1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maafisa wa Rwanda wahukumiwa kifungo

14 Januari 2011

Hukumu hiyo imetolewa kwa maafisa wanne wa zamani wa Rwanda bila kuwepo kwao mahakamani, kwa madai ya kuhujumu usalama wa taifa.

https://p.dw.com/p/zxii
Rais wa Rwanda, Paul KagamePicha: picture-alliance/dpa

Mahakama ya kijeshi nchini Rwanda leo imewahukumu maafisa wanne wa zamani wa serikali kifungo kati ya miaka 20 na 24 gerezani baada ya kupatikana na hatia ya kutishia usalama wa nchi. Mahakama hiyo imewahukumu kifungo cha miaka 24 jela mkuu wa zamani wa majeshi, Jenerali Faustin Kayumba Nyamwasa na Meja Theogene Rudasingwa. Mkuu wa kijasusi wa zamani, Patrick Karegeya na Gerald Gahima, aliyekuwa mwanasheria mkuu, walihukumiwa kifungo cha miaka 20 jela.

Nyamwasa na Karegeya wanaishi uhamishoni nchini Afrika Kusini, huku Gahima na Rudasingwa wakiwa wanaishi uhamishoni nchini Marekani. Maafisa hao wameshitakiwa kutokana na madai ya kutishia usalama wa taifa, kutoa matamshi ya kukashifu na kufanya njama za jinai.

Msemaji wa jeshi, Luteni Kanali, Jill Rutaremara ameliambia shirika la habari la AFP kuwa mashtaka zaidi dhidi yao yatafuata. Amesema mashtaka mengine ikiwemo ugaidi pia yatafikishwa kwa mwendesha mashtaka mkuu wa serikali na kwamba bado wanachunguzwa. Hukumu hiyo imetolewa bila maafisa hao kuwepo mahakamani.