1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Kagame abakia - Demokrasia ya Rwanda ni ya uwongo

Andrea Schmidt
4 Agosti 2017

Katiba ya Rwanda inaruhusu mfumo wa vyama vingi lakini uchaguzi uliofanyika Agosti 4 hauwezi kuitwa sehemu ya ushindani wa vyama vingi, anasema Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya DW, Andrea Schmidt, katika maoni yake.

https://p.dw.com/p/2hihp
Ruanda Präsidentschaftswahlen Kampagne Präsident Paul Kagame
Picha: Reuters/J. Bizimana

Uchaguzi uliohusisha vyama vingi  nchini Rwanda ulikuwa ni kiini macho tu cha uchaguzi huru na wa haki. Mbali na rais Paul Kagame kutoka chama kinachotawala  cha RPF (Rwanda Patriotic Front), wagombea wengine wawili ambao waliruhusiwa kushiriki ni Frank Habineza wa Chama cha Kijani na mgombea wa kujitegemea Philipp Mpayiman. Pia kwa sababu ya ukosefu wa hali ya ushindani ni kutokuwepo mpinzani mkubwa dhidi ya Rais Paul Kagame. Vingine vyote vilikuwa ni vizingiti vya urasimu. Kagame kiongozi pekee mwenye mamlaka havumilii upinzani.

Muimla mwenye mafanikio

Ingawa amepata mafanikio makubwa, katika ukuaji wa uchumi kwa asilimia saba, mfumo mzuri wa afya, nchi yenye kiwango cha chini cha rushwa na upunguzaji wa umasikini. Hata hivyo, kama katika nchi nyingine za Afrika, ni wachache tu wanaonufaika. Ni mfano wa pazia linalong'ara. Katika barabara safi za mji wa Kigali huwa rahisi kwa wanasiasa wa kigeni kusahau kwamba katika nchi hiyo "wakulima" bado wanafanya kazi kwa kutumia pembejeo duni katika kulima mashamba yao. Pia wanaambiwa nini cha kupanda.

DW Kiswahili | Andrea Schmidt
Mkuu wa Idhaa ya Kiswahili ya DW, Andrea SchmidtPicha: DW/L. Richardson

Hata katika hali ya vikwazo kwa vyombo vya habari na uhuru wa maoni, kuna uwezekano mkubwa wa kupuuzwa mambo haya badala ya kuwekwa  shinikizo la kutosha. Tangu mauaji ya kimbari ya 1994 yalipotokea, chama cha RFP kimo katika mamlaka nchini Rwanda na Kagame amekuwa Rais wa nchi hiyo  tangu mwaka wa 2000. Kwanza, Wanyarwanda wengi walirudi nyumbani kutoka uhamishoni kwa lengo la kuja kusaidia katika ujenzi wa taifa lao, lakini leo hii wengi wanataka kuondoka nchini. Nani apendaye kuishi katika nchi ambamo kila mpinzani  anazuiwa kabla hata hajafungua mdomo wake.

Katika nchi nyingi za Afrika zinazotawaliwa na madikteta kwa mfano Burundi na Uganda, viongozi huruhusu mabadiliko ya katiba ili waweze kubakia madarakani kwa muda mrefu. Rais Kagame pia mnamo mwaka 2015, alibadili katiba katika kura ya maoni iliyoamrishwa na serikali yake kwa ajili ya kuondosha kizuizi cha rais kubakia madaraakani kwa mihula miwili tu.

Utulivu hauwezi kuhalalisa kila kitu

Kwa mujibu wa mtazamo wa kimataifa, Rwanda ni moja ya nchi zilizo imara zaidi barani Afrika. Kwa kauli mbiu inayosema bora udikteta unaoleta utulivu katika nchi kuliko machafuko. Hii ni kweli, hata hivyo, hoja ya mauaji ya kimbari isitumiwe kuendeleza udikteta kana kwamba hakuna njia nyingine. Kwa maoni ya Andrea Schmidt lawama kutoka nchi za nje ambazo hazileti tija sio haki. 

Kutokuelewana lazima kuwekwe wazi kabisa. Nchini  Rwanda hofu ni  ajenda ya juu kabisa, wanasiasa wanalazimika kukimbilia uhamishoni wengine wamo kwenye hali mbaya katika magereza na baadhi yao wametoweka bila ya maelezo.

Kagame sasa atatawala kwa miaka saba katika kipindi chake cha tatu kama rais wa Rwanda. Yanabaki kuwa matumaini kwamba katika muda mrefu huu, kutakuwepo na Rwanda iliyo huru, na kwamba jumuiya za kiraia zitapewa huru ili maendeleo ya kidemokrasia na uhuru wa maoni yaweze kuruhusiwa katika uchaguzi wa mwaka 2024 ambapo wagombea wa kweli wanaweza kushindana.  Kuna maana gani kuwa na aina hii ya uchaguzi? Katika hali yoyote demokrasia haipaswi kutumiwa kama kipodozi . Nchi yenye idadi kubwa ya vijana wanaotaka kushiriki katika michakato ya kisiasa nakuwa na uhuru wa kutoa maoni wasipoyapata, ni nchi inayoweza kulipuka.  Kuzuia hayo ni lazima kuwepo na shinikizo kutoka nje.

 

Mwandishi: Andrea Schmidt

Tafsiri: Zainab Aziz

Mhariri: Mohammed Khelef