1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kuanza vita vya pili vya dunia

1 Septemba 2009

Kanzela Merkel kwenda Poland

https://p.dw.com/p/JMzs
Rais Lech Kaczynski wa Poland katika kumbukumbu ya 70 ya vita vya pili vya duniaPicha: AP

Leo ni siku viliporipuka vita vya pili vya dunia miaka 70 iliopita : Viongozi kutoka pande zote mbili zilizopigana vita hivyo, wamekusanyika kuikumbuka siku hii pale manuwari ya kijerumani ilipoihujumu kambi ya wanamaji ya Poland katika pwani ya baltic.Alfajiri ya leo saa 10.45 barabara -saa za ulaya ya kati, Rais Lech Kaczynski na waziri wake mkuu Donald Tusk ,walijiunga na wajumbe wa kibalozi na wakongwe wa vita vya pili vya dunia kuwakumbuka wahanga katika vita vile vilivyochukua maisha ya watu si chini milioni 50 barani ulaya pamoja nao mayahudi milioni 6.

Katika hafla zitakazofanyika baadae leo ,viongozi kutoka mataifa 20 kati yao Kanzela Angela Merkel wa Ujerumani na waziri mkuu wa Russia,Wladmir Putin,watajiunga nao kuikumbuka historia ya vita vilivyomwaya damu nyingi kabisa na ambavyo masalio yake yanaugawa ulimwengu hadi leo.

Waziri mkuu wa Poland alisema na ninamnukulu,

"Tupo hapa kujikumbusha nani katika vita vile alikua mchokozi,nani aliekuwa mateka ,kwani bila kukumbuka kwa dhati si ulaya wala poland na si ulimwengu uttweza kuishi katika hali ya usalama."

Hafla za ukumbusho huu wa kuanza kwa vita vya pili vya dunia, zinafanyika huko Gdansk-zamani Danzig na 1939 ndiko ilipokuwapo kambi ndogo ya wanamaji wa Poland.

Polen Deutschland Angela Merkel bei Donald Tusk in Danzig
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Waziri Mkuu wa Poland Donald TuskPicha: AP

Kwa wapoland ,kambi hiyo ni alama ya upinzani mkali uliooneshwa na mashujaa wa Poland.Kwani, wanamaji wake 180 walizuwia kutekwa kwa kambi hiyo kwa muda wa siku 7 dhidi ya kikosi cha askari 3.500 wa Ujerumani.

kambi hiyo kwa kweli ilihujukiwa siku kama leo septemba mosi,1939 na manuwari ya kijerumani "Schleswig-Holstein" ambayo ilijigamba imewasili hapo kwa ziara ya kirafiki.

Manuwari hiyo ikaamriwa na dikteta wa Ujerumani ya Manazi ,Adolf Hitler kufyatua risasi ifikapo alfajiri ya saa 10.45.Na huo ni wakati unaoangaliwa ni mwanzo wa vita vya pili vya dunia.

Kanzela Angela Merkel, amesema leo kuwa nchi yake imesababisha "maafa yasio na mwisho" kwa kuanzisha vita vya pili vya dunia,lakini pia alikumbusha hatima ya wakaazi wa asili ya kijerumani waliotimuliwa makwao huko baada ya kumalizika vita.

Kanzela alisema na ninamnukulu,

"Ujerumani iliishambulia Poland,Ujerumani ilianzisha vita vya pili vya dunia.Tulisababisha maafa yasio na mwisho ulimwenguni.Watu milioni 60 waliuwawa ndio matokeo yake."

-alisema Kanzela Angela Merkel katika TV siku hii ya ukumbusho wa miaka 70 tangu kuanza vita vya pili vya dunia.

Lakini kutimuliwa kwa wajerumani milioni 12 kutoka sehemu zilizokua Ujerumani zamani na Poland ya leo pia haikuwa haki, alisema pia Kanzela Merkel.

Bibi Merkel,aliezaliwa baada ya vita vya pili vya dunia hapo 1954 na aliekulia Ujerumani Mashariki ya kikoministi,atahudhuria baadae hii leo huko Poland makumbusho ya leo.Kabla ya kuondoka alisema:

"Nimefurahi sana leo kama Kanzela wa Ujerumani nikifuata nyayo za makanzela walionitangulia,ninakwenda Poland kama mshirika na katika hali ya urafiki."

Muandishi: Ramadhan Ali

Uhariri: Othman Miraji