1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiongozi wa zamani wa Korea Kusini afungwa miaka 24 jela

Sudi Mnette
6 Aprili 2018

Kiongozi wa zamani wa Korea Kusini amehukumiwa kifungo cha miaka 24 kwa makosa ya rushwa na kuhitimishwa kwa anguko lake kutoka neema ya mwanamke wa kwanza kiongozi ambae amegeuka kuwa chukizo la umma na wa kudharaulika.

https://p.dw.com/p/2vakd
Park Geun-hye
Kiongozi wa zamani wa Korea Kusini Park Geun-hyePicha: picture-alliance/AP Photo/K. Hong-Ji

Hukumu hiyo imetolewa baada ya kesi iliyodumu miezi kumi ambayo imekamilika kwa Park Guen-hye   kukutwa na hatia ya makosa kadhaa ikiwa pamoja na utoaji rushwa na matumizi mabaya ya madaraka. Mrithi wa kiongozi huyo ameielezea hukumu hiyo kuwa ni ya kuvunja moyo kwa taifa na kiongozi huyo wa zamani mwenyewe. Jaji Kim Se-yoon, aliyeitoa hukumu hiyo, amesema Park anatuhumiwa kuyatumia vibaya madaraka aliyopewa na umma.

Aidha ameongeza kusema kiasi cha hongo ambacho Park alipokea au kudai kwa ushirikiano na mshirika wake wa karibu na rafiki wa muda mrefu Choi Soon-sil kilikuwa zaidi ya dola milioni 20. Park mwenye umri wa miaka 66, alisusia sehemu kubwa ya vikao vya kesi hiyo akilalamika kuhusu hatua ya kuwekwa kizuizini. Idadi kubwa ya tuhuma za kashfa za vitendo vya rushwa zenye kuwaunganisha wafanyabiashara wakubwa na wanasiasa nchini Korea Kusini, zilizusha maandamano makubwa dhidi ya kiongozi huyo wa zamani.

Uamuzi wapokewa kwa wasiwasi

South Korea Corruption Scandal
Wafuwasi wa Park Geun-hyePicha: picture alliance/AP Photo/A. Young-Joon

Lakini uamuzi huu wa Ijumaa hii imepokewa kwa hali ya wasiwasi katika mitaa ya karibu na jengo la mahakama mjini Seuol, na mamia ya waandamanaji, wafuasi wa Park walikuwa wakipeperusha bendera. Wengi wao walikuwa wakibubujikwa na machozi huku wengine wakifanya mkusanyiko wa kupinga hukumu. Mwanandamanaji mmoja mwenye umri wa miaka 27 Han Geun hyung alisikika akisema "Utawala wa sheria katika taifa hili umekufa."

Wakili wa Park Kang Cheol-Gu amesema "Upande wa utetezi tumejitahidi, lakini tunasikitishwa na uamuzi wa leo wa mahakama, ambao kwa kweli ni mbaya. Hata hivyo huu ni uamuzi wa hukumu ya kwanza. Tunaamini majaji watatoa uamuzi sahihi katika rufaa na Mahakama Kuu."

Hata hivyo Park mwenyewe hakuwepo mahakamani wakati hukumu yake ikitolewa, katika hatua hiyo ya nadra kabisa iliyokuwa ikioneshwa moja kwa moja na televisheni. Alikuwa akifanya mgomo wa kuhudhuria mahakamani karibu kesi zake zote wakati akishikiliwa rumande. Lakini mahakama imempa muda wa siku saba kuukatia rufaa uamuzi huo.

Park anakuwa kiongozi wa tatu wa Korea Kaskazini kukutwa na hatia ya vitendo vya uhalifu baada ya kuondoka madarakani, akiungana na Chun Doo-whan na Roh Tae-woo, ambao wote kwa pamoja walikutwa na hatia ya uhaini na ruswa katika miaka ya tisini. Aidha Park aliingia madarakani mwaka wa 2013, na cbaada ya miaka minne akavuliwa madaraka yote kufuatia miezi kadhaa ya maandamano ya umma ambayo yalifanywa na mamilioni ya watu.