1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obam ataka nishati safi

Admin.WagnerD4 Agosti 2015

Wahariri karibu wote wanatoa maoni juu ya mpango uliozinduliwa na Rais Obama juu ya kuwapa Wamarekani nishati safi.Lakini pia wanazungumzia juu ya uwezekano wa Kansela Merkel kuwania muhula wa nne

https://p.dw.com/p/1G9Qt
Rais Barack Obama
Rais Barack ObamaPicha: Reuters/J. Ernst

Gazeti la "Hannoversche Allgemeine" linautilia maanani mpango uliozinduliwa na Rais Barack Obama wa kuwapa Wamerekani nishati safi.Obama anataka Marekani ipunguze gesi chafu kwa asilimia 32 hadi kufikia mwaka wa 2030.

Mhariri wa gazeti hilo anasema lengo la Obama ni zaidi kuliingiza jina lake katika vitabu vya historia kuliko kuleta mabadiliko ya kweli katika ulinzi wa mazingira.

Hata hivyo mhariri wa gazeti la "Hannoversche Allgemeine" anasema ikiwa Marekani itaanza kuleta mageuzi katika suala la mabadiliko ya tabia nchi, China, Brazil na India nazo zitaiona haja ya kuwajibika.

Mhariri wa gazeti la "Badische" anasema mpango uliozinduliwa na Rais Obama utawapa wajumbe wa Marekani kwenye mkutano wa mjini Paris,uwezo wa kuzishinikiza nchi nyingine.

Naye mhariri wa "Thuringer Allgemeine" anasema Obama anataka Marekani ipunguze utoaji wa gesi chafu kwa asilimia 32 hadi kufikia mwaka wa 2030.Hizo ni habari za kusisimua. Lakini anauliza jee itawezekana kuutekeleza mpango huo. Wenye viwanda vinavyotumia nishati ya makaa ya mawe nchini Marekani,siku nyingi walikubaliana na Republican kwamba lengo hilo haliwezi kufikiwa. Watu hao hawatakubali mpango wa Obama utekelezwe.

Republican wajitayarisha kumpinga Obama


Na mhariri wa "Thüringische"anatilia maanani kwamba mpango wa Obama utawapa Republican zana katika kampeni ya uchaguzi wa Rais. Mhariri huyo anaeleza kwamba watu wa Republican wanalifurahia pendekezo la Rais Obama. Siyo ati kwa sababu ya kuliunga mkono, bali kwa sababu mabepari wakubwa wenye viwanda vya mafuta na makaa ya mawe watatoa fedha zaidi kwa ajili ya kampeni ya kuwapigia debe Republican.

Mpango wa Obama unawapa Republican motisha wa kufanya kila linalopasa kumzuia mjumbe wa chama cha Demokratik kuingia Ikulu. Gazeti la " Rhein" linazungumzia juu ya uwezekano ,kwamba huenda Kansela wa Ujerumani Angela Merkel akawania muhula wa nne wa ukansela. Juu ya uwezekano huo mhariri wa "Rhein" anasema:

Mifano imeonyesha kwamba mwisho wa kukaa sana madarakani, ni kupata sura mbaya. Mfano ni yale yaliyotokea kwa kansela wa hapo awali Helmut Kohl.Katika siku za mwisho, baada ya kukaa muda mrefu madarakani, Ujerumani ilipata sura ya mkwamo, msongamano wa mambo yaliyohitaji mageuzi na sura uchovu. Kukaa sana madarakani kunasababisha ulemavu wa macho- kiongozi anakuwa haoni tena.

Mwandishi: Mtullya Abdu./Deutsche Zeitungen.

Mhariri: Mohammed Khelef