1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama ya UN yamfunga Radovan Karadzic maisha

Iddi Ssessanga
20 Machi 2019

Majaji wa mahakama ya rufaa ya Umoja wa Mataifa wamemhukumu kifungo cha maisha, Radovan Karadzic kwa makosa ya mauaji ya kimbari na uhalifu wa kivita, na kuongeza kifungo chake cha awali cha miaka 40.

https://p.dw.com/p/3FNRX
Bildkombo Radovan Karadzic und Dragan Dabic
Picha: picture-alliance/dpa/M. Evstafiev/Healthy Life Magazine

Akisoma uamuazi wa mahakama hiyo muda mfupi uliopita, Jaji kiongozi Vagn Joensen amasema majaji wa kamati ya rufaa mjini The Hague wametoa kifungo cha maisha baada ya kutupilia mbali rufaa ya Karadzic dhidi ya hatia ya ukatili uliohusisha mauaji ya Srebrenica ya mwaka 1995, iliyotolewa dhidi yake mwaka 2016.

Katika hukumu hiyo ya mwaka 2016 Karadzic alihukumiwa kifungo cha miaka 40 gerezani. Lakini Karadzic pamoja na upande wa mashtaka walikataa rufaa kupinga hukumu hiyo.

Mahakama imethbitisha hukumu ya kwanza, lakini imekubaliana na upande wa mashtaka kwamba hukumu hiyo ilikuwa ndogo sana kwa kuzingatia ukubwa wa uhalifu ambao alihukumiwa.

Hoja za kamati ya rufaa

Karadzic mwenye umri wa miaka 73 sasa, alisimama kizimbani bila kujongea huku akiwa na uso mzito wakati majaji wakisema wanathibitisha hukumu za mwaka 2016 na kuongeza kifungo chake kutoka miaka 40 hadi maisha.

Jaji Joensen amesema majaji waliosikiliza kesi ya mwanzo hawakuzingatia uzito wa jukumu la Karadzic katika uhalifu huo mbaya zaidi kutendwa wakati wa kipindi cha mgogoro, uliokuwa mkubwa isivyo kawaida na wa ukatili wa aina yake.

Radovan Karadzic verkleidet als Dragan Dabic
Karadzic alifuga ndevu na kubadilisha muonekano wake ili kukwepa mkono wa sheria lakini siku za mwizi ni arobaini.Picha: picture-alliance/dpa/EPA/STR

Majaji wamekataa madai ya Karadzic kwamba hakufahamu maagizo ya vikosi vya Waserbia wa Bosnia kuwauwa Waislamu wanaume na wavulana mjini Screbrenica, na kuwalenga raia bila kuchagua mjini Sarajevo.

Pia wameketaa madai yake kwamba hakujua kuhusu agizo alilolianda na kulitia saini kuhusu hatma ya Srebrenica, ambalo lilitaka kuunda mazingira yasiyohimilika pasipo na matumaini ya kunusurika tena kwa wakaazi w amji huo.

Hukumu ya mwaka 2016

Mwaka 2016 Karadzic alikutwa na hatia katika mashtaka 10 yakiwemo kupanga mzingiro wa karibu miaka minne wa mji mkuu wa Bosnia Sarajevo, ambako zaidi ya watu 100,000 walikufa katika kampeni ya kulenga shabaha na mashambulizi, kwa mujibu wa waendesha mashtaka.

Pia alikutwa na hatia ya mauaji ya kimbari katika eneo la mashariki mwa Bosnia la Srebcrenica, ambako wanajeshi wa Kiserbia waliwachinja zaidi ya wanaume na wavula Waislamu 8000, katika eneo ambalo lilipaswa kuwa chini ya ulinzi wa Umoja wa Mataifa,mjini Sarajevo na kisha miili yao kuzikwa katika makaburi ya halaiki.

Hukumu ya Jumatano ndiyo ya mwisho na haiwezi kukatiwa tena rufaa, na itakuwa na mvumo mkubwa katika iliyokuwa Yugoslavia, hasa Bosnia, ambako jamii za wachache zinaendela kugawika, na Karadzic bado anaangaliwa na Wabosnia wengi wenye asili ya Serbia kama shujaa.

/ape,afpe,dpae.