1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Lijue kundi C la michuano ya Euro 2020

9 Juni 2021

Michuano ya mataifa ya Ulaya ya Euro 2020 inaanza Juni 11. Kundi C lina timu nne nazo ni Ukraine, Uholanzi, Austria na Macedonia Kaskazini.

https://p.dw.com/p/3ue98
EURO 2020 Fußball Qualifikation Mannschaft Niederlande
Picha: Dean Mouhtaropoulos/Getty Images

Ukraine, inashiriki michuano ya mataifa ya Ulaya kwa mara ya tatu sasa.

Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka 2012, 2016 na mwaka huu. Timu hiyo imekuwa katika fomu nzuri kuelekea michuano ya Euro baada ya kukosa kushiriki kombe la Dunia la mwaka 2018.

Hata hivyo, katika michuano ya mataifa ya Ulaya ya mwaka 2016, Ukraine iliingia kwenye rekodi baada ya kuwa timu pekee iliyobanduliwa nje ya michuano hiyo bila ya kuzoa alama yoyote wala kufunga hata bao moja.

EURO 2020 Fußball Qualifikation Mannschaft Ukraine
Timu ya taifa ya UkrainePicha: Srdjan Stevanovic/Getty Images

Kocha wake Andriy Shevchenko, zamani akitamba wakati akiichezea AC Milan, amekibadilisha kabisa kikosi cha sasa ikiwemo kuifunga Ureno ambayo ni bingwa mtetezi katika mechi zake za hivi karibuni. Ukraine inataraji kutumia uzoefu wa wachezaji Andriy Yarmolenko anayechezea West Ham United pamoja na winga wa Dynamo Kiev Victor Tsygankov.

Uholanzi ina uzoefu wa kushiriki michuano hii ya mataifa ya Ulaya, mara hii ikiwa ya kumi. Uholanzi ilishiriki michuano ya 1976, 1980, 1988, 1992, 1996, 2000, 2004, 2008, 2012 na mwaka huu.

Uholanzi ilishindwa kufuzu katika michuano iliyopita ya Euro na kombe la Dunia japo wakati huu inaingia ikiwa na matumaini ya kufanya vyema.

Bildergalerie | Fussballer vor dem Wechsel 2021
Staa wa Uholanzi Memphis DepayPicha: Norbert Scanella/imago images

Mashabiki wa Uholanzi wanahisi kikosi cha sasa chenye wachezaji wa haiba kubwa kama vile Memphis Depay, Matthijs de Ligt, Frenkie de Jong, Donny van de Beek, Georginio Wijnadum na Virgil van Dijk wana uwezo wa kuifunga timu yoyote ile.

Mara ya mwisho kwa Uholanzi kushinda taji la Ulaya ilikuwa ni mwaka 1988 wakati wa enzi za Marco van Basten, Ruud Gullit na Frank Rijkaard. Je, mwaka huu wataweza?

Austria inashiriki michuano ya Ulaya kwa mara ya tatu katika historia yao.

Kuanzia mwaka 2008, 2016 na mwaka huu. Timu hiyo ilimaliza ya pili katika kundi lao wakati wa mechi za kutafuta tiketi ya kufuzu kwa michuano hiyo.

Kocha wake Franco Foda ana wachezaji kadhaa wa kutegemewa akiwemo David Alaba aliyejiunga na Real Madrid hivi karibuni, Julian Baumgartlinger na Marko Arnautovic anayecheza soka la kulipwa nchini China.

Timu hiyo inataraji angalau kuvuka katika hatua ya makundi, ikiwa ni mara ya kwanza kushiriki katika michuano ya kimataifa tangu kombe la Dunia la 1982.

Macedonia Kaskazini. Hii ni mara ya kwanza kwa timu hii kushiriki michuano ya mataifa ya Ulaya.

EM-Qualifikation Georgien - Nordmazedonien, Jubel in Skopje
Mashabiki wa Macedonia Kaskazini washeherekea baada ya timu yao kufuzu kwa michuano ya Euro 2020Picha: Pixsell/imago images

Staa wao ni Goran Pandev anayechezea klabu ya Genoa nchini Italia. Pandev mwenye umri wa miaka 37 ndiye mchezaji mwenye uzoefu mkubwa timuni akiwa ameichezea timu yake ya taifa mara 117 na kufunga magoli 37. Mchezaji mwengine wa kutegemewa ni Ezgjan Alioski wa Leeds United.

Kiuhalisia inaonekana kama timu ndogo lakini katika soka lolote linaweza kutokea. Nani alidhani kuwa North Macedonia ingeifunga miamba Ujerumani ugenini katika mechi ya kutafuta tiketi ya kombe la Dunia mnamo mwezi Machi?

Ulikuwa ushindi ambao utasalia kumbukumbu miongoni mwa mashabiki wa North Macedonia. Wachambuzi wa soka wanatoa onyo dhidi ya yeyote atakayepambana na North Macedonia-ni timu yenye kustahili heshima!!!