1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kundi la ADF lafanya shambulizi na kusababisha DRC

John Kanyunyu24 Septemba 2021

Waasi wa kundi la ADF waliushambulia mji mdogo wa kibiashara wa Komanda katika wilaya ya Irumu mkoani Ituri kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, usiku wakuamkia Ijumaa. Matokeo ya awali na ambayo hayajathibishwa na jeshi, yanaonyesha kuwa watu zaidi ya kumi waliouawa na nyumba kuchomwa moto.

https://p.dw.com/p/40ncv

Shambulizi hilo linatokea wakati serikali ya Kongo ikitangaza kwamba hali ya usalama inaendelea kuboreka katika eneo hilo. 

Shambulizi hilo la hivi karibuni limefanyika katika mji mdogo wa kibiashara wa Komanda, kwenye moja wapo ya kata za mji huo, wakati shughuli za kibiashara zilipokuwa bado zinaendelea.

Waliouawa ni watu waliokuwa wanajaribu kuokoa maisha yao, kwa mjibu wa duru toka baadhi ya wakaazi wa Komanda waliozungumza na DW kwa njia ya simu.

Na akizungunza na idhaa hii, mjumbe maalumu wa gavana wa mkoa wa Ituri katika mji mdogo wa Komanda Moïse Utondi alisema, kuwa hadi sasa ni vigumu kujuwa idadi kamili ya watu waliouawa, kwani bado hali ni ya hekaheka. 

Raia wa Kongo wauawa licha ya kutangazwa hali ya dharura

"Ni waasi wa ADF waliotokea sehemu ya Mlima Hoyo ambao walishambulia Komanda kupitia kata moja mashariki ya mji huo. Waliwauwa watu na kuchoma pia nyumba. Tangu saa kumi na mbili jioni hadi saa tano usiku milio ya risasi ilikuwa ikisikika na kwa sasa watu wanaendelea kukimbia na matokeo ya awali bado kujulikana," amesema Moïse Utondi délégué .

Kabla ya kuushambulia mji wa Komanda, waliwateka nyara wakaazi tisa wa kijiji cha Mount Hoyo, kama anavyotueleza Christophe Munyanderu, mwenyekiti wa shirika la kutetea haki za binaadamu katika wilaya ya Irumu CRDH.

"Kuna wakaazi tisa waliotekwa nyara na kwa sasa raia wa Mont Hoyo ambao baadhi wamewasili Ngombenyama pale wengine wakikimbilia Komanda wakihofia usalama wao. ADF waliwasili katika eneo hilo kutokea katika tundu la Jiwe kubwa la Mount Hoyo,"  amesema Christophe Munyanderu.

ADF ambao wameonekana kupanua maeneo ya vitendo vyao vya uhalifui katika mikoa miwili sasa, yaani Kivu ya Kaskazini pamoja na Ituri.
ADF ambao wameonekana kupanua maeneo ya vitendo vyao vya uhalifui katika mikoa miwili sasa, yaani Kivu ya Kaskazini pamoja na Ituri.Picha: Alexis Huguet/AFP/Getty Images

Waasi wa ADF wauwa tena mashariki mwa DRC

Habari toka Komanda zaeleza  kuwa wakaazi wa mji huo wamekuwa wakiuhama, na kukimbilia mahala wanakohisi kuna usalama. 

Kushambuliwa kwa mji wa kibiashara wa Komanda katika mkoa wa Ituri, kunakinzana na matamshi ya rais Félix Antoine Tshisekedi kwenyi baraza kuu la Umoja wa mataifa, alikosema kwamba hali ya usalama inaendelea kuboreka katika mikoa ya Kivu ya Kaskazini pamoja na Ituri, ambako alitangaza hali ya dharura. 

Komanda ndio makao makuu ya jeshi katika operesheni dhidi ya ADF katika wilaya ya Irumu, na mji huo unahifadhi ma mia ya magari yanayosubiri kusindikizwa na jeshi la Congo pamoja na lile la Umoja wa mataifa Monusco, ili kwenda Beni na Butembo, kusini mwa wilaya ya Irumu.