1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la klabu bingwa Afrika na nani kuibuka bingwa wa Wimbeldon ?

25 Juni 2007

Kombe la klabu bingwa barani Afrika lilikuwa uwanjani -mabingwa Al Ahli walitamba 2:0 mbele ya Al Hilal ya Sudan. Mashindano ya ubingwa wa tennis ya Wibledon yaanza leo.Na Ufaransa yaipiku Ujerumani katika ubingwa wa Ulaya wa riadha huko Munich.

https://p.dw.com/p/CHbs

Katika kinyan’ganyiro cha kombe la klabu bingwa barani Afrika- FAR Rabat ya Morocco- yalazwa bao 1:0 na Etoile Sahel ya Tunisia.

Mabingwa Al Ahli ya Misri, waiitimua nje Al Hilal ya Sudan kwa mabao 2-0.

Roger Fedrer wa Uswisi, ajiwinda kutetea taji lake la wimbledon hii leo.Na nchini Kenya, ilikua zamu ya wanariadha- wake kwa waume- kutamba katika mbio za marathon za hifadhi ya mbuga ya wanayam:

Katika kombe la klabu bingwa barani Afrika,mabingwa Al Ahli ya Misri,waliikomea Al Hilal ya Sudan dakika 5 za mwisho mabao 2:0 mjini Cairo.

Flavio na Osama Hosni waliifutia aibu Al Ahli walipotia mabao hayo dakika za mwisho .Al Ahli ina kiu cha kutwaa ubingwa wa Afrika kwa mara ya tatu mfululizo.Bao la dakika ya 85 alilotia Flavio lilikua farja kubwa kwa mashabiki wa Al Ahli ambao hodi hodi zao za mara kwa mara katika lango la Al hilal hazikuitikiwa.Sasa Al Ahli inaongoza kundi B baada ya Esperence ya Tunisia na ASEC Abidjan ya Ivory Coast kutoka suluhu 0:0 mjini Tunis jumamosi.

Katika kundi jengine mahasimu 2 wakubwa wa Afrika kaskazini FAR Rabat ya Morocco iliikandikwa Etoile du sahel ya Tunisia bao 1:0.

Timu za kanda ya Ulaya zinazoania tiketi ya Kombe lijalo la dunia 2010 nchini Afrika Kusini zitagawanywa makundi 8 kila moja likiwa na timu 6 na kundi moja likiwa na timu 5 tu-hii ni kwa muujibu wa UEFA-shirikisho la dimba la Ulaya.

Kati ya timu 53 za UEFA ,13 zitawakilishwa bara hilo katika kombe la dunia la tim u 32 la kwan za mara ijayo kuandaliwa barani afrika.Washindi wa makundi hayo 9 ya Ulaya watakata tiketi zao moja kwa moja na timu 8 bora kabisa zilizomaliza nafasi ya pili kwenye makundi hayo zitaania nafasi zao kwa kucheza nyumbani na nje kuania nafasi 4 zilizosalia.

RIADHA:

Katika mashindano ya riadha ya ubingwa wa Ulaya mjini Munich,Ufaransa kwa mara nyengine imetoroka na taji la upande wa wanaume huku Ujerumani ikifuata nafasi ya pili wakati Russia kwa mara nyengine imetamba upande wa wasichana.

Hii ni mara ya 11 kwa warusi kutwaa taji.Licha ya kubatilishwa ushindi wao katika mbio za kupokezana za mita 400X4,wasichana wa Russia walitoroka na taji baada ya kukusanya pointi 127 huku Ufaransa ikija nafasi ya pili kwa pointi 107 na wasichana wa Ujerumani wakibidi kuridhika na nafasi ya tatu nyumbani.

Katika changamoto ya wanaume, kinyan’ganyiro cha ubingwa kilikua kikali mno kati ya wanariadha wa Ufaransa na wa Ujerumani.Mwishoe,lakini Ufaransa na Ujerumani zilimaliza sawa kila upande pointi 116.Ufaransa lakini ilipewa taji kwa kuwa ilitamba zaidi katika kunyakua nafasi za pili kuliko ilivyofanya Ujerumani.

Katika medani ya Tennis,leo mashindano ya Wimbledon yaanza huku bingwa wa mwaka uliopita mswisi Rogedr Federer akijiandaa kutwaa taji hilo kwa mara ya 5 mfululizo.Katika safu ya wasichana bingwa wa mwaka uliopita mfaransa Amelie Mauresmo atakuwa uwanjani kesho akipambana na muamerika Jamea Jackson.Dada wawili akina Williams watampa changamoto kwa mara nyengine tena.