1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la Afrika la mataifa laanza Angola

8 Januari 2010

Misri watatetea taji lao Luanda ?

https://p.dw.com/p/LOs2
Bendera ya wenyeji Angola kupepea viwanjani.Picha: AP Graphics/DW Fotomontage

Miezi 6 kamili kabla firimbi kulia huko Afrika kusini, kuanzisha Kombe la dunia la FIFA 2010,firimbi italia kesho mjini Luanda,Angola, kuanzisha kinyan'ganyiro cha kombe la Afrika la mataifa. Jumla ya timu 16 zinaania Kombe hilo kati ya Januari 10 hadi 31. Miongonmi mwa timu hizo 5 ni zile zitakazoania Kombe la kwanza la dunia barani Afrika:Kamerun,Ghana,Ivory Coast,Nigeria na Algeria.

Mabingwa mara 6 -Misri,wamepania kuvaa taji hili kwa mara ya 3 mfululizo na kufuta machozi kwa kutokwenda Afrika Kusini kwa Kombe la Dunia.Misri, ilitolewa na Algeria. Dimba lakini, litafunguliwa kesho jioni mjini Luanda na wenyeji Angola wakinyoana na Mali , kabla siku ya pili yake Tembo wa Ivory C oast wakiongozwa na nahodha wao Didier Drogba hawakuingia uwanjani huko Kabinda kwa zahama za kundi B na Burkina Faso.

Mabingwa watetezi (mafiraouni) Misri,watabidi kuufanya ufiraouni wao wote wa dimba kuzima changamoto za timu 5 zinazowakilisha Afrika katika Kombe lijalo la dunia zilizopania kuwavua taji. Miongoni mwao ni Algeria, ile timu ilioichezesha Misri kindumbwe-ndumbwe na mwishoe, kuizika mjini Khartoumna nje ya kombe la dunia.

Wenzake Algeria katika Kombe la dunia mbali na Bafana Bafana,Afrika kusini isioshiriki katika Kombe hili,simba wa nyika Kamerun na nahodha wao samuel Eto-o,Ghana na Michael Essien pamoja na Corte d' Iviore ikiongozwa na Didier Drogba billa kuwasahau Super Eagles-Nigeria, kuondoka na Kombe Luanda, ni kutoa salamu kwa mashabiki wa nyumbani na wa nje kwamba, wanakusudia pia kutamba katika Kombe la dunia.

Kocha wa Nigeria, Shaibu Amodu, anakumbusha " Sisi ni taifa kuu la dimba barani Afrika tukiwa na maarifa ya kucheza dimba katika daraja ya juu barani Ulaya."

Nahodha wa "Black Stars -Ghana" Michael Essien, ameandika nae katika mtandao wake: "kombe la Afrika kama desturi , litakuwa changamoto kali, lakini timu yetu ina imani na uwezo wake na itapigana hatua zote hadi finali."

Sehemu kubwa ya mastadi katika Kombe hili la Afrika nchini Angola, wanazichezea klabu mbali mbali za ulaya,kuanzia Premier League,Uingereza, la Liga Spain, Ligi ya Ufaransa,Serie A,Itali na bila kuisahau Bundesliga.

Mabingwa wa ulaya FC Barcelona,Real Madrid,Inter Milan na Juventus,zajiunga na vilabu kadhaa vya ulaya vinavyobidi kuendelea na Ligi zao bila ya mastadi wao kutoka Afrika.Na hii, imezusha mabishano makubwa na CAF-Shirikisho la dimba la Afrika.

Angola, mwenyeji imetia raslimali kubwa katika miundo-mbinu kama barabara na viwanja ili kuandaa kombe hili kwa timu 16.Viwanja 4 vipya huko Luanda,Benguela,Cabinda na Lubangovimejengwa.Viwanja vyote hivyo 4 vilifunguliwa tu wiki iliopita na bado havikujionea changamoto.

Shirikisho la dimba la Afrika CAF,linakisia kwamba Angola, wenyeji wa dimba linaloanza Jumapili kwa mpambano kati yao na Mali, imetumia dala bilioni 1 kwa matayarisho,miaka 7 tu tangu nchi hii kutoka vita vya kienyeji.

Mwandishi:Ramadhan Ali /RTRE/AFPE

Uhariri: Aboubakry Liongo