1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Risasi na gesi za kutoa machozi zafyetuliwa

12 Mei 2015

Milio ya risasi imehanikiza huku polisi wakiwafyetulia gesi za kutoa machozi waandamanaji wanaovurumisha mawe katika kitongoji kimoja cha mji mkuu wa Burundi-Bujumbura hii Leo.

https://p.dw.com/p/1FOXa
Maandamano yameenea mjini BujumburaPicha: Getty Images/AFP/P. Moore

Haijulikani bado nani wamefyetua risasi katika mapigano hayo katika wilaya ya Butarere ambako mamia ya waandamanaji walikusanyika,wakisema mhula wa tatu anaopanga kuupigania Pierre Nkurunziza ni kinyume na katiba na kinyume pia na makubaliano ya amani yaliyomaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe mwaka 2005.

Waandamanaji walimkamata polisi mmoja wa kike na kumpiga,wakimshutumu kuwafyetulia risasi-walimuachia baadae,akiwa na majaraha.

Katika kipindi cha zaidi ya wiki mbili za maandamano yaliyoitumbukiza nchi hiyo katika mashaka makubwa,polisi wamekuwa wakifyetua risasi hewani na baadhi ya wakati walionekana wakiwafyetulia risasi mpaka waandamanaji.Polisi wanakanusha wanasema hawajawafyetulia risasi waandamanaji. Lakini watu wasiopungua 19 wameuwawa kufuatia maandamano hayo.

Viongozi wa jumuia ya nchi za Afrika Mashariki wakutana Tanzania kesho

Matumizi ya nguvu yamekosolewa vikali na nchi za magharibi-wafadhili wakubwa wa Burundi.Marekani inayolisaidia jeshi la nchi hiyo imehimiza "matumizi ya nguvu dhidi ya waandamanaji" yasitishwe haraka.

Tansania Flüchtlinge aus Burundi
Maelfu ya wakimbizi wa Burundi wanaoingia nchini TanzaniaPicha: DW/P. Kwigize

Viongozi wa nchi za Afrika Mashariki,akiwemo pia Pierre Nkurunziza watakutana nchini Tanzania kesho kuzungumzia mzozo huo pamoja na kuzidi mvutano katika eneo lenye historia ya ugonvi wa kikabila.Zaidi ya watu 50 elfu wameihama Burundi na kukimbilia katika nchi jirani .

Waandamanaji wa wilaya ya Butarere,mojawapo ya vitogoji vya mji mkuu ambako maandamano yamekuwa yakifanyika kila mara, ameweka vizuwizi barabarani,wakitumia mawe na mipira ya magari inayowaka moto.Vyombo vya habari vya nchi hiyo vinasema waandamanaji hao walijaribu kuifunga njia inayaoelekea uwanja wa ndege,walizuwiliwa lakini na polisi.

Wafadhili wa Burundi wataka uchaguzi uakhirishwe

Pierre Nkurunziza anashikilia azma yake ya kupigania mhula wa tatu ingawa Marekani na mataifa mengine ya magharibi na baadhi ya nchi za kiafrika yanamsihi asigombee.

Burundi Präsident Pierre Nkurunziza
Rais Pierre NkurunzizaPicha: Reuters/T. Mukoya

Umoja wa Ulaya na mashirika mengineyo yamesitisha au yanatathmini upya misaada yao yakishurutisha matumizi ya nguvu yakome.

Nchi za magharibi zimepaza sauti zikidai uchaguzi uliokuwa uitishwe baadae mwezi huu na ujao uakhirishwe.

"Tumeihimiza serikali ya Burundi ichukue hatua za kutuliza hali ya mambo na machoni mwetu, fikra ya kubadilisha ratiba ya uchaguzi ingekuwa ya maana,"amesema mjumbe maalum wa umoja wa ulaya katika eneo hilo Koen Vervaeke,aliyetoa kauli hiyo pia kwa niaba ya Uswisi na Marekani.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Reuters/AFP

Mhariri. Iddi Ssessanga