1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makundi ya washia yawania udhibiti wa miji kusini mwa Iraq.

Sekione Kitojo21 Aprili 2007

Jimbo la Basra ambalo lina utajiri mkubwa wa mafuta kusini mwa Iraq linajikuta hivi sasa katika mapambano makali zaidi kati ya makundi hasimu ya Washia.

https://p.dw.com/p/CHlA

Basra , mji wa pili kwa ukubwa nchini Iraq ukiwa na idadi ya wakaazi wanaokadiriwa kuwa milioni 2.6, ni mji mkuu wa jimbo la kusini la Basra na bandari kuu ya Iraq. Hifadhi kubwa kabisa ya mafuta ambayo imefanyiwa utafiti nchini humo inapatikana katika jimbo hilo.

Kundi linaloongozwa na kiongozi wa kidini anayepinga majeshi ya Marekani kuikalia Iraq Muqtada al Sadr wa madhehebu ya Shia , ambaye hivi karibuni aliamuru wanasiasa wake kuondoka katika serikali ya Iraq kutokana na upinzani wake dhidi ya majeshi ya Marekani kuikalia nchi yake, amesema kuwa kundi lake halitamkubali tena gavana wa jimbo la Basra Mohammed al –Wai’ili kwasababu ni mwanachama wa chama cha Washia cha al –Fadhila.

Chama cha Al – Fadhila kimeondoa kutoka katika muungano wa kisiasa wa washia unaoongoza serikali mwezi March.

Viongozi wa Al-fadhila wamesema kuwa wanakataa kushiriki katika siasa za kimadhehebu. Chama hicho kimetangaza kuwa kitaendelea kuwa kama kundi la pekee.

Licha ya ukweli kuwa makundi yote yameamuru kuondoa wawakilishi wao kutoka katika serikali ya Iraq, yenyewe binafsi yanaendelea kuwa katika mgongano.

Kundi la Sadr vinawania udhibiti mkubwa zaidi wa miji kusini mwa Iraq, na linatuhumiwa kuwa na uhusiano na serikali ya Iran. Al-Fadhila inapinga sera hizi. Gavana huyo pia anakataa kuingilia kati kwa Iran katika siasa za makundi ya Washia nchini Iraq.

Sadr ana uungwaji mkono mkubwa nchini Iraq, ambapo , inakadiriwa kuwa katika mamilioni , na wapiganaji wake ni moja kati ya makundi yenye nguvu nchini humo. Al Fadhila ina ngome ndogo, kijeshi ama vingine.

Sadr amekuwa haelewani na kiongozi mkuu wa kidini mzaliwa wa Iran Ayatollah Ali al-Sistani ambaye ana mahusiano ya karibu na viongozi wa kidini wa Iran. Chama cha Fadhila hakina urafiki na Sistan pia, ambaye anaendelea kuukumbatia utawala unaendelea kuporomoka wa serikali ya Iraq.

Lakini kufanana kwa mambo mengi kwa msimamo wa makundi hayo hakujaleta hali ya kupunguza tofauti miongoni mwa makundi hayo.

Chama cha Fadhila kinasema kuwa kinataka kuleta hali ya umoja nchini Iraq, na kuishutumu serikali, ambayo hadi hivi karibuni imekuwa na wawakilishi wa Sadr ambao wamekuwa wakiendekeza siasa za kimadhehebu nchini Iraq. Sadr pia anasema kuwa anataka Iraq yenye umoja, lakini jeshi lake la Mehdi linaendelea kuwashambulia Wasunni, hususan mjini Baghdad.

Muqtada al-Sadr hivi karibuni aliwataka wafuasi wake kuandamana dhidi ya gavana wa Basra. Kiasi cha waandamanaji 2,000 walijiunga na maandamano hayo, wachache zaidi kuliko alivyotarajia.

Wale ambao wanakubali miito ya al-Sadr sio wengi katika mji wa Basra , mwalimu mkuu wa shule ya sekondari Muhammad Hussein ameliambia shirika la habari la IPS. Amelaumu wafanya ghasia katika kila upande. Ni wahuni tu ambao watapenda kupora mali ya serikali watafaidika na ghasia.

Wiki chache zilizopita zimeona mapigano kadha kati ya watu wenye silaha kutoka katika makundi yote hayo. Katika tukio moja watu wenye silaha wanaoaminika kuwa wanatoka katika jeshi la al Sadr la Mehdi wamevamia ofisi za chama cha Al fadhila.

Watu wa kawaida wanasema kuwa majeshi ya Uingereza yaliyoko katika eneo hilo ambayo yana wajibu wa ulinzi kusini mwa Iraq, na hususan Basra, hawataki kuingilia katika mizozo hii mipya ya kisiasa.

Lakini watu wengi katika jimbo la Basra wanalaumu uvamizi wa jeshi la Marekani kwa hali hiyo mbaya inayotokea.