1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makundi ya wazalendo wa kizungu yanachipukia Marekani

Admin.WagnerD16 Agosti 2017

Kizazi kipya cha makundi ya wazalendo wa Kizungu kinachipukia chini ya utawala wa rais wa Marekani Donald Trump anayehimiza juu ya utukufu wa Marekani kwanza.

https://p.dw.com/p/2iKNs
USA Virginia Charlottesville - Ausschreitungen nach Demonstrationen
Picha: Reuters/J. Roberts

Maandamano makubwa yaliyopeleka kifo cha mwanamke mmoja katika mji wa Charlottesville, jimbo la Virginia nchini Marekani yamewashtusha Wamarekani kupitia vidio katika televisheni iliyoonyesha takriban wanazi mambo leo elfu moja na Wamarekani wanaotukuza Wamarekani Weupe wakilindwa na wanamgambo waliokuwa na silaha.

Wakihimizwa na Rais Donald Trump na kuchochewa na mitandao ya kijamii, kizazi kipya cha wafuasi wenye itikadi kali kinachipukia na kukita mizizi, kikiundwa na kikundi cha vijana weupe wenye ghadhabu walio na shauku ya kutumia hofu ya uhamiaji wa Walatino, wafuasi wa itikadi kali ya Kiislamu, kupungua kwa idadi ya watu weupe Marekani na mabadiliko ya kitamaduni yaliyosababishwa na utandawazi.

Wachambuzi wanasema makundi haya huenda yakawa na wanachama takriban elfu kumi na wafuasi wanaokaribia laki moja.

Wamechukua ngome za zamani za makundi ya Wamarekani weupe wanaofuata siasa kali za kizalendo na  kuzidhibiti. Ngome hizo zilimilikiwa na Wamarekani waliopinga wageni, walikuwa wapinzani wa serikali na waliendeleza uanaharakati wa ufashisti ikiwemo kundi la kidini la Ku Klux Klan KKK ambalo wafuasi wake wamepungua.

Licha ya jitihada za muungano wa mshauri wa Trump Steve Bannon, mwenye ushawishi mkubwa, vuguvugu hilo la wanaofuata nadharia za siasa kali za kizalendo limegawanyika wasiweze kukubaliana juu ya itikadi sawa, na malengo na mbinu za kuyakomesha machafuko na uhasama.

Hata hivyo hali hii inaweza kubadilika.

Kuongezeka kwa wimbi la vijana ambao wana itikadi kali za kizalendo kunaimarisha makundi hayo.

USA Virginia Charlottesville - Ausschreitungen nach Demonstrationen
Maandamano ya Charlottesville, MarekaniPicha: picture-alliance/dpa/ZUMA Wire/G. Nakamura

Malengo ya makundi ya siasa kali za kizalendo Marekani

Makundi ya siasa kali za kizalendo yanapigania utamaduni wa wamarekani weupe na kupinga maswala ya wageni kuingia na kuchafua utamaduni wa marekani na watu kutangamana na tamaduni mbali mbali.

Wanapigania makundi sio ya wamarekani weupe na kuunga mkono haki sawa kwa wanawake, mashoga na vilevile makundi ya watu wachache.

Makundi kadha wa kadha ya wamarekani weupe wenye misimamo mikali ya kizalendo walishiriki kwenye machafuko ya Charlottesville.

Mkutano wa siku ya Jumamosi iliyopita, uliongozwa na Richard Sperker ambaye taasisi yake ya kitaifa ya kutoa ushauri imejitolea kulinda urithi, utambulisho na mustakabali wa watu wa Ulaya wanaoishi Marekani.

Makundi aliyoyaalika ni ya wanazi mambo leo, na wazungu wa siasa kali za kizalendo kama vile Vangurd America ambalo wanachama wake walipiga kelele wakisema "damu na mchanga" maneno yaliyotumiwa zamani na wafuasi wa Hitler miaka ya thelathini.

Kundi la Identity Europa linapigania ubepari wa Wazungu na kujitenga na watu wa nchi nyengine pamoja na chama cha Traditionalist Wokers Party kinachounganisha nembo ya manazi na nadharia ya wakristo weupe pekee, makundi haya yote yanawapinga mayahudi.

Kundi maarufu lilolishiriki machafuko ya Charleston ni "Oath keepers" lililoundwa na wanachama wa zamani wa jeshi la Marekani kuilinda katiba.

Kuwepo kwa wafuasi wa makundi ya siasa kali za kizalendo kuibua wasiwasi nchini Marekani.

Mwandishi: Fathiya Omar/Afpe

Mhariri: Mohammed Khelef