1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maadhimisho ya kupigania haki za raia weusi Marekani

8 Machi 2015

Rais Obama amesema hatua kubwa imepigwa katika kuleta haki za raia wote nchini Marekani katika kipindi cha miaka 50 iliyopita. Hata hivyo ameeleza kwamba safari ya kuelekea kwenye haki kamili bado haijamalizika

https://p.dw.com/p/1EnFF
USA Selma 50. Jahrestag Blutiger Sonntag von 1965 Präsident Obama
Picha: Reuters/Jonathan Ernst

Obama ambae ni Rais wa kwanza mweusi nchini Marekani aliyatamka hayo katika maadhimisho ya mwaka wa 50 tokea polisi wa Marekani walipowashambulia kikatili hasa Wamarekani weusi waliokuwa wanafanya maandamano ya amani kwenye mji wa Selma katika jimbo la Alabama.

Polisi walifanya ukatili

Polisi walitumia virungu na mabomu ya kutoa machozi kuyazuia maandamano hayo. Katika hotuba yake Rais Obama aliwapongeza wanaharakati waliojitoa mhanga, miaka 50 iliyopita, kufanya maandamano ili watu weusi wapate haki zao. Amesema maandamano hayo ndiyo yaliyomfungulia njia ya kuingia Ikulu ya Marekani.

USA Selma Blutiger Sonntag von 1965
Polisi wakiwashambulia waandamanaji mwaka wa 1965Picha: picture-alliance/AP Photo

Licha ya kupigwa virungu walisonga mbele

Obama aliwaambia watu waliohudhuria maadhimisho ya mjini Selma kwamba, wamekwenda kuuenzi ujasiri wa Wamarekani wa kawaida, waliokuwa tayari kupigwa virungu,mabomu ya machozi, na kukanyagwa na farasi; na licha ya kuvunjwa mbavu, wanawake na wanaume hao walisonga mbele na maandamano. Obama amesema wanaharakati hao walisimama imara kama nyota ya kaskazi.

Rais Lyndon Johnson apitisha sheria

Kutokana na harakati hizo na zingine, Rais wa Marekani wa wakati huo Lyndon Johnson aliipitisha sheria ya kuwapa haki watu weusi ya kupiga kura.

Hata hivyo Rais Obama ameeleza kuwa sheria hiyo imo hatarini kwa mara nyingine, kwa sababu serikali inataka kuzikaza sukurubu za utaratibu wa kuwaandikisha wapiga kura. Obama aliuliza kwa nini sheria hiyo ihatarishwe, huku akitilia maanani kwamba, sheria hiyo ilitiwa nguvu upya na marais wa Republican, Ronald Reagan na George W Bush aliehudhuria madhimisho ya mjini Selma.

USA Selma 50. Jahrestag Blutiger Sonntag von 1965 Präsident Obama Ankunft Montogomery
Umati uliohudhuria maadhimisho ya Selma miaka 50 iliyopitaPicha: Reuters/Jonathan Ernst

Rais Obama amewataka wabunge 100 waliohudhuria maadhimisho ya mjini Selma wajiunge na wabunge wengine ili wailinde sheria inayowapa Wamarekeni wote haki ya kupiga kura. Katika hotuba yake Obama pia aligusia juu ya matukio ya hivi karibuni yaliyohusu kuuliwa Wamarekani weusi na polisi nchini Marekani.

Ubaguzi wa rangi bado upo

Matukio hayo yalisababisha maandamano na malamiko juu ya kuwepo rasmi kwa ubaguzi wa rangi wa kina kirefu.Obama ameeleza kuwa watu wanahitaji kuyafungua macho na nyoyo zao ili kujua kwamba historia ndefu ya ubaguzi bado inalipelemba taifa la Marekani. Amesema "tunajua kwamba safari yetu bado haijafikia mwisho" Ameeleza kuwa ushindi kamili dhidi ya ubaguzi bado haujapatikana.

Rais Obama pia alitilia maanani kwamba wabunge mia moja walikuwapo kwenye maadhimisho ili kuwaenzi wanaharakati waliokuwa tayari kufa ili kuilinda sheria ya kuwapa watu wote haki ya kupiga kura.

Mwandishi:Mtullya Abdu.afpe/rtre.

Mhariri: Bruce Amani