1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macho ya wahariri yameelekezwa Afrika kaszakini na Cologne

Oummilkhheir12 Aprili 2007

Mashambulio ya Algiers na kuundwa baraza la KRM ndizo mmada zilizomulikwa hii leo magazetini

https://p.dw.com/p/CHTG

Baada ya vita vikali vya wenyewe kwa wenyewe,njia ya kuelekea suluhu ya taifa nchini Algeria haikua rahisi.Hivi sasa njia hiyo imezidi kuwa na miba.Katika mashambulio mabaya kabisa ya mabomu kuwahi kushuhudiwa tangu zaidi ya miaka 10 iliyopita,watu zaidi ya 20 wamepoteza maisha yao mjini Algiers.Wanaobeba jukumu la mashambulio hayo,wanajiita „Al Qaida“.Kuhusu mashambulio hayo ya kigaidi ,gazeti la WESER-KURIER la mjini Bremen linaandika:

„Mpango wa kuwaachia huru wanaharakati wa kiislam wanaoshikiliwa korokoroni ulilengwa kurejesha amani nchini.Inadhihirika lakini kana kwamba hakuna majadiliano yoyote ya amani yatakayofanyika pamoja na watu wanaoitumia dini ili kutoa roho na kujiangamizia pia maisha yao .Neno majadiliano na ufanisi,wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam hawalijui-wanajua tuu mashambulio na uhaini.Na katika kulipiza kisasi kwa uhaini,wengi wasiokua na hatia wanapoteza maisha yao.“

Mod:

Hayo ni maoni ya gazeti la WESER KURIER la mjini Bremen.Ama KÖLNER RUNDSCHAU linahisi:

„Kitendo hicho wametaka kieleweke kama tangazo la vita dhidi ya serikali ya Algeria.Shambulio hilo linaonyesha kwa mara nyengine tena: hujuma za kigaidi za wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam si mapambano ya tamaduni dhidi ya ulimwengu wa magharibi tuu.Uwanja wa mapambano unakutikana zaidi kati ya wale wanaoiangalia dini kama jukumu la kibinafsi na kwamba serikali isijishughulishe na mambo ya kidini na wale wanaoitumia dini kisiasa na kutaka kwa kila hali kuunda taifa la kidini,ikilazimika hata kwa matumizi ya nguvu.“

Mod:

Gazeti la LANDESZEITUNG la mjini LÜNEBURG linahisi mwanya unazidi kua mpana kati ya nchi za magharibi na ulimwengu wa kiislam,gazeti linaendelea kuandika:

„Nchi za magharibi zitafanya la maana kama hazitopuuza wimbi hili jipya la matumizi ya nguvu –kinyume na namna zilivyofanya kati ya mwaka 1992 na 1999.Wakati ule vita vya kuania madaraka vilipamba moto kati ya wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam na serikali.Hii leo magaidi wanaofuata itikadi kali ya dini ya kiislam wanaripua mabomu ili kujijengea ngome katika eneo la Afrika kaskazini kuweza kuzihujumu nchi za Ulaya.Wanataraji kupata uungaji mkono wa umma uliopotelewa na matumaini ya kimaisha katika eneo hilo .Nchi za Umoja wa ulaya zinaweza kuzuwia jambo hilo lisitokee kwa kuimarisha ushirikiano kati yao na nchi zinazopakana na bahari ya Mediterenia na kubuni eneo la neema na maisha bora katika bahari ya kati.“

Mod:

Mada ya pili magazetini inahusu kuungana jumuia nne za waislam wa Ujerumani na kuunda „Baraza la kusimamia masuala ya waislam-KRM.Gazeti la HEILBRONNER STIMME linachambua:

„Serikali kuu,serikali za majimbo na mabaraza ya miji wanahitaji mshirika kutoka jamii ya waislam ili mazungumzo yaweze kuleta tija.Kutokana na ukweli huo mtu anaweza kusema kuundwa baraza la kusimamia masuala ya waislam na jumuia nne kubwa za waislam wa Ujerumani ni jambo la maana katika uhusiano kati ya serikali na waumini wa kiislam humu nchini.Lakini jumuia hizo nne zinafuata msimamo wa kihafidhina.Waumini wanaofuata nadharia za wastani hawatakua tena wakisikilizwa siku za mbele.Na wao pia walikua waunde jumuia yao tena tangu zamani.!