1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya Italia na maafa ya Bangladesh

Abdu Said Mtullya25 Aprili 2013

Pamoja na masuala mengine wahariri wa magazeti wanazungumzia juu ya juhudi za kuunda serikali nchini Italia na dhamira ya Uswisi ya kupunguza idadi ya wahamiaji.

https://p.dw.com/p/18NJc
Enrico Letta alieteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Italia
Enrico Letta alieteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa ItaliaPicha: Reuters

Wahariri wa magazeti pia wanatoa maoni juu ya mkasa uliotokea nchini Bangladesh baada ya jengo moja la kiwanda kuporomoka.

Gazeti la "Die Welt" limeandika juu ya kuteuliwa kwa Enrico Letta kuwa Waziri Mkuu wa Italia. Mhariri wa gazeti hilo anakumbusha kwamba,alipokuwa Waziri Mkuu wa Italia Silvio Berlusconi alichimba handaki kati ya kambi za mirengo ya kushoto na kulia. Hakutoa japo mwanya tu wa mwafaka. Mhariri wa "Die Welt" anaeleza kuwa sasa jukumu la kuzileta kambi hizo mbili pamoja litapaswa kubebwa na Enrico Letta alieteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Italia.

Rais wa Italia Napolitano hivi karibuni alikumbusha juu ya imani ya miaka ya 70 ambapo wanasiasa wa Christian Demokratik walipeana mikono na Wakomunisti. Ilikuwa hatua ya kihistoria ya kuuondoa mzibo wa kisiasa nchini Italia wakati huo.Ni matumaini ya kila mtu kwamba moyo kama huo utarejea tena nchini Italia leo.

Gazeti la "Frankfurter Allgemeine" linasema Enrico Letta aliepewa jukumu la kuunda serikali nchini Italia ni mtu mwenye tajiriba ya kisiasa licha ya kuwa na umri wa miaka 46 tu. Na huo ujana wake ndiyo unaomfanya azipe kisogo siasa za kale za nchini Italia. Jawabu, kwake ni kuunda serikali ya mseto.

Uswisi yafunga milango kwa wahamiaji

Uswisi imeamua kuifunga milango yake kwa wahamiaji kutoka nchi za Umoja wa Ulaya. Juu ya hatua hiyo gazeti la "Schwarzwälder Bote" linasema wote wanapaswa kusikia juu ya hatua hiyo.Hatua hiyo ni sawa na kulitovuga jeraha. Barani Ulaya pana mgogoro wa madeni,nchini Italia kuna mgogoro wa kisiasa.Gazeti hilo linasema bara la Ulaya lina kizunguzungu! Kila mtu anatafuta njia ya kutoa duku duku lake, iwe ni kwa sababu ya kulinda nafasi za kazi za wananchi wake iwe ni uhaba wa nyumba au wasiwasi wa wananchi. Hatua ya Uswisi kuifunga milango yake kwa wahamiaji kutoka Umoja wa Ulaya,siyo uvumbuzi wa nchi hiyo tu. Jee bara la Ulaya linaelekea wapi?

Maafa ya Bangladesh:

Gazeti la "Märkische Oderzeitung" linatoa maoni juu ya maafa yaliyotokea nchini Bangladesh kufuatia kuporomoka kwa jengo moja la kiwanda na kusababisha msiba mkubwa. Gazeti linasema wa kulaumiwa kwa maafa hayo siyo mkandarasi wa ujenzi tu. Bali pia wateja, kwa sababu ya kutaka rahisi.Wakati wa kununua mahitaji watu wanaangalia bei tu! Lakini bei rahisi mbele, mauti nyuma!

Mwandishi:Mtullya abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri:Josephat Charo