1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo

Josephat Nyiro Charo21 Julai 2009

Mzozo wa serikali ya jimbo la Schleswig-Holstein, mauaji Afghanistan na uhaba wa waalimu Ujerumani

https://p.dw.com/p/Itqw
Waziri mkuu wa Schleswig-Holstein Peter Harry Carstensen (CDU)Picha: AP

Gazeti la Frankfurter Allgemeine Zeitung limejishughulisha na mzozo ndani ya serikali ya jimbo la Schleswig-Holstein. Mhariri wa gazeti hilo anasema kwa kuwa chama cha Christian Democratic Union, CDU, kimekuwa kwa miezi kadhaa iliyopita kikitafuta sababu ya kuivunjuka serikali ya muungano na chama cha Social Democratic, SPD, hatua hii bila kutiliwa shaka inaoana na matokeo ya kura.

Hususan juu ya mtu mmoja; naye ni bwana Ralf Stegner, mwenyekiti wa chama cha SPD katika jimbo la Schleswig-Holstein. Yeye na waziri mkuu wa jimbo hilo, Peter Harry Carstensen ni watu wawili wenye hulka tofauti kabisa.

Wakati viongozi wa vyama wanapokuwa na maelewano mazuri basi chama cha CDU na chama cha SPD kwa pamoja viwaweza kufanikisha mambo kadha wa kadha. Lakini hilo pengine linafanyika mashariki mwa Ujerumani kuliko eneo la magharibi mwa nchi.

Huku serikali ya mseto ya jimbo la Scleswig-Holstein mjini Kiel ikiwa imevunjika, vyama vya CDU na SPD katika majimbo ya Mecklenburg-Vorpommern, Sachsen, Sachsen-Anhalt na Brandenburg, vinafanya kazi kwa pamoja na kwa karibu bila kutoa kauli za malumbano.

Nalo gazeti la Die Welt kuhusu hali katika jimbo la Schleswig-Holstein kaskazini mwa Ujerumani linaileza kuwa tukio la kipekee. Mhariri wa gazeti hilo anasema serikali za mseto mara nyingi zinakuwa hazivutii, kwa hiyo ingawa vyama katika serikali hufanya kazi kwa pamoja, serikali kwa ujumla inakuwa utendaji wake si barabara.

Katika jimbo la Schleswig-Holstein mambo yalikuwa tofauti. Chama cha Christian Democratic Union, CDU na chama cha Social Democratic Party, SPD, viliungana kuunda serikali kwa sababu hapakuwa na njia nyingine. Serikali hii ya mjini Kiel tangu mwanzoni ilikuwa na dalili za kuwa uwanja wa mivutano.

Deutschland SPD Schleswig-Holstein Ralf Stegner
Mwenyekiti wa chama cha SPD jimboni Schleswig-Holstein Ralf StegnerPicha: picture-alliance/ dpa

Na hii si kwa sababu tu kwamba waziri mkuu wa jimbo la Schleswig-Holstein, bwana Peter Harry Carstensen na mwenyekiti wa chama cha SPD katika jimbo hilo, Ralf Stegner, walikuwa hawaelewani kama moto na maji, bali kwanza kabisa, ni kutokana na kwamba vyama vya vya CDU na SPD kwa zaidi ya miongo miwili vimekuwa vikihasimiana tangu kifo cha Uwe Barschel, mwanasiasa wa chama cha CDU, aliyekuwa waziri mkuu wa jimbo la Schleswig-Holstein kati ya mwaka 1982 na 1987. Uchunguzi uliofanywa haujafaulu kubainisha wazi ikiwa mwanasiasa huyo alijiua mwenyewe au aliuwawa.

Mauaji Afghanistan

Kuhusu kifo cha kijana wa Afghanistan aliyepigwa risasi na wanajeshi wa Ujerumani nchini Afghanistan, gazeti la Süddeutsche Zeitung linasema kwa mara nyingine raia wa Afghanistan na ambaye bado ni kijana ameuwawa. Kwa mara nyingine tena waongozaji mashataka watafanya uchunguzi dhidi ya wanajeshi hao wa kulinda usalama. Na kwa mara nyingine tena kesi hiyo yumkini ikawa ndefu.

Gazeti la Süddeutsche Zeitung linasema matatizo mengi ya wanajeshi bado hayajatutiliwa, kwa sababu bunge na serikali haijatoa muongozo mpya wala kuanzisha mipango yoyote ya kuandaa muongozo mpaka wa leo. Katika muongozo huo kunatakiwa kuwepo jopo la mawakili ambalo litakuwa likiwasimamia wanajeshi wanaofanya makosa katika eneo fulani walikotumwa kuhudumu.

Uhaba wa waalimu Ujerumani

Hapa Ujerumani jumuiya ya waalimu imetangaza kuwepo kwa uhaba wa waalimu katika shule za humu nchini kwa masomo ya hesabu na sayansi. Gazeti la Die Rheinpfalz kutoka mjini Ludwigshafen lina wasiwasi kuhusu kulitatua tatizo hilo kwa kuchukua waalimu kutoka nchi za Ulaya Mashariki.

Gymnasium, Schülerin meldet sich
Somo likiendelea katika darasa la 11c shule ya Justus-Liebig-Gymnasium huko DarmstadtPicha: dpa

Waokozi kutoka Romania, Bulgaria na Hungary sasa wanaweza kuja Ujerumani, lakini ingawa waalimu kutoka Mashariki mwa Ulaya wamepata ujuzi barabara wa taaluma yao, jumuiya ya waalimu ya Ujerumani imesema watalazimika kurudi darasani kwanza.

Kuja kwao kutapunguza pengo lililopo, lakini hakutalitaua tatizo zima. Uhaba wa waalimu Ujerumani umesababishwa humu humu nchini, huku sera ya elimu ikishindwa kuwafunza vijana na kuwapa ajira ili kuweza kutolesheleza mahitaji ya elimu nchini.

Gazeti la Rheinpfalz linamalizia kwa kusema, kwa kuwa waalimu wanapungua mashuleni na mchanganyiko wa waalimu vijana chipukizi na wazee wenye uzoefu wa miaka mingi haupo madarasani, uhaba huu wa waalimu ulitabarika kirahisi.