1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la mashirikisho laanza kesho Johannesberg

12 Juni 2009

Afrika Kusini yafungua dimba na Misri-mabingwa wa Afrika.

https://p.dw.com/p/I841
Logo Kombe la Dunia 2010 Süd Afrika

Firimbi italia kesho mjini Johannesberg,kuanzisha kinyanganyiro cha Kombe la mashirikisho-Confederations Cup-kombe linalofungua pazia la Kombe la Dunia,Juni mwakani na la kwanza barani Afrika.Jumla timu 8 zinashiriki pamoja na hizo dola kuu za dimba,mabingwa wa dunia-Itali; mabingwa wa Amerika kusini-Brazil,mabingwa wa Ulaya-Spian.

Kwa mashabikiwa afrika lakini, macho yatakodolewa kesho mpambano wa ufunguzi baina ya wenyeji-Bafana Bafana au Afrika kusini na mabingwa wa Asia-Iraq.Iraq imeahidi msangao mwengine kama ilivyofanya ilipotoroka na Kombe la Asia hadi Baghdad.

Nae kocha wa mabingwa wa Afrika -"mafirauni wa Misri"-Hassan Shehata,ameipelekea salamu Brazil kuwa keshokutwa jumatatu itakiona "kilichomtoa kanga manyoya".

Kwa mashabiki wa riadha:muethiopia Kenenisa Bekele na mrusi Yelena Isinbayeva wanakitapia tena kitita cha mwaka huu cha dalya milioni 1 cha Golden League wakiteremka uwanjani kesho katika uwanja wa Olimpik wa Berlin.

Baada ya wanariadha kuingia uwanjani katika duru ya kwanza ya Goldean-League mjini Berlin, kesho,kuania kile kitita cha dala milioni 1 kwa kushinda katika mbio zote za miji 6 ,macho ya mashabik iwa dimba ulimwenguni yatakodolewa mjini Johannesberg,Afrika kusini:

Wenyeji Bafana Bafana wanafungua dimba na mabingwa wa Asia Iraq kuania Kombe la mashirikisho-mwaka kamili kabla kuanza Kombe la dunia la FIFA.

Kinyanganyiro hiki amesema hivi punde rais wa FIFA Sepp Blatter, ni muhimu sana kujua vipi Kombe la dunia mwakani litakavyokwenda.Na ndio maana amesema, hua ndaliwa mwaka kabla kombe la dunia kuanza.

Ushindi kesho kwa mabingwa wa Asia-Iraq dhidi ya wenyeji Bafana Bafana,

moja kati ya timu 2 zinazowakilisha Afrika mbali na mabingwa Misri, utazusha shangwe na shamra-shamra nyengine huko Baghdad.Kwa Afrika kusini utazima vishindo na kelele za mazumari yao ya kienyeji.

"Simba wa Mesopotamia"-kama timu ya Taifa ya Iraq inavyoitwa, hawatacheza katika Kombe lijalo la dunia na kwahivyo, wameazimia kunguruma kweli katika pori la Afrika katika Confederations Cup.Iraq inakabiliwa na mlima mrefu wa kupanda katika kundi A linalojumuisha mabingwa wa ulaya Spian na New Zealand.Spain ndio iliopo kileleni mwa ngazi ya FIFA wakati huu kuwa ni "timu bora duniani" na wanapigiwa upatu hata kutwaa Kombe la dunia mwaka ujao.

Kwa upande mwengine,Bafana Bafana wangali wanayumbayumba baada ya kuachwa mkono na kocha wao mbrazil Alberto Parraira na kupigwa kumbo nje ya finali za kombe lijalo la Afrika la mataifa nchini Angola.Licha ya ushindi wao wa bao 1:0 juzi dhidi ya Poland, Bafana Bafana, bado hawatazamiwi kufua dafu na kulibakisha Kombe hili nyumbani ili kutoa salamu kwa dunia kuwa mwaka ujao, ni "mwaka wa Afrika".

Matumaini ya Iraq yako mabegani mwa kocha wao mpya Bora Mulutonivic,msabia alieziongoza Mexico,Costa Rica,Marekani na Nigeria hadi duru ya pili ya Kombe la dunia. Mpambano wa kesho utaoneshwa kwa wairaqi katika mapazia 3 makubwa kabisa mjini Baghdad na pengine hadi qasri la "Haroun Rashid".

Changamoto kali iko kundi B hapo jumatatu ambapo mabingwa wa Amerika Kusini-Brazil, watafungua dimba na mabingwa wa Afrika- Misri.Wengine katika kundi hili ni mabingwa wa dunia Itali,Marekani na Misri.

Kocha wa "mafiraouni" -gwiji la dimba Hassan Shehata, ameambia timu yake "mabingwa wa Afrika" kuwa wasiwaogope Brazil na mastadi wao akina Kaka na Robinho.Kombe hili la mashirikisho ambalo mabingwa wake ni Brazil walioikomea Argentina mabao 4-1 katika finali hapa Ujerumani 2005,lilianzishwa miaka 10 iliopita ili kufungua pazia la Kombe la dunia.

Ama katika medani ya riadha,kinyanganyiro cha kuania kitita cha dala milioni 1 cha mashindano ya Golden League,kinaanza kesho alaasiri katika Uwanja wa Olimpik wa Berlin-kituo cha mashindano ya ubingwa wa riadha ulimwenguni hapo Augusti,mwaka huu.Majina ya wanariadha 2 daima hutajwa upande wa wanaume na wanawake kuhusu nan i atatoroka na kitita hicho.Mwaka jana lakini ilikua msichana wa Kenya,bingwa wa olimpik wa mita 800 Beijing,Pamela Jelimo aliefuata nyayo za mwamamsubiji,Maria Mutola alietwaa kitita hicho 2003 .Ni wanariadha 3 tu katika historia ya Golden League wametoroka na kitita kizima bila kubidi kugawana na wenzao.Mbali na waafrika hao 2 alikuwa mrusi Tatyana Lebedeva .Mara hii ,itakua zamu ya Kenenisa Bekele wa Ethiopia au Usain Bolt -bingwa wa rekodi ya dunia ya mita 100 kutoka Jamaica au hata Yelena Isinbayeva kuondoka na kitita hicho?

Muandishi: Ramadhan Ali /DPAE/RTRE

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman