1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazeti ya Ujerumani Leo

Othman, Miraji25 Juni 2008

Maoni ya magazeti ya leo ya Ujerumani

https://p.dw.com/p/EQY7
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Frank-Walter SteimeierPicha: AP

Mada tatu zimezingatiwa sana hii leo na magazeti ya hapa Ujerumani, nayo ni mpango wa kuongezwa wanajeshi wa Kijerumani huko Afghanistan, matokeo ya mkutano wa Berlin juu ya Mashariki ya Kati, na, bila ya kusahau, pia mapambano ya leo ya nusu finali ya kandanda baina ya Ujerumani na Uturuki kuwania kombe la Ulaya.


Katika mada ya kwanza, gazeti la BADISCHE ZEITUNG kutoka mji wa Freiburg lilikuwa na haya ya kuandika:


" Hii ni ishara muhimu tangu majeshi ya Ujerumani kuanza kupelekwa Afghanistan. Kiwango cha juu kabisa cha wanajeshi ambao wanaweza kupelekwa kwa operesheni hiyo ni wanajeshi 4,500. Hapo kabla kiwango cha juu kabisa kilichowekwa kilikuwa 3,500. Kwa miezi sasa, Shirika la Kujihami la NATO limekuwa likizibinya nchi shirika kutuma wanajeshi zaidi. Kwani, kama ilivokuwa hapo kabla, hali ya usalama katika Afghanistan ni tete, idadi ya mashambulio dhidi ya wanajeshi wa Kijerumani imeongezeka na Wataliban wanapata nguvu. Kwa muda mrefu wanajeshi wa kimataifa watahitajika huko Afghanistan. Jeshi la Ujerumani linahitajika, na ndio maana linaongezwa."


Mod:


Gazeti la FRANKFURTER ALLGEMEINE ZEITUNG lilielezea kama hivi juu ya ukosefu wa nguvu za kukata maamuzi:


"Nyuma ya siasa ya Ujerumani ya kutia na kutoa juu ya Afghanistan kuna woga wa chama tawala cha CDU kukabiliana na kampeni ya uchaguzi ya chama cha SPD itakayotwama juu ya amani. Kiongozi wa Chama cha CDU, Angela Merkel, sio tu amepata funzo kuhusu siasa ya kijamii katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2005, lakini pia katika siasa ya kigeni hapo kabla, mwaka 2002. Wasiwasi huo sio kwamba hauna haki, kwani haijulikani vipi utakavokuwa msimamo wa waziri wa sasa wa mambo ya kigeni na mtu ambaye huenda akawa mtetezi wa ukansela wa Chama cha SPD, Frank-Walter Steinmeier. Pale siasa za ndani za Ujerumani zitaacha kuwa na hamu ya nini kinatokea huko Afghanistan, mwishowe dhara kwa pande hizo mbili kutokana na mbinu zao za kisiasa zitakuwa kubwa zaidi kuliko faida ambazo vyama hivyo vitapata."


MOD:


Gazeti la DER PRIGNITER pia linaona tatizo katika kuengezwa wanajeshi wa Kijerumani huko Afghanistan, na limeandika kama hivi:


" Jamii ya kimataifa imeshindwa tena kuwa na mkakati wa pamoja. Mabingwa wote wanasema Afghanistan haiwezi kuwa na amani kwa kutumia tu njia za kijeshi. Lazima misingi ya utawala wa sheria ijengwe na mamlaka ya dola yaimarishwe. Pia Ujerumani inashughulikia zaidi upande wa kijeshi, kwa njia hiyo hakuwezi kupatikana ushindi. Baada ya karibu miaka saba tangu majeshi kuanza kupelekwa huko, ingefaa jambo hilo litambuliwe."


MOD:


Gazeti la MAGDEBURGER VOLKSTIMME lilikua na haya ya kusema kuhusu matokeo ya mkutano wa kimataifa wa Berlin juu ya Mashariki ya Kati:


"Wawakilishi wa nchi 40 wameahidi kusaidia kujengwa jeshi la polisi na mifumo ya mahakama katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan. Jambo hilo ni zuri, kwani usalama na utawala wa sheria ni sharti muhimu ya kuweko mifumo ya dola ya Kipalastina. Bila ya kuweko mifumo ya usalama na sheria ilio madhubuti na yenye kufanya kazi, Israel haitoweza kukubali kuundwa dola ya Kipalastina."


MOD:


Liliandika MAGDEBURGER VOLKSSTIMME.


Magazeti mengi ya Ujerumani yameelekeza makala yao ya uhariri kuhusu mchuano wa leo wa kandanda wa nusu finali kati ya Ujerumani na Uturuki kuwania Kombe la Ulaya. Gazeti la TAGESZEITUNG liliandika namna hivi:


"Mara nyingi mtu alisikia hofu kwamba kunaweza kukatokea fujo baada ya mchezo wa leo. Lakini haifikiriwi kwamba jambo hilo litatokea, kwani magazeti ya Kijerumani na ya Kituruki yametangaza kwamba mchezo huu utakuwa wa kirafiki. Gazeti la Kituruki la HÜRRIYET limewataka wasomaji wake waende kuutizama mchezo wa leo wakibeba bendera za nchi zote mbili. Kwamba watu hao wana uaminifu kwa nchi zote mbili ni jambo linaloaminika. Kwani pindi Ujerumani leo itashinda, Waturuki wengi wa hapa Ujerumani itawabidi waipigie dau Ujerumani katika mchezo wa mwisho wa finali. Lakini vipi itakua pindi Uturuki itashinda leo? Pia yawezekana Wajerumani, ambao si wenye asili ya Kituruki, wakajaribu kuisherehekea Uturuki."


Naam hayo ndio yalioandikwa na gazeti la TAGESZEITUNG la mjini Berli, na ndilo linalotukamilishia makala haya ya kutoka Magazeti hii leo.













"