1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majeshi ya Iraq yaelekea kuukomboa mji wa Mosul

Sekione Kitojo
25 Juni 2017

Majeshi ya Iraq yamefungua njia za kupita mamia ya raia kuukimbia mji mkongwe wa Mosul jana Jumamosi wakati yakipambana kukomboa eneo hilo kutoka wanamgambo wa Dola la Kiislamu wakipigana kutetea ngome yao mjini Mosul.

https://p.dw.com/p/2fKpS
Irak Kampf um Mossul
Picha: picture-alliance/MAXPPP

Vikosi  vilivyopewa  mafunzo  na  Marekani  katika  vita  vya  mjini  vinaendelea  na mapambano  yake  katika  mitaa  miwili  muhimu ambayo  inakutana katikati  ya  mji  huo mkongwe, kwa  lengo  la  kuwatenga  wanamgambo  wa  jihadi  katika  maeneo  madogo madogo  manne.

Mapambano  hayo  yaliyodumu  kwa  wiki  moja  sasa  katika  mji  huo  mkongwe yanafikia sasa  mapigano  makali  mno katika  kampeni  ya  miezi  minane  hivi  sasa  inayoungwa mkono  na  Marekani kuukomboa  mji  huo  wa  kaskazini, ambao  uliangukia  mikononi  mwa wanamgambo  Juni , 2014.

Irak Kampf um Mossul
Raia wakikimbia kutoka mstari wa mbele wa mapambano mjini MosulPicha: Getty Images/AFP/A. Al-Rubaye

Mwandishi  habari  wa  shirika  la  habari  la  Reuters alimuona  msichana  mdogo akiwa  na majeraha  usoni  akitembea  akiwa  amechoka akipita  mstari  wa  mbele  wa  mapambano kutoka  katika  wilaya  yenye  watu  wengi  akiwa  na  kundi  la  majirani. Familia  yake  yote imeuwawa wakati nyumba  yao  ilipoanguka, wanasema.

Umoja  wa  mataifa  umeeleza  hali  ya  hatari  jana  Jumamosi kwa idadi  kubwa  ya  vifo  vya raia  katika  mapigano, ukisema  zaidi  ya  watu  12  waliuwawa  na  mamia  wamejeruhiwa siku  ya  Ijumaa.

Mapigano makali

Irak Kampf um Mossul
Mapambano yanaendelea , wanajeshi waliopata mafunzo ya mapigano ya mijiniPicha: Getty Images/AFP/A. Al-Rubaye

"Mapigano  ni  makali  mno katika  mji  mkongwe na  raia wako  katika  hali  mbaya, na hatari ambayo  haina mfano. Kuna  ripoti  kwamba  maelfu, huenda  hata  mamia  kwa  maelfu , ya watu wanashikiliwa  kama  ngao  ya  binadamu na  wanamgambo  wa  Dola  la  Kiislamu," Lise Grande , mratibu  wa  masuala  ya  kiutu  wa  Umoja  wa  mataifa  nchini  Iraq, amesema katika  taarifa. "Mamia  ya  raia , ikiwa  ni  pamoja  na  watoto, wanapigwa risasi."

Maafisa  nchini  Iraq wanamatumaini  ya  kutangaza  ushindi  katika  mji  huo  wa  kaskazini mwa  Iraq katika  wakati  wa  sikukuu  ya  Eid , ambayo  ni kuadhimisha  mwisho  wa  mfungo mtukufu  wa  Ramadhan, katika  siku  chache zijazo.

Helikopta zenye  silaha  zilikuwa  zinasaidia  mapambano   ya  vikosi  vya  ardhini , zikishambulia maeneo  waliko wanamgambo katika  mji  mkongwe, mwandishi  wa  shirika la  ndege  la  Reuters ameripoti  kutoka katika  eneo  karibu  na  mstari wa  mbele  wa maambano.

Irak Kampf um Mossul
Katika mitaa mingi ya Mosul haiwezekani tena kuptisha gari lenye silaha, wanajeshi wanalazimika kutembea kwa miguu nyumba kwa nyumbaPicha: Getty Images/AFP/A. Al-Rubaye

Kusongambele  kwa  majeshi  ya  serikali kunatengeneza  njia  za  kupita  raia  wakikimbia kutoka  katika  maeneo  yanayoshikiliwa  na  kundi  la  Dola  la  Kiislamu.

Raia wanakimbia  mapigano 

Kumekuwa  na mmiminiko taratibu  wa  familia  zinazokimbia  jana , baadhi  wakiwa wamejeruhiwa pamoja  na  watoto  ambao wamedhoofu  kwa  njaa. "Mtoto  wangu  amekuwa akila  mkate  na  maji  kwa  siku  nane  zikizopita," mama  mmoja  alisema.

Kiasi raia 100 waliwasili  salama katika  eneo  linaloshikiliwa  na  serikali  magharibi  mwa mji  mkongwe  katika  kipindi  kimoja  cha  dakika  20, wakiwa  wamechoka, wakiwa  na  hofu na   njaa. Wanajeshi waliwapa  chakula  na  maji.

Zaidi  ya  raia 100,000 , miongoni  mwao  nusu  wanaaminika  kuwa  ni  watoto, wanaendelea kunaswa  katika  majengo  ambayo  ni  magofu  katika  mji  huo  mkongwe, wakiwa  hawana chakula, maji  ama  matibabu.

Irak Kampf um Mossul
Kila mahali hali ni ngumu kupitikaPicha: Getty Images/AFP/A. Al-Rubaye

Majeshi  yanayopigana  vita  vya  mjini  yanaongoza kampeni  kusafisha  eneo  hilo kuwaondoa  wapiganaji  kutoka  katika mitaa kadhaa  ya  mji  huo  mkongwe, wakitembea kwa  miguu  nyumba  kwa  nyumba katika  maeneo  yaliyojaa  vifusi  na  kuwa  taabu  kwa magari  ya  kivita kupita.

Mwandishi  habari  raia  wa  Ufaransa  Veronique Robert alifariki mjini  Paris  baada  ya kujeruhiwa katika  mripuko mjini  Mosul maema  wiki  hii, mwajiri  wake televisheni  ya Ufaransa  amesema siku  ya  Jumamosi. Bomu  liliripuka na  kumuua  mwandishi  habari  wa Iraq Bakhtiyar Haddad  na  mwandishi  habari  wa  Ufaransa  Stephane Villenueve wakati mwandishi  mwingine  wa  kujitegemea  alipata  majeraha  madogo.

Irak Selbstmordanschlag in Mossul
Majeruhi wakiondolewa kutoka katika eneo la mapigano Picha: Getty Images/AFP/A. Al-Rubaye

Mashirika  ya  kutoa  misaada  na  maafisa  wa  Iraq wanasema kundi  la  Dola  la  Kiislamu linawazuwia  raia kutoka ili  kuweza  kuwatumia kama  ngao ya  binadamu. Mamia  ya  raia wanaokimbia  kutoka  mji  mkongwe  wamepigwa  risasi na  kuuwawa  katika  wiki tatu zilizopita.

Mwandishi : Sekione  Kitojo / rtre

Mhariri: Yusra Buwayhid