1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya mauaji ya Newtown

Abdu Said Mtullya18 Desemba 2012

Pamoja na masuala mengine wahariri hao wanatoa maoni yao juu ya mauaji yaliyotokea katika jimbo la Connecticut Marekani. Jee sheria juu ya kumiliki silaha itabadilishwa nchini Marekani?

https://p.dw.com/p/174Rq
Maombolezo wa watu waliouawa Newtown,Connecticut
Maombolezo ya watu waliouawa Newtown,ConnecticutPicha: Reuters

Mhariri wa "Berliner Zeitung" anasema watetezi wa silaha pamoja na wajumbe wa chama cha Republican wanazuia mageuzi juu ya sheria ya kudhibiti umiliki wa silaha.Watu hao wanahoji kwamba sheria hiyo inatokana na mabadiliko ya katiba yaliyofanyika mnamo mwaka wa 1791.

Lakini mhariri wa "Berliner Zeitung" anawakumbusha wapinzani wa mageuzi kwamba sheria hiyo ilipitishwa wakati Marekani ilipokuwa ni mkusanyiko tu wa nchi zilizokuwamo katika vurumai.

Mhariri wa gazeti la "Delmenhorster Kreisblatt" anasema ibara ya pili katika katiba ya Marekani inayohakikisha uhuru wa watu binafsi kumiliki silaha, inafaa kutupwa katika jaa la historia. Lakini mhariri huyo ana mashaka iwapo hilo linaweza kufanyika hata baada ya mauaji ya Newtown.

Lakini hata hivyo mhariri anasema Ibara hiyo haitatupwa katika jaa la historia. Kwa namna moja au nyingine yatatokea mauaji kama yale yaliyotokea Newtown na katika sehemu nyingine. Kwani hayo ndiyo malipo, katika jamii isiyotaka kuibadilisha sheria ya kumpa kila mwananchi binafsi, haki ya kumilki silaha.

Tatizo si sheria ni mtazamo

Gazeti la "Nürnberger "linasema tatizo la Marekani siyo sheria inayowapa watu haki ya kumiliki silaha.Bali tatizo ni mitazamo ya watu wenyewe.Mhariri huyo anafafanua kwa kusema kwamba hata ikiwa sheria itafanyiwa mageuzi, ili iwe vigumu kwa watu kupata silaha ,hakuna kitachobadilika. Tayari pana bunduki ,300,000,000 zilizomo katika mikono ya wananchi mbalimbali.

Gazeti linasema tatizo nchini Marekani siyo umiliki wa silaha bali ni mtazamo wa mtu unaomwezesha kuitimia. Anaeleza kuwa tofauti na Ulaya, msingi wa jamii ya Marekani ni matumizi ya mabavu, na mpaka leo mtazamo huo bado haujabadilika.

Syria yazidi kubomolewa

Hali inazidi kuwa mbaya nchini Syria. Hayo ni maoni ya gazeti la "Handelsblatt"
Mhariri wa gazeti hilo anasema matumaini ya pekee yaliyobakia ni kwa Urusi na China kuchukua hatua za kisiasa ili kuubabilisha msimamo wa Rais Assad.

Lakini kwa sasa suala halimo katika ajenda.Kwa sababu nchi za magharibi mpaka sasa hazijatoa ishara kwa China na Urusi . Assad anaendelea kuwamo madarakani kwa sababu Urusi na Iran bado zimeshikamana naye. Mwisho wa Assad utakuja haraka ikiwa nchi hizo zitamtelekeza.

Mwandishi:Mtullya Abdu.Deutsche Zeitungen:

Mhariri: Josephat Charo