1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron, Guterres kuendeleza jitihada za kuisaidia Lebanon

Lilian Mtono
2 Desemba 2020

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres watakuwa wenyeji wa mkutano wa kimataifa wa msaada kwa taifa la Lebanon.

https://p.dw.com/p/3m86t
Frankreich Präsident Emmanuel Macron
Picha: Lewis Joly/AP Photo/picture alliance

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres watakuwa wenyeji wa mkutano wa kimataifa wa msaada kwa taifa la Lebanon utakaofanyika kwa njia ya video kutokea Paris Jumatano hii. Serikali ya Ufaransa imethibitisha kufanyika kwa mkutano huo.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron anafuatilia juhudi zake za kuisaidia Lebanon kufuatia mlipuko mkubwa uliotokea katika mji mkuu Beirut Agosti 4. Kufuatia janga hilo lililosababisha vifo vya zaidi ya watu 190, Macron alisafiri hadi Beirut mara moja.

Aidha, Macron aliitsha mkutano wa ufadhili kwa ajili ya kukusanya msaada wa dharura kuisaidia Lebanon. Hata hivyo, Macron mara zote amekuwa akiuhusisha msaada huo wa muda mrefu na mabadiliko muhimu ya kisiasa nchini humo.

Libanon Beirut Feuer Hafen
Moshi mkubwa uliogubika eneo la bandari mjini Beirut, kufuatia mlipuko mkubwa uliosababisha vifo na kujeruhiwaPicha: Reuters/A. Kanaan

Kiasi ya watu 6,000 walijeruhiwa na karibu wengine 300,000 walikosa makazi kufuatia mlipuko huo. Hali ya kiuchumi pia imezorota sana nchini Lebanon tangu mwanzoni mwa mwaka huu.

Janga la virusi vya corona na mlipuko huo kwa pamoja vimechochea hali kuwa mbaya zaidi na watu wengi wameangukia kwenye shimo la umasikini wa kutupwa.

Mkutano huo wa Jumatano utaangazia suala la msaada kwa raia wa Lebanon. Serikali ya Ufaransa inatarajia wakuu wa mataifa, mashirika ya kimataifa na wafadhili, mashirika yasiyo ya kiserikali na wawakilishi wa mashirika ya kiraia ya Lebanon kuhudhuria mkutano huo.

Ofisi ya Macron imesema mkutano huo unalenga kufanya tathmini ya awali ya msaada ambao tayari taifa hilo limeupokea na msaada gani ambao unahitajika kwa sasa.

Wataalamu wa masuala ya fedha wa Lebanon wanakisia kwamba taifa hilo litahitaji msaada zaidi wa dola milioni 200 hadi 300.

Lebanon mnamo mwezi Mei ilianza mchakato wa makubaliano na shirika la kimataifa la fedha, IMF kuhusu njia zitakazotumika kwenye programu yake ya kusaidia kujinasua kwenye mzozo mbaya kabisa tangu kumalizika kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe mwaka 1990. Lakini katika wakati ambapo hakujafanyika mageuzi, mazungumzo hayo pia yamesimama kwa miezi kadhaa.

Soma Zaidi:Ulimwengu waichangia Lebanon zaidi ya Euro milioni 250 

Mashirika: AFPE