1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kongamano la kiuchumi la nchi za Latin Amerika mjini Rio

Oumilkher Hamidou14 Aprili 2009

Viongozi wa mataifa ya Latin Amerika wakutana na wawakilishi wa jamii kusaka njia za kuufumbua mgogoro wa kiuchumi

https://p.dw.com/p/HWlj
Rais Lula da Silva wa BrazilPicha: AP

Kongamano la siku tatu la kiuchumi la mataifa ya kusini mwa bara la Amerika,linaanza hii leo mjini Rio de Janeiro nchini Brazil.Kongamano hilo linawaleta pamoja wawakilishi mia kadhaa kutoka sekta za kisiasa,kiuchumi na kijamii kwa lengo la kubuni hali bora ya siku za mbele.Mgogoro wa sasa wa kiuchumi ulimwenguni unatazamiwa kugubika kongamano hilo.Rais Lula da Silva wa Brazil,Alvaro Uribe wa Columbia na Oscar Arias wa Costa Rica watajadiliana na wataalam wa kiuchumi toka mataifa karibu 40,namna ya kulinusuru eneo la Latin Amerika na mgogoro wa kiuchumi unaoisibu dunia.

Kongamano la kimataifa la uchumi kwa nchi za Latin Amerika linaloanza leo,litamalizika April 16 ijayo,siku moja tuu kabla ya mkutano wa kilele wa nchi za Amerika huko Trinidad na Tobago ambako viongozi wa taifa,mfano Barack Obama wa Marekani na wenzake watajaribu kutafuta ufumbuzi wa matatizo yanayoikumba sehemu hiyo ya magharibi ya dunia yetu.Na huko pia juhudi za kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kiuchumi ni miongoni mwa mada zitakazojadiliwa.Viongozi watatilia maanani hali mahsusi ya nchi za Latin Amerika.Kwasababu madhara ya mgogoro huo kwa nchi za Latin Amerika ni ya aina nyengine kabisa.

"Tatizo halisi la Latin Amerika,sio kwamba bara letu ni maskini kupita kiasi,lakini pia kwasababu hali hazilingani hata kidogo.Tunajikuta katika mgogoro,lakini asili mia 90 ya pato la ndani la kimkoa limefikia kiwango cha uwekezaji.Hii ni hali ya aina pekee.Nnazungumzia kuhusu Brazil,Mexico,Colombia,Peru na Chile.Mfumo wa Benki wa nchi zote hizo unathamini zaidi mtaji kupita nchi za magharibi;na soko la ndani la nchi hizo linaashiria ukuaji wa kiuchumi ambao ni kinga dhidi ya kupungua shughuli za biashara ya nje wakati wa mgororo."


Emilio Lozoya ni mwenyekiti wa kongamano la kiuchumi kwa nchi za Latim Amerika.Katika kongamano hili la nne anapanga kuhamasisha mjadala wa kina kutoka wawakilishi 550 wa sekta za kiuchumi,kisiasa na wawakilishi wa mashirika ya huduma za jamii.


Kwanza,kwa kadiri gani eneo hilo la Latin Amerika lenye hali tofauti za kiuchumi,linaweza kuathirika na mgogoro huu wa kiuchumi.Nchi mfano Brazil inayotegemea shughuli za kilimo,haitikiswi sawa na mgogogoro huo kama nchi mfano wa Mexico ambayo shughuli zake za kibiashara zinaitegemea zaidi Marekani.


Pili watajadiliana jinsi makampuni yatakavyoweza kutia njiani kile kijulikanacho kama "mfumo wa maendeleo ya kijani".Nchi za Latin Amerika zinaweza kufaidika na rasli mali waliyo nayo.Na zaidi kuliko yote wawakilishi watajishughulisha na suala kwa jinsi gani sekta ya kibinafsi inaweza kuchochea ukuaji wa kiuchumi.


Si suala la bahati nasibu kwamba Brazil imechaguliwa kuwa mwenyeji wa kongamano hilo la kimataifa la kiuchumi kwa mwaka 2009.Nchi hiyo inaangaliwa kama mfano wa kuigizwa.Sekta yake ya fedha ni imara.Na hata kama shughuli zake za kiuchumi zinaathirika kama kwengineko,lakini soko la ndani limezidi kukua miaka ya hivi karibuni na kuna kizazi kipya kilichochomoza ambacho kiu chake cha matumizi ni muhimu katika kuinua uchumi.

Mwandishi Krieger/Hamidou Oummilkheir

Mhariri Abdul Rahman