1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano na migomo yaiandama Brazil

16 Mei 2014

Brazil inakabiliwa na mtihani wa maandalizi yake ya usalama kwa ajili ya michuano ya soka Kombe la Dunia wakati waandamanaji wakikasirishwa na gharama kubwa za kuandaa michuano hiyo wakijiunga na maandamano na migomo.

https://p.dw.com/p/1C1Au
Waandamanaji Sao Paulo.
Waandamanaji Sao Paulo.Picha: picture alliance/AP Images

Brazil inakabiliwa na mtihani wa maandalizi yake ya usalama kwa ajili ya michuano ya soka Kombe la Dunia wakati waandamanaji wakikasirishwa na gharama kubwa za kuandaa michuano hiyo wakijiunga na maandamano na migomo ya wafanyakazi katika miji kadhaa mikubwa nchini humo.

Migomo ya kazi inayoendelea kufanywa na walimu na polisi na tishio la kufanyika kwa mgomo wa taifa zima lililotolewa na polisi pia inazusha hofu ya vurugu ikiwa zimebakia wiki nne tu kabla ya kuanza kwa michuano hiyo ya soka Kombe la Dunia.

Jumla ya watu 10,000 wameandamana katika mitaa ya mji wa Belo Horizonte, Brasilia, Manaus, Porto Alegra,Rio na Sao Paulo.Katika mji mkuu wa kibiashara wa Sao Paulo takriban wanachama 5,000 wa Vugugu la Wafanyakazi Wasiokuwa na Makaazi waliwasha matairi ya magari na kuandamana hadi katika uwanja wa Corinthians Arena ambapo ndipo patakapofanyika pambano la ufunguzi kati ya Brazil na Croatia hapo Juni 12.Waandamanaji pia waliyazingira mabasi yaliokuwa yamejaa abiria.

Kabumbu lapendwa lakini .......

Polisi ilitumia gesi ya kutowa machozi kuwatawanya waandamanaji hao katika makundi madogo madogo.

Waandamanaji Sao Paulo.
Waandamanaji Sao Paulo.Picha: Reuters

Katika mji wa Sao Paulo ambapo maelfu ya watu wengine walijiunga na maandamano ya walimu,waandamanaji 20 walitiwa mbaroni na wapiga picha wawili walijeruhiwa.

Katika mji mkuu wa Brasilia muandamanaji Carlos Serrano mwenye umri wa miaka 32 ameliambia shirika la habari la AFP kwamba analipenda kabumbu lakini ziada ya hilo kuna matatizo mengine mazito ambayo ni haki ya usafiri,afya na elimu.

Rais wa zamani wa Brazil Lula da Silva ambaye alikuwa mstari wa mbele katika juhudi za kuipatia Brazil haki ya kuwa mwenyeji wa michuano hiyo miaka saba iliopita, ameshutumu maandamano hayo kuwa yamepindukia mipaka.

FIFA yashutumiwa

Waandamanaji wengi walielekeza hasira zao kwa Shirikisho la Soka Duniani FIFA ambalo wanaliona kwamba linashughulika na maslahi yake tu.

Duka lililoporwa Recife.
Duka lililoporwa Recife.Picha: Reuters

Baadhi ya mabango ya waandamanaji yalikuwa na mananeo kama vile " FIFA nenda kwenu Uswisi","Msamaha kamili wa kodi kwa FIFA na wafadhili wake","Kombe la Aibu" na"Eee FIFA lipa ada yangu ya kiingilio "

Katika miji ya Rio na Brasilia polisi ilitumia vipulizi vya pilipili kuwatawanya waandamanaji.

Katika mji wa Recife vijana walitumia fursa ya mgomo uliofanyika kwa muda wa polisi wa jeshini kupora maduka na kufanya ghasia ambapo jumla ya watu 170 wamekamatwa katika mji huo katika kipindi cha siku mbili.

Brazil imetumia zaidi ya dola bilioni 11 kuandaa michuano hii ya Kombe la Dunia fedha ambazo waandamanaji wanasema bora zingelitumika katika fani kama vile za usafiri, elimu,nyumba na huduma za afya.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP

Mhariri :Mohammed Abdul-Rahman