1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya Cuba na Marakeni

Abdu Said Mtullya18 Desemba 2014

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani katika kurasa zao za maoni leo wanazungumzia juu ya uhusiano baina ya Cuba na Marekani na juu ya uamuzi wa Ujerumani wa kuwapeleka askari wake kaskazini mwa Irak

https://p.dw.com/p/1E6id
Watoto wakiwamo darasani nchini Cuba jee watanufaika na uhusiano mpya?
Watoto wakiwamo darasani nchini Cuba jee watanufaika na uhusiano mpya?Picha: picture-alliance/dpa

Gazeti la "Berliner" lnasema uamuzi wa Rais Obama wa kutaka kuurejesha uhusiano mzuri baina ya Marekani na Cuba ni wa kihistoria. Mhariri wa gazeti hilo anasema hata wakosoaji wake wanapaswa kukubali kwamba Rais Obama hakutunukiwa kwa makosa tuzo ya amani ya Nobel.

Mhariri wa gazeti la "Mittelbayerische" anasema uamuzi wa kuusawazisha uhusiano na Cuba ulipaswa kuchukuliwa siku nyingi na Marekani. Hata hivyo mhariri wa gazeti hilo amesema kuwa hatua iliyochukuliwa na Marekani ni ya kihistoria. Naye mhariri wa gazeti la "Rheinische Post" pia anasema uamuzi wa utawala wa Obama ,kuurejesha uhusiano mzuri na Cuba ni hatua ya kihistoria.

Hata hivyo mhariri huyo anakumbusha kwamba hatua za kujenga hali ya kuaminiana na kukaribiana baina ya Cuba na Marekani zilikuwa zinachuliwa kwa faragha tokea Rais Obama aingie madarakani. Lakini pia palikuwapo na kisengere nyuma katika hatua hizo. Na ndiyo sababu kwamba sasa inapasa kuyaharakisha mambo.

Wanajeshi wa Ujerumani kutoa mafunzo kaskazini mwa Iraq

Bunge la Ujerumani limekubaliana juu ya kuwapeleka wanajeshi wa Ujerumani hadi 100 kaskazini mwa Iraq, ili kutoa mafunzo kwa Wakurdi wanaopambana na wapiganaji wa dola la Kiislamu

Wanajeshi wa Ujerumani wakitoa mafunzo kwa Wakurdi wa Iraq
Wanajeshi wa Ujerumani wakitoa mafunzo kwa Wakurdi wa IraqPicha: Bundeswehr/Florian Räbel/dpa

Juu ya uamuzi huo gazeti la "Märkische Oderzeitung" linahoji kwamba watu wanaotishiwa na dola la kiislamu wanayo haki ya kusaidiwa ili waweze kuepuka kuuliwa zaidi, kubakwa,kuchinjwa na kutumikishwa kitumwa.

Lakini mahariri wa gazeti hilo anasema Ujerumani inapaswa ,kutambua jambo moja wazi kabisa. Kwa kuwapeleka askari wake kutoa mafunzo kwa Wakurdi wa kaskazini mwa Iraq, tayari inasimama dhidi ya upande wa dola la Kiislamu. Ndiyo kusema Ujerumani imo vitani vie vile. Na kwa hivyo Ujerumani inaweza kushambuliwa na magaidi kutokea ndani ya nchi.


Mhariri wa "Frankfurter Allgemeine" anakubaliana na uamuzi wa Bunge la Ujerumani wa kuwapeleka askari kaskazini mwa Iraq ili kuwaunga mkono wapiganaji wa Peshmerga wanaopambana na dola la Kiislamu.Lakini mhariri huyo anatahadharisha kwa kusema kuwa hakuna uhakika iwapo Wakurdi hao watafanikiwa kuwatimua wapiganaji wa dola la Kiislamu.Lakini inapasa kuwasaidia kwa kadri itakavyowezekana.

Wanajeshi wa Peshmerga hawapigani kwa ajili yao tu au kwa ajili ya jirani zao, bali wanapigana pia kwa niaba ya nchi za magharibi.

Mwandishi:Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri: : Yusuf Saumu