1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya mkutano wa G7

Abdu Said Mtullya5 Juni 2014

Katika maoni yao wahariri wa magazeti ya Ujerumani wanazungumzia juu ya mkutano wa nchi za G 7 juu ya Syria na hotuba iliyotolewa na Rais Obama wakati wa ziara yake nchini Poland.

https://p.dw.com/p/1CCc6
Mkutano wa kilele wa viongozi wa G7 mjini Brussels
Mkutano wa kilele wa viongozi wa G 7 mjini BrusselsPicha: Reuters

Gazeti la "Rhein" linauzungumzia mkutano wa nchi zinazoongoza katika maendeleo ya viwanda duniani, zinazojulikana kama G Saba. Viongozi saba wa nchi hizo wamekutana mjini Brussels. Mhariri wa gazeti la "Rhein" anasema viongozi hao wameitumia sehemu kubwa ya mkutano wao pia kumjadili Rais Vladimir Putin wa Urusi kutokana na matukio ya nchini Ukraine.

Mhariri wa gazeti hilo anasema sasa Rais Putin anapaswa kuamua, kwa sababu miito ya kuiwekea Urusi vikwazo zaidi inazidi kuwa ya sauti za juu. Siasa kali ya Putin juu ya Ukraine inaweza kuwa na madhara makubwa kwake.

Mhariri wa gazeti la "Rhein" anautilia maanani ujumbe unaotoka kwa viongozi wa nchi za G Saba mjini Brussels unaosisitiza matumaini ya kupatikana suluhisho la mgogoro wa nchini Ukraine.

Japo hayupo lakini lake Putin lipo

Gazeti la "Thüringische Landeszeitung" linasema Rais Putin mwenyewe hakuwepo kwenye mkutano wa viongozi wa nchi za viwanda mjini Brussels lakini jina lake lilikuwamo vinywani kwenye mkutano huo.

Mhariri wa gazeti hilo anaeleza kwamba Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ametoa masikitiko yake kwamba mkutano wa mjini Brussels umefanyika bila ya ushiriki wa Rais Putin. Hata hivyo yapo matumaini kwamba Putin atashiriki kwenye mkutano ujao nchini Ujerumani. Lakini kwa sasa yaliyopo ni matumaini tu, kwamba Urusi itaibadilisha sera yake juu ya Ukraine. Nchi za magharibi zinaweza kuweka vikwazo zaidi. ikiwa pamoja na kuacha kabisa kuagiza gesi na mafuta kutoka Urusi. Lakini mazungumzo baina ya pande mbili hizo yanapaswa kupewa kipaumbele.

Mshikamano na Ulaya Mashariki

Gazeti la "Darmstädter Echo" linaizungumzia hotuba iliyotolewa na Rais Obama nchini Poland.Gazeti hilo linaeleza kuwa Rais Obama amesisitiza mshikamano na Poland na nchi zote za Ulaya mashariki zilizomo katika mfungamano wa kijeshi wa NATO. Watu wengi nchini Poland na katika nchi nyingine za Ulaya mashariki wamekuwa wanasuburi kuisikia kauli kama hiyo.

Jee Assad aendelee madarakani?


Mhariri wa gazeti la "Südwest Presse" anaizingatia hali ya kisiasa ya nchini Syria baada ya Rais Assad kutangazwa mshindi wa uchaguzi .Mhariri huyo anasema Rais Assad anaishi na uhakika kwamba utawala wake utaimarika angalau katika maeneo yanayodhibitiwa na serikali yake. Assad anahisi kuwamo katika njia ya ushindi na kwamba wapinzani wake hawataweza kumwondoa madarakani katika miaka ijayo.Na kutokana na hali hiyo wapinzani wake wote wa ndani na wa nje kadhalika wanajiuliza iwapo sasa waachane na mpango wa kutaka kumwangusha na wakubali utawala wake uendelee kuwapo.Kwani bila ya hivyo.

Mwandishi:Mtullya abdu.Deutsche Zeitungen.

Mhariri:Yusuf Saumu