1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni juu ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Abdu Said Mtullya14 Februari 2014

Ufaransa inahitaji kuungwa mkono kijeshi pia na Ujerumani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.Mauaji yanayotokana na sababu za udini pamoja na vurumai ni tishio kwa eneo lote la Afrika ya Kati anasema Claus Stäcker

https://p.dw.com/p/1B8Dj

Picha za kutisha ambazo DW haiwezi kuzionyesha zimetokea Jamhuri ya Afrika ya Kati. Katikati ya mji mkuu ,Bangui mtu mmoja aliuliwa kiholela barabarani. Waandishi habari wa kimataifa walipiga picha kuonyesha jinsi mtu huyo alivyokuwa anakatwa vipande vipande,bila ya msalie.

Mpita njia mmoja alionyeshwa akizila sehemu za mwili za mtu huyo

Deutsche Welle Claus Stäcker
Claus Stäcker Mkurugenzi wa idara ya AfrikaPicha: DW

.Ni kitendo cha kinyama sana. Lakini unyama mkubwa zaidi ni kwamba hata askari wa Ufaransa waliokuwa karibu, na waliokuwa wameshamiri kwa silaha hawakuweza kuuzuia unyama ukatili huo.

Sehemu kubwa ya Jamhuri ya Afrika ya kati imeenda mrama

Ilisemekana hapo awali kwamba askari,1600 wa Ufaransa wanatosha kuudhibiti mji mkuu Bangui kwa kiwango kikubwa. Ndege za misaada za Umoja wa Mataifa kutokea Cameron zingeweza kutua katika uwanja wa ndege wa mjini Bangui.Aidha Rais wa kipindi cha mpito amechaguliwa haraka

Rais mkakamavu wa kipindi cha mpito ameteuliwa.Kutokana na uwepo wa majeshi ya Ufaransa Rais huyo Catherine Samba-Panza ameweza kutoka nje kidogo ya mji wa Bangui.Lakini hakuweza kufika mbali sana. Sehemu kubwa ya nchi haidhibitiki. Kwa sababu katika sehemu hizo hakuna askari wa Ufaransa wala wa Afrika. Majina ya miji ambako mauaji ya kimbari yanafanyika yanasahaulika haraka :majina kama vile Boda,Bouka au Nzakoun.

Wanamgambo wa kiislamu wanawaua wanawake na watoto, na makundi ya kujihami ya wakristo nayo yanalipiza kisasi kwa kuwaua Waislamu kwa ukatili mkubwa .Mpaka sasa watu zaidi ya 2,000 wameshauawa lakini idadi halisi ni kubwa zaidi. Mashirika ya kutetea haki za binadamu yanatanabahisha juu ya kutokea maujai ya kimbari, wakati Umoja wa Mataifa umesema katika Jamhuri ya Afrika ya Kati yanatokea maafa ya kibinadamu yasiyo semeka.Kamishna wa Umoja wa Mataiafa anaewashughulikia wakimbizi Guitteres amesema watu Milioni moja na nusu wamegeuka wakimbizi katika Jamhuri ya Afrika ya Kati na wanahitaji msaada wa chakula.

Mafanikio ya Ufaransa nchini Mali

Ufaransa iliyopata mafanikio ilipoingilia kati nchini Mali ,ikiwa na ari mpya ilifanya makosa makubwa katika tathmini ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.Askari wa Ufaransa wanaweza kuvirudisha nyuma vikosi vya kijeshi na kuvinyang'anya silaha. Lakini ni vigumu kwa askari wa Ufaransa kuyazuia magenge yanayozuka ghafla na kuua watu kiholela barabarani. Majeshi ya nchi za Afrika Misca, yalichukua hatua za haraka sana ambazo siyo za kawaida, kwa kuwapeleka askari 5,000 katika Jamhuri ya Afrika ya Kati. Lakini askari hao wanachukiwa sana kwa sababu idadi kubwa ni ile ya askari wanaotoka katika nchi jirani ya Chad ambayo tokea mwanzo imehusika sana na mgogoro wa Jamhuri ya Afrika ya Kati.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon aliiomba Ufaransa iongeze idadi ya askari wake katika Jamhuri ya Afrika ya kati.

Rais wa kipindi cha mpito Samba-Panza ametaka askari wa Umoja wa Mataifa. Lakini mchakato huo ungelichukua muda wa angalau nusu mwaka. Na hadi wakati huo Jamhuri ya Afrika ya kati ingelikuwa imemegeka kama kashata kati ya sehemu ya Waislamu kaskazini mwa nchi na sehemu ya Wakristo kusini mwa nchi. Hakuna anaejua athari zake kwa eneo lote-eneo lenye makundi chungunzima ya waporaji katika Sudan,Sudan Kusini,Kongo au Uganda.

Sera ya Ujerumani juu ya Afrika inapaswa ijumlishe nyanja ya kijeshi

Mnamo miaka ya nyuma Ufaransa ilifanya makosa mengi katika sera yake juu ya makoloni yake ya zamani, na hasa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati. Rais Hollande alitaka kuifunga sera hiyo na kuonyesha kuwa mkweli.Mambo yalienda vizuri nchini Mali.Katika Jamhuri ya Afrika ya Kati ambako Ufaransa haiwezi kutuhumiwa kuwa na maslahi ya kiuchumi,mtazamo mpya ungeliweza kuendelezwa, lakini Ufaransa inahitaji kuungwa mkono na washirika.Lakini washirika wake wa Umoja wa Ulaya mpaka wameonyesha ari ndogo sana. Ujerumani ilitoa kauli kuonyesha mshikamano lakini ilichokifanya ni kutoa msaada wa ndege ya wagonjwa. Hayo hayatatosha kuituliza hali katika Afrika ya Kati.

Sasa mengi yanazungumzwa nchini Ujerumani juu ya mkakati mpya wa Ujerumani barani Afrika. Ujerumani inapaswa itoe ufafanuzi juu ya dhima ya kijeshi barani Afrika. Panajengeka mfungamano wa ujasiri baina ya mawaziri watatu wa Ujerumani, wa mambo ya nje, wa ulinzi na wa ushirikiano wa maendeleo. Na kwa haki kabisa Waziri wa ulinzi wa Ujerumani Ursula von der Leyen amekumbusha juu ya kushindwa kwa jumuiya yote ya kimataifa katika kuzuia mauaji ya kimbari nchini Rwanda na katika Kongo.Mawaziri hao watatu wanapaswa waifafanue dhima ya kijeshi ya Ujerumani katika baraza la mawaziri. Wanapaswa kuelekeza juhudi kwa lengo la kuanzisha mkakati wa usalama wa Umoja wa Ulaya na mgatuo wa majukumu.

.Hakuna taifa kubwa linaloonyesha haja ya kujiingiza kijeshi barani Afrika.Na kwa hivyo dhima kuu juu ya bara jirani linaiuangukia Umoja wa Ulaya.Inapasa kutambua kwamba uimara wa mabara ya Ulaya na Afrika unategemeana kama matukio ya Lampedus yalivyothibitisha. Ujerumani haiwezi kujifanya kuwa haioni kichatokea katika Jamhuri ya Afrika ya Kati au haiwezi kuiacha Ufaransa peke yake. Katika muktadha kama wa Jamhuri ya Afrika ya kati kinachotakiwa kwa Ujerumani kufanya ni kuonyesha dhamira na mshikamano. Kwa msemo wa wanajeshi ,Ujerumani inapaswa ionyeshe mshikamano wa imani katika jumuiya.