1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano yaitikisa Afrika Kusini

Saumu Mwasimba
12 Aprili 2017

Maelfu wamiminika kwenye maandamano ya kushinikiza Zuma aondoke madarakani kufuatia kadhia za ufisadi na kumtimua waziri wa fedha anayekubalika

https://p.dw.com/p/2b8jP
Südafrika Protest gegen Zuma in Pretoria
Picha: Reuters/S. Sibeko

Maelfu ya Waafrika Kusini wamejitokeza kuandamana kumpinga rais wa nchi hiyo Jacob Zuma katika mji mkuu wa kiserikali Pretoria.Waandamanaji wanamshinikiza Zuma aliyetimiza miaka 75 ya kuzaliwa hii leo kung'oka madarakani.Waandamanaji wamemiminika na kujikusanya katika majengo ya serikali,na majengo ya vyama vya wafanyakazi wakiwa wamebeba mabango yanayosema Zuma lazima aporomoke.

Polisi inasema takriban watu 30,000 wameshiriki maandamano ya amani mjini Pretoria.Waandamanaji walibeba mabango yenye ujumbe mbali mbali ikiwemo yale yanayosema kwamba nchi yetu haiuzwi.Ujumbe huu ukilenga madai ya kashfa za rushwa zinazomuandama rais Zuma.Leo (12.04.2017) ni siku ya kuzaliwa na rais huyo aliyetimiza miaka 75  lakini siku hii imesadifu na siku ya kuzaliwa pia waziri wa fedha aliyeondolewa Pravin Godhan ambaye kutimuliwa kwake kumechochea mashirika mawili ya viwango vya ukopeshaji kuushusha uwezo wa Afrika wa kukopesha na kulipa madeni yake na pia kuzusha maandamani makubwa dhidi ya rais huyo.Maandamano ya leo yameongozwa na vyama saba vya upinzani vilivyokuja pamoja kwa maslahi ya taifa ikiwa ni miongoni mwa maandamano makubwa kabisa kuwahi kuitikisa Afrika Kusini katika kipindi cha siku kumi.Kila aliyejitokeza katika maandamano hayo alikuwa na ujumbe mmoja tu Zuma lazima aporomoke.

Protest gegen Zuma Südafrika
Picha: Reuters/M.Hutchings

''Tunaandamana ili Zuma awajibike kwa makosa yote aliyoyafanya.Tunamtaka aondoke madarakani ikiwa hawezi kusimamia kile ambacho ni haki kwa waafrika Kusini. Tunapambana kupigania uhuru kwa ajili ya uhuru wa kiuchumi na hicho ndicho tunakipigania''alisema mmoja wa waandamanaji.

Wengine wamekwenda umbali na kusema kwamba hawamtaki mwizi kuiongoza nchi hiyo huku wakati huohuo  ripoti zikisema aliyekuwa waziri wa masuala ya tawala za mikoa amejiuzulu kiti chake bungeni na kuwa waziri wanne wa zamani kuchukua uamuzi kama huo tangu Zuma alipoamua kufanya mabadiliko yake ya baraza la mawaziri wiki mbili zilizopita.Chama cha African National Congress kimetangaza uamuzi wa Ramathlod katika mtandao wa Twita kikimshukuru kwa mchango wake wa kukisaidia chama hicho.

Wafuasi wa chama cha siasa kali za mrengo wa kushoto kinachopigania ukombozi wa kiuchumi EFF na chama kikuu cha upinzani DA pamoja na vyama vingine vidogo vimeshirikiana kuandamana  kuonesha Umoja na mshikamano nchini humo.Pamoja na kwamba hakuna mchakato wa kura ya maoni uliopangwa kufanyika dhidi ya Zuma bungeni Aprili 18 lakini huenda kuna uwezekano hatua hiyo inaonesha kusogezwa mbele kwa mchakato huo ili kutoa nafasi ya kufanikisha jaribio la chama cha upinzani cha Demokratic Alliance la kutaka ifanyike kura ya siri kuwapa nafasi wapinzani wa Zuma ndani ya chama cha ANC wapige kura ya kutokuwa na imani nae.

Mwandishi:Saumu Mwasimba

Mhariri:Josephat Charo