1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Leverkusen yapanda hadi nafasi ya nne

Bruce Amani
2 Novemba 2020

Bayer Leverkusen iliandikisha ushindi wa tatu mfululizo kwa kuibwaga Freiburg 4 - 2. Lucas Alario alitupia mbili kambani na kuhakikisha kuwa Leverkusen inapanda hadi nafasi ya nne

https://p.dw.com/p/3klxy
Bundesliga Freiburg gegen Leverkusen | Lucas Alario
Picha: Alex Grimm/Getty Images

Bayer Leverkusen iliandikisha ushindi wa tatu mfululizo kwa kuibwaga Freiburg 4 - 2. Lucas Alario alitupia mbili kambani huku Nadiem Amiri na Jonathan Tah pia wakifunga na kuhakikisha kuwa Leverkusen inapanda hadi nafasi ya nne na pengo la pointi tatu dhidi ya vinara Bayern na Dortmund.

Wolfsburg ni timu nyingine ambayo haijapoteza mchezo mpaka sasa lakini ipo nafasi ya kumi baada ya sare ya 1 - 1 na Hertha Berlin katika mechi nyingine ya jana.

Augsburg imepanda hadi nafasi ya sita baada ya winga Andre Hahn kufunga mabao mawili ya dakika za mwisho katika ushindi wao wa 3 - 1 dhidi ya Mainz. "Tumefanya kazi nzuri sana kama timu, ulikuwa ushindi muhimu sana kwetu leo. Tulijua ungekuwa mchezo mkali kweli, na tungehitajika kukimbia sana, na kuyamudu mapambano ya mchezaji dhidi ya mwingine. Nadhani tulifanikiwa mwishowe. Pia tulicheza kandanda safi. Kwa hiyo, kwa jumla nadhani tulistahili ushindi."

Bundesliga 1. FC Köln v FC Bayern München | Jubel Gnabry
Bayern wamekamata usukani wa BundesligaPicha: Marius Becker/AFP/Getty Images

Imebaki wiki moja tu kabla ya mpambano wa miamba ya Bundesliga Bayern Munich na Borrusia Dortmund, na makocha Hansi Flick na Lucien Favre wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kuvibadilisha vikosi vyao wakati ili kupambana na mrundikano wa mechi za ligi lakini pia za ligi ya mabingwa Ulaya na za kimataifa.

Jumamosi, Bayern na Dortmund ziliiondoa RB Leipzig na kupanda kileleni mwa ligi zikiwa na pointi sawa kabla ya mchuano wao wa Der Klassiker wikiendi ijayo.

Munich iliwapumzisha Robert Lewandowski na Leon Goretzka wakati Dortmund ikimuweka pembeni muangamizaji wao Erlin Haaland ambaye alikuwa na matatizo ya goti. Bayern ilipata ushindi wa jasho wa 2 - 1 dhidi ya FC Cologne. Serge Gnabry alirudi kikosini na kuifungia Bayern bao "Tulifanya mambo kuwa magumu kwetu, hatukucheza kwa kushambulia vizuri leo. Tulitengeneza nafasi chache za kufunga kuliko inavyokuwa, tukapoteza mipira kiholela kwa hiyo Cologne wakarudi mchezoni na bila shaka wakapata motisha. Na hilo ndio lilikuwa tatizo letu leo.

Kocha wa Dortmund Favre aliwaleta wachezaji watano wapya kikosini katika mechi waliyoifunga Arminia Bielefeld 2 - 0. Katika mechi hiyo, mfungaji wa mabao yote mawili beki Mats Hummels alichechemea na kuondoka uwanjani baada ya kupata tatizo la msuli.

Leipzig ilifungwa 1 - 0 na Borussia Moenchengladbach ambayo sasa imekamata nafasi ya tano. Hannes Wolf ndiye aliyefunga bao la ushindi "Bila shaka hilo linakupa furaha kama mchezaji kwa sababu unaweza kutiwa motisha katika mechi kama hizi. Baada ya kuichezea Leipzig kwa mwaka mmoja na muda niliokuwa nao Ujerumani kwa ujumla, nilitaka kudhihirisha hilo wakati mmoja, bila shaka na leo imetimia na nna furaha kuhusu hilo."

Reuters, AFP, AP, DPA