1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini: Mtandao wa madanguro haramu Ujerumani wakamatwa

Sekione Kitojo
19 Aprili 2018

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wamejishughulisha na mada kuhusu makundi ya wanaofanya biashara haramu ya kusafirisha watu na kuwatumia katika ukahaba,na miaka 70 tangu kuundwa kwa taifa la Israel.

https://p.dw.com/p/2wJVw
Bundesweite Razzia gegen Organisierte Kriminalität
Picha: picture-alliance/dpa/A. Vogel

Mhariri  wa  gazeti  la  Leipziger Volkszeitung  anazungumzia  kuhusu msako  uliofanywa  na  polisi nchini  Ujerumani  dhidi  ya makundi ya watu wanaofanya  biashara  ya  kuwasafirisha  watu kinyume  na sheria  na  kuwatumia  katika  madanguro ya  ukahaba nchini Ujerumani. Mhariri  anaandika:

Katika  msako  mkubwa  kabisa  katika  historia  yake polisi  ya Ujerumani ilikamata  mtandao  wa  madanguro, ambayo  yaliwaajiri watu waliobadilisha  jinsia na kuwaingiza nchini  Ujerumani  kufanya kazi  ya  ukahaba  kwa  nia  ya  kujipatia  fedha  na  kuwaingiza nchini  humo  kwa  njia  ya  kuwapatia  visa  za  kitalii  kutoka Thailand.  Nchi  hii  ya  Thailand ambayo  ni  kivutio  kikubwa  cha utalii kwa  watu  wanaotaka  kwenda katika  mapumziko  ya likizo, imejiweka  katika taswira mbaya  ya  kuwa  uwanja  wa  biashara  ya haramu  ya  kimataifa ya  kusafirisha  binadamu.

Kuhusu  mada  hiyo  hiyo mhariri  wa  gazeti  la Neue Osnabrücker Zeitung, anaandika  kwamba msako  mkubwa  umefanyika dhidi  ya mtandao  wa  madanguro. Mhariri  anaandika:

Biashara ya kusafirisha  watu kwa  njia  haramu, ukahaba wa kulazimishwa, haya ni  maneno  mazito, ambayo  yanajihusisha  zaidi na picha zinazolingana na  hali  hiyo.  Hii  si  mada  ya  kuipuuzia. Lakini  pia  ni  lazima  kutofautisha. Sio  kila  mwanamke, ambaye anapata  fedha  kwa  kutumia mwili wake, analazimishwa. Kwa kuwa katika  nchi  hii kwa kiasi  kikubwa ukahaba ni  jambo  linaloruhusiwa kisheria na kwa kuwekewa  sheria  maalum kuna  uwazi  katika shughuli  hiyo. Ni muhimu basi  kusisitiza  kwa  hiyo, kutojitumbukiza katika  hatua  ambazo si  lazima  kuzichukua. Hata  hivyo  kuchukua hatua  dhidi  ya biashara  haramu ya kuwasafirisha  watu  kama ilivyo  hivi  sasa  si  hatua  mbaya. Kwa sababu kuna upande uliojificha  katika  biashara  hii  ya ukahaba. Wanawake  na wanaume  wanalazimishwa  kwa kutumia nguvu, kujiuza.

Jamii  ya  Kiyahudi  ni sehemu  ya  jamii  ya  Wajerumani  tangu enzi na  enzi. Anaandika  mhariri  wa  gazeti  la General-Anzeiger  la  mjini Bonn, anapoandika  maoni  yake  kuhusu mashambulizi  dhidi  ya Wayahudi nchini  Ujerumani. Mhariri  anaandika:

Tangu  wakati  huo  jamii  hii  imekuwa  mara  kwa  mara  ikikabiliwa na  chuki dhidi  yake, madharau  na  kuwatoa  thamani. Wanafunzi na  waalimu  wanapaswa kuwa  na  uwezo  wa  uvumilivu  na maridhiano  zaidi na  kunapotokea  hali  ya  kutokuwa  na  uvumilivu na  maridhiano  wachukue hatua  kali. Mashirika  ya  Waislamu na misikiti  yanapaswa kuwa na  msimamo  wa  wazi. Sheria zinapaswa kutumiwa  na  kuzuwia  kila  aina  ya  chuki.

Mhariri  wa  gazeti  la  Stuttgarter Zeitung  anaandika  kwamba uwajibikaji  wa  kihistoria  kuihusu  Israel  uko  katika  msingi  wa taifa  na  watu  wake. Mhariri  anaadika hayo  kuhusiana  na  mada ya  maadhimisho  ya  miaka  70   tangu  kuundwa  kwa  taifa la Israel. Mhariri  anaadika:

Lakini  hii  haina  maana  kwamba  kila njia  ambayo  serikali  yoyote ya  Israel  inaamua kuchukua ni  lazima  kuiunga  mkono. Hata  hivyo Ujerumani  pia  ni  lazima  ichukue  tahadhari  kuhusiana  na ongezeko  la  chuki  dhidi  ya  Wayahudi  na pia  kutilia  maanani ongezeko  la siasa  kali  za  mrengo  wa  kulia. Ubalozi  wa  Israel nchini  Ujerumani  ni  muhimu hivi  sasa  kuliko  wakati  wowote ule.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo / inlandspresse

Mhariri: Josephat Charo