1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maalim Seif azikwa Pemba

Grace Kabogo
18 Februari 2021

Aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad aliyefariki jana amezikwa leo kijijini kwao Nyali Mtambwe Mkoa wa Kaskazini Pemba.

https://p.dw.com/p/3pYcR
Tansania Dar es Salaam | Beerdigung von Maalim Seif Sharif Hamad
Picha: Eric Boniface/DW

Maelfu ya wananchi wamefika kuuaga mwili wake katika uwanja wa Mnazi Mmoja, Unguja na kisha uwanja wa Gombani kisiwani Pemba.

Majira ya saa 8 mchana ndege ilitua katika uwanja wa ndege wa Pemba huku wafuasi na viongozi kadhaa wa serikali wakionesha majonzi wakati wakiupokea mwili huo ambao haukugusha na yeyote isipokuwa wanajeshi pekee waliopewa jukumu la kuuteremsha na kuufikisha katika gari maalumu lililotayarishwa kwa ajili ya kuubeba mwili huo na kutembea nao polepole.

Maelfu ya wananchi wajitokeza

Maelfu ya wananchi walisimama njiani huku nyuso zao zikionyesha majonzi makubwa na baadhi yao kuangusha vilio walipoliona gari lilipopakia jeneza la Maalim Seif huku wengine wakiinamisha vichwa nyao na kuvitikisa kwa ishara ya maumivu makali.

Kabla ya kuelekea Zanzibar, mwili wa Maalim Seif ulipelekwa katika Msikiti wa Maamur jijini Dar es Salaam kwa ajili ya swala ya kuuaga. Viongozi mbalimbali walihudhuria kiwemo Rais wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.

Afrika Sansibar Beisetzung Vizepräsident Maalim Seif Sharif Hamad
Rais mstaafu wa Tanzania, Jakaya Kikwete akiwa katika msikiti wa Maamur jijini Dar es SalaamPicha: Eric Boniface/DW

Watu mbalimbali walitoa maoni yao wakiwemo waliofanya naye kazi kwa muda mrefu katika siasa akiwemo Hamad Rashid aliyeunda chama chake cha ADC baadae na Mussa Haji Kombo ambaye alitofautiana mawazo na Maalim Seif kwa kubaki katika chama cha Wananchi CUF wakati wa migogoro ya kisiasa, lakini bado wanamuona Maalim Seif ni mfano wa kuigwa.

Miongoni mwa wanasiasa waliomzungumzia Maalim Seif ni aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai na Salim Mwalimu kutoka Chadema. 

Baadhi ya wananchi walibeba mabango yalioandikwa ujumbe wa aina mbalimbali ukiwemo unaosema ''Ahsante Maalim Seif kwa kutimiza ndoto yako, Ahsante Maalim Seif kwa kutuunganisha wanzanzibari, Mwenyezi Mungu akulipe pepo iliyotukuka''.

Safari yake ya maisha ya miaka 77 ulimwenguni iliyokumbwa na misukosuko na mitihani mingi katika maisha yake Maalim Seif Sharif Hamad imemalizikia leo kwenye kijiji chao cha Mtambwe alipozaliwa. Inna lillahi wainna ilayhi rajiuun.