1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makampuni ya kigeni yalalamikia kodi kubwa Tanzania

Grace Kabogo
29 Novemba 2016

Baadhi ya makumpuni makubwa ya kigeni yaliyowekeza nchini Tanzania huenda yakafikiria kupunguza au kusitisha shughuli zake kwa sababu ya masharti magumu yanayowekwa dhidi ya makampuni hayo, ikiwemo kodi kubwa.

https://p.dw.com/p/2TQqs
Tansania Kigamboni Brücke Bauarbeiten
Picha: Imago/Xinhua

Kwa mujibu wa mahojiano yaliyofanywa na shirika la habari la Reuters pamoja na wakurugenzi wakuu wa makapuni ya kigeni yaliyowekeza nchini Tanzania, kiasi ya makampuni sita yanafikiria mipango mipya kuhusu uwekezaji katika sekta ya madini, mawasiliano ya simu au usafirishaji kwa kutumia meli. Hiyo yote inatokana na juhudi zinazofanywa na Rais wa Tanzania, John Magufuli kuubadili uchumi wa nchi hiyo.

Makampuni matatu yamesema huenda yakapunguza shughuli zake za uwekezaji kwenye taifa hilo la Afrika Mashariki, huku makampuni mengine mawili yakisema yanafikiria kutanua zaidi shughuli zake katika nchi jirani na kampuni moja imesema inaandaa mchakato wa kujiondoa kabisa nchini Tanzania. Makampuni hayo yaliombwa kutotajwa majina kwa sababu ya umuhimu wa suala hili na kwa sababu mipango yao hiyo bado haijatangazwa hadharani.

Kampuni moja bado haijatoa msimamo wake jinsi ya kukabiliana na mageuzi hayo ya serikali ya Tanzania, huku makampuni matano yakisema kuwa mipango yao haikuathirika na mageuzi hayo, ikiwemo miradi miwili mikubwa, ule wa kiwanda cha kusindika gesi asilia-LNG wenye thamani ya Dola bilioni 30 na mradi wa kiwanda cha mbolea wenye thamani ya Dola bilioni 3.

Tanzania na uwekezaji wa kigeni

Tanzania inategemea zaidi uwekezaji wa kigeni wa moja kwa moja, kuliko nchi nyingine za ukanda huo, kutokana na ukubwa wa uchumi wake. Mwaka uliopita nchi hiyo ilipokea zaidi ya Dola bilioni 1.5, kwenye uchumi ambao thamani yake ilikuwa chini ya Dola bilioni 45. Hiyo ni kwa mujibu wa takwimu za Mkutano wa Biashara na Uwekezaji wa Umoja wa Mataifa pamoja na Benki ya Dunia.

Tansania John Magufuli
Rais wa Tanzania, John MagufuliPicha: Getty Images/AFP/D. Hayduk

Rais wa Tanzania, John Magufuli ambaye amepewa jina la utani ''Tingatinga'' kutokana na miradi yake ya miundombinu na aina ya uongozi wake, alizindua mchakato wa mageuzi yake ya kiuchumi, baada ya kuchaguliwa kuiongoza nchi hiyo mwaka uliopita, akiahidi kuubadilisha uchumi wa nchi hiyo, kuondoa urasimu na rushwa pamoja na kutekeleza mradi mkubwa wa ujenzi.

Mwaka huu serikali ya Magufuli iliongeza kodi katika utumaji wa fedha kwa kutumia simu za mkononi, mabenki, huduma za utalii na zile za usafirishaji wa mizigo. Kodi ya mapato kwa mwaka wa fedha 2014/2015 jumla ilikuwa Shilingi za Tanzania trillioni 9.8 ambazo ni sawa na Dola bilioni 4.5. Kwa mwaka wa fedha 2016/2017, serikali ina lengo la kukusanya kodi ya mapato zaidi ya trilioni 15.1, ikiwa ni ongezeko la zaidi ya asilimia 50.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Adolf Mkenda, amesema wameyasikia malalamiko yanayotolewa na milango iko wazi, lakini wanahakikisha kuwa kila mtu analipa kodi anayopaswa kulipa kwa kuzingatia haki. Amesema lazima kuwepo na mageuzi mapya ambayo ni magumu, ili kuufanya uchumi kuwa imara.

Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA, Richard Kayombo amesema ongezeko la kodi ya mapato lilihitajika kwa ajili ya kulipia miundombinu mipya nchini humo. Makampuni makubwa ya kigeni ambayo yamewekeza nchini Tanzania ni pamoja na yale ya nishati, uhandisi, mawasiliano ya simu, madini, na usafirishaji kwa kutumia meli.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/Reuters
Mhariri: Saumu Yusuf