Mabaki ya ndege iliyomchukua Sala yapatikana
4 Februari 2019Mabaki ya ndege iliyomchukua mchezaji kutoka Argentina Emiliano Sala na rubani wake yamepatikana wiki mbili baada ya ndege hiyo kupotea katika eneo la ujia wa maji kati ya Uingereza na Ulaya bara, mmoja kati ya wachunguzi amesema leo.
Sala mwenye umri wa miaka 28, alikuwa akitokea Ufaransa kwenda kujiunga na klabu yake mpya, ya ligi ya Premier ya Uingereza ya Cardiff City, wakati ndege hiyo ndogo ilipopotea Januari 21 kaskazini mwa kisiwa cha Guernsey. Mtafutaji wa mabaki ya meli baharini David Mearns , ambaye alikodiwa na familia ya mshambuliaji huyo baada ya juhudi rasmi za uokozi kuamua kuachana na juhudi hizo , alisema ndege hiyo ilipatikana Jumapili asubuhi.
Baba yake Sala aliamka jana na kufahamishwa kwamba ndege iliyosababisha kifo cha mwanae imepatikana. "Siamini. ni ndoto mbaya ninayoota," Horacio Sala amesema alipowasiliana na kituo cha televisheni cha Cronica nyumbani kwake mjini Progreso.
Mwandishi: Sekione Kitojo / afpe / rtre / ape / dpae
Mhariri: Idd Ssessanga