1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya vifo vya vijana wa Israel

Abdu Said Mtullya2 Julai 2014

Wahariri wanatoa maoni juu ya msimamo wa Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu juu ya vifo vya vijana watatu wa nchi yake.Na pia wanaizungumzia hukumu ya Mahakama ya Ulaya juu ya vazi la Burka.

https://p.dw.com/p/1CUQg
Israeel yaomboleza vifo vya vijana watatu wa kiyahudi
Israel yaomboleza vifo vya vijana watatu wa kiyahudiPicha: DW/K. Shuttleworth

Gazeti la "Eisenacher Presse" linautazama msimamo wa baadhi ya wanasiasa wa nchini Israel juu ya vifo vya vijana watatu wa nchi hiyo. Mhariri wa gazeti hilo anasema msimamo wa wanasiasa wa Israel, wenye mrengo mkali, wa kutaka kutumia nguvu dhidi ya Hamas kama jibu la vifo vya vijana hao, unaweza kueleweka, hatahivyo mhariri huyo anahoji kwamba hakuna atakaefika mbali na matumizi ya nguvu.Anasema matumizi ya nguvu yataleta maafa katika pande zote.


Mahariri wa gazeti la "Stuttgarter Nachrichten"anasema kutumia nguvu dhidi ya Wapalestina siyo suluhisho la mgogoro wa Mashariki ya Kati. Inapasa kuitafuta sababu ya mgogoro wenyewe.

Kuuliwa vijana watatu wa kiyahudi ni shambulio dhidi ya Israel

Gazeti la "Kieler Nachrichten" pia linazungumzia juu ya vifo vya vijana watatu wa Kiisraeli. Mhariri wa gazeti hilo anaeleza kuwa kwa serikali ya Israeli, kuuliwa vijana hao watatu, siyo tu ni kosa la mauaji, bali pia ni shambulio dhidi ya nchi ya Israel.Lakini huko ni kutia chumvi nyingi sana,sawa na kuutumia msemo wa agano la kale",jino kwa jino na jicho kwa jicho."Tunamtaka kiongozi wa Israel,Benjamin Netanyahu aitumie busara ,lakini litakuwa kosa kuilaumu Israel kwa mvutano unaopamba moto sasa.

Kuhusu hali ya mvutano katika Mashariki ya Kati hivi sasa gazeti la "Nurnberger " linatilia maanani kwamba katika pande zote mbili, ule wa Israel na ule wa Wapalestina, wapo watu wasiotaka amani.Gazeti hilo linasema yapo makundi yanayohamasishwa na matukio ya nchini Iraq.

Vazi la Burka marufuku nchini Ufaransa

Jee vazi la Burka,la kuufunika uso wote wa mwanamke, linastahili kupigwa marufuku?. Ufaransa imeichukua hatua hiyo na sasa imethibitishwa na Mahakama ya Ulaya ya haki za binadamu.Gazeti la "Mannheimer Morgen" linauliza jee ni sawa kwa jamii kuwaruhusu wanawake fulani watembee wakiwa wamejifunika nyuso gubi gubi? Jibu ni moja tu,siyo sawa

.Ni sahihi kwa mahakama ya Ulaya ya haki za binadamu,kuithibitisha hukumu ya mahakama ya Ufaransa ya kulipiga marufuku vazi la Burka.Vazi hilo linauzuia mtangamano wa jamii. Na gazeti la "Pforzheimer " linasema mahakimu wameitoa hukumu sahihi. Vazi la Burka la kuufunika uso wote wa mwanamke halihusiani na uhuru wa dini wala uhuru wa mtu binafsi. Vazi hilo ni ishara ya udhalimu, ishara ya kukandamizwa kwa binadamu. lazima liondolewe mbali kwenye mitaa ya barani Ulaya.

MODE:...Concl...

Mwandishi:Mtullya Abdu./Deutsche Zeitungen.

Mhariri:Yusuf Saumu.