1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Manchester City yatwaa kombe la Capital One

29 Februari 2016

Kombe la kwanza la msimu wa kandanda England limekwenda katika klabu ya Manchester CITY baada ya kuipiku Liverpool kupitia mikwaju ya penalti katika fainali ya Kombe la Ligi za Uingereza uwanjani Wembley

https://p.dw.com/p/1I4Nf
Fußball Liga-Pokal-Endspiel Liverpool vs. Manchester City
Picha: Getty Images/C. Brunskill

Mchuano huo ulikamilika kwa sare ya bao moja kwa moja baada ya muda wa ziada lakini City wakashinda penalty tatu kwa moja.

Na hata kabla ya kupumzika kutokana na kichapo hicho, Liverpool watawakaribisha City uwanjani Anfield siku ya Jumatano katika mchuano wa Ligi ya Premier.

Kabla ya fainali ya Wembley, kuna chipukizi aliyeendelea kugonga vichwa vya habari baada ya miujiza yake katika uwanja wa Old Trafford.

Marcus Rashford mwenye umri wa miaka 18 aliiduwaza Arsenal baada ya kuifungia Manchester United magoli mawili na kupeana pasi ya goli jingine, katika ushindi wao wa 3-2. Mshambuliaji huyo pia alifunga mabao mawili katika mchuano wa wiki iliyopita ambao United iliizaba Midtjylland mabao matano kwa moja katika Europa League.

Matokeo hayo ni pigo kwa Arsenal katika matumaini yake ya kuwania taji maana sasa wako pointi tano nyuma ya viongozi Leicester City na tatu nyuma ya nambari mbili Tottenham Hotspurs. Lakini kocha Arsene Wenger amewataka vijana wake wafufuke na kuyarekebisha mambo katika mchuano wao wa Jumatano dhidi ya Swansea kabla ya kukutana na Spurs Jumamosi. Kabla ya hapo lakini lazima Spurs wachuane na nambari sita kwenye ligi West Ham.

Leicester City wanaweza kuendeleza ndoto yao ya kinyang'anyiro cha taji ikiwa watawanyamazisha West Brom kesho usiku. United ambao wako ambao wako katika nafasi ya tano nyuma ya City na pengo la pointi tatu, watachuana na Watford. Kocha Louis Van Gaal janaa liwachekesha mashabiki kwa kujiangusha uwanjani akilalamika namna wachezaji wa Arsenal walivyokuwa na wakianguka ovyo. Chelsea itakwaruzana na Norwich.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/AP
Mhariri: Mohammed Khelef