1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Löw achagua kikosi chake cha mwisho

9 Juni 2014

Kocha wa Ujerumani Joachim Löw amekitaja kikosi chake cha mwisho. Marcel Schmelzer, Kevin Volland na Shkodran Mustafi wote hawatasafiri kushiriki katika dimba la Kombe la Dunia nchini Brazil.

https://p.dw.com/p/1CAsR
DFB Training in Düssledorf 31.5.2014
Picha: Getty Images

Baada ya kutoka sare ya magoli mawili kwa mawili na Cameroon katika mchuano wa kujipima nguvu mjini Mönchengdladbach Jumapili usiku, kocha Joachim Löw alichagua kikosi chake cha mwisho cha wachezaji 23 anachohisi kitarejea nyumbani na Kombe la nne la Dunia.

Mchezaji wa Borussia Dortmund Marcel Schmelzer, Shkodran Mustafi wa Sampdoria na Kevin Volland wa Hoffenheim ndio wachezaji watatu walioachwa nje katika kikosi hicho cha mwisho, na kuwapa chipukizi wa Dortmund Erik Durm, Christoph Kramer wa Gladbach na Matthias Ginter wa Freiburg fursa ya kutamba nchini Brazil. Kikosi cha Ujerumani kimeathirika na majeraha wakati wa maandalizi ya dimba hilo, na kimpa wakati mgumu Löw kufanya uteuzi wake. Kiungo wa Leverkusen Lars Bender aliachwa nje kwa ajili ya jeraha, na akajiunga na kakake katika orodha ya watazamaji tu. Huku Sami Khedira akiendelea kuimarika baada ya kupona jeraha lake, kujumuishwa kwa kiungo wa ulinzi Cristoph Kramer kunaonekana kuwa muhimu.

Deutschland Fußball WM Miroslav Klose im DFB-Trainingslager in Südtirol
Miroslav Klose ndiye mshambuliaji pekee aliyepewa jukumu la kuongoza mashambulizi ya UjerumaniPicha: DW/J. Weber

Kuchaguliwa beki wa kushoto Erik Durm kunashangaza ikizingatiwa kuwa amecheza mechi 19 pekee za ligi ya nyumbani – Bundesliga msimu huu. Anaonekana kupata sifa kumliko mwenzake wa Dortmund Marcel Schmelzer baada ya wasiwasi kuhusu hali ya Schmelzer kuendelea kukithiri wakati wa kambi yao ya mazoezi Tyrol Kusini, kaskazini mwa Italia.

Wakati kuachwa nje kwa Mustafi kulikuwa kumetarajiwa, Matthias Ginter wa Freiburg – ambaye alicheza katika nafasi ya kiungo mkabaji atafurahia kuchaguliwa. Kutemwa kwa Volland kuna maana kuwa Ujerumani ilimteua mshambuliaji mmoja pekee, Miroslav Klose – ambaye amefikisha umri wa miaka 36.

Kikosi cha Ujerumani cha Kombe la Dunia 2014:

Walinda lango: Manuel Neuer (Bayern Munich), Roman Weidenfeller (Borussia Dortmund), Ron-Robert Zieler (Hannover 96)

Mabeki: Erik Durm, Mats Hummels, Kevin Grosskreutz (all Borussia Dortmund), Per Mertesacker (Arsenal), Philipp Lahm, Jerome Boateng (both Bayern Munich), Benedikt Höwedes (Schalke)

Viungo: Lukas Podolski, Mesut Özil (both Arsenal), Bastian Schweinsteiger, Toni Kroos, Thomas Müller, Mario Götze (all Bayern Munich), Marco Reus (Borussia Dortmund), Andre Schürrle (Chelsea), Sami Khedira (Real Madrid), Matthias Ginter (Freiburg), Julian Draxler (Schalke), Christoph Kramer (Gladbach)

Mshambuliaji: Mirsolav Klose (Lazio)

Mwandishi: Sekione Kitojo/AFP
Mhariri: Mohammed Abdulrahman