wa Afghanistan na usalama wa taifa na amani nchini mwetu."

Hata kama hakuna uhakika iwapo Rabbani, angefanikiwa kupata makubaliano ya amani katika nchi iliyokumbwa na vita vya miongo mitatu, moja ni hakika: mauaji yake ni pigo kwa jitahada za serikali na yamedhihirisha jinsi waasi walivyojiimarisha. Vile vile, kifo cha Rabbani wa kabila la Tajik, huenda kikatifua zaidi uhusiano wenye utata, kati ya makundi ya kikabila ya walio wachache na jamii kubwa ya kabila la Pashtun nchini Afghanistan.

An Afghan policeman runs to the scene of a suicide attack in Kabul, Afghanistan, Tuesday Sept. 20, 2011. Former Afghan President Burhanuddin Rabbani, who headed a government peace council set up to facilitate contacts with Taliban insurgents, was assassinated Tuesday by a suicide bomber concealing explosives in his turban, officials said. Four of Rabbani's bodyguards also died and a key presidential adviser was wounded. (Foto:Kamran Jebreili/AP/dapd)
Polisi wamezingira eneo lenye nyumba ya RabbaniPicha: dapd

Leo mjini Kabul, mamia ya watu waliobeba picha za Rabbani na mabango wamekusanyika karibu na nyumba yake kumkumbuka mwanasiasa huyo na kupinga mauaji yake. Wengine wamekusanyika nje ya mlango mkuu wa nyumba ya Rabbani wakisoma Qurani. Rais Karzai amesema, Rabbani atazikwa keshi au kesho kutwa kwa heshima za taifa.

Mwandishi: Martin,Prema/ Hasrat-Nazimi, Waslat

Mhariri: Abdul-Rahman