1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vijana wa Afrika na Ulaya wajadili uwajibikaji na Umoja

Angela Mdungu
7 Mei 2019

Vijana wa nchi za kiafrika zinazoshiriki katika kongamano la kujadili uzalendo na umoja wametakiwa kutumia nafasi zao kuwafikia vijana wengine ambao hawapati nafasi ya kushiriki katika programu za kubadilishana uzoefu

https://p.dw.com/p/3I4yK
AGYI Symposium
Picha: DW/S. Fröhlich

Akizungumza katika kongamano la siku tatu linalofanyika mjini Bonn nchini Ujerumani, mjumbe maalumu wa Umoja wa Afrika anayehusika na masuala ya vijana Aya Chebbi amesema, pamoja na changamoto  ambazo umoja wa Afrika unakumbana nazo katika kuwapa vijana jukwaa la kubadilishana uzoefu, lengo kubwa la umoja huo ni kusaidia kuwafikia vijana popote walipo hasa walio vijijini, pembezoni na ambao hawapati taarifa kutokana na kukosa huduma za mtandao wa mawasiliano wa intaneti.

"Nadhani kwa kizazi chetu ni muhimu zaidi kuvuka mipaka na tofauti mbalimbali. Ni muhimu kwa kuwa kizazi chetu ni cha ulimwengu ambao wanaamini katika dunia isiyo na mipaka.''

Mtandao wa Intaneti kikwazo katika kusambaza taarifa

Chebbi amesema vijana wanatafuta uhuru na kujieleza kama na ndio maana hivi sasa wamehamia kwenye jukwaa la mtandao kwa sababu ni mahali wanaweza kupata nafasi ya kujadili kwa uwazi.

AGYI Symposium
Kuanzia kushoto, Karin Küblböck (Mwongoza mjadala, Aya Chebbi (Mjumbe maalumu wa vijana wa umoja wa nchi za kiafrika), Josseline da Silva Gbony (Balozi wa Benin nchini Ujerumani) Jean Daniel Balme (Frace Voluntaires) na Dr. Jens Kreuter (Mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya Engagement Global)Picha: DW/A. Mdungu

Mwakilishi huyo wa vijana wa umoja wa Afrika ameongeza kuwa, pamoja na vijana kufunguliwa dirisha la dunia kupitia mtandao, bado vijana wengi wa kiafrika hawapati mtandao kwani asilimia 70 ya watu barani Afrika hawana huduma hiyo, jambo linalofanya upatikanaji na usambazaji wa taarifa kutokuwa na usawa duniani.

Mshiriki wa kongamano hilo kutoka Tanzania Lidya Richard Maika amesema kupitia kongamano hilo amejifunza mengi ikiwemo namna nchi yake inavyoweza kushirikianana nchi za nyingine za Afrika kufanya programu za mabadilishano ya vijana kupitia taasisi anayoifanyia kazi.

Kongamano hilo la vijana linakamilika siku ya Jumatano, na nchi za Benin, Tanzania, Afrika ya kusini zinashiriki kama nchi za majaribio za programu ya kubadilishana uzoefu ambayo itakamilika mwaka 2020 na kuandaliwa na Taasisi ya Engagement Global kwa kushirikiana na France Volontaires, Taasisi ya ushirikiano ya Norway NOREC chini ya ufadhili wa wizara ya maendeleo na ushirikiano wa kiuchumi ya Ujerumani.