1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni:Mapambano dhidi ya Boko Haram nchini NIgeria

8 Mei 2014

Mashambulio na visa vya kutekwa nyara watu vinavyofanywa na Boko Haram vimevuruga juhudi za rais Jonatrhan za kutaka kuitakasa hadhi ya Nigeria.Badala yake ulimwengu unashuhudia kushindwa sera zake

https://p.dw.com/p/1Bvae
Mkuu wa matangazo ya lugha za kiafrika,kiiengereza na kifaransa za DW kwa bara la Afrika,Claus StäckerPicha: DW

Eti wasichana waliotekwa nyara ni 200,276 au zaidi ya 300?Eti wamepelekwa Kamerun,Tchad au bado wanakutikana katika misitu ya kiza kaskazini mashariki ya Nigeria kama baadhi ya mashirika ya habari yanavyoashiria?Suala la maelezo kamili halitiliwi maanani sana nchini Nigeria.Hakuna ajuaye kwa uhakika,na kama yupo haruhusiwi kusema.

Rais aliyechaguliwa kwa njia za kidemokrasia,lakini anaezongwa na mambo mengine,Goodluck Jonathan,anaonekana kupendelea zaidi kuitumbukiza kidogo kidogo nchi hiyo mikononi mwa wanajeshi.Analitegemea jeshi kuhakikisha anachaguliwa tena uchaguzi utakapoitishwa mwaka 2015.Wanaomkosoa,hata wale wenye nia njema,wanatolewa kazini.Baadhi yao wanafika hadi ya kutumbukizwa korokoroni.

Katika mikoa yote,tangu miezi kadhaa sasa sheria ya hali ya hatari inatumika,vizuwizi vimewekwa majiani , watu wanazuwilia kutoka,na hakuna habari zinazotoka nje.

Watu 600 wameuliwa na Boko Haram katika kipindi cha miaka mitano iliyopita

Kwa namna hiyo sio visa vyote vya kutekwa nyara watu na Boko Haram vinavyojulikana.Hata mashambulio ni nadra mtu kupata habari za kuaminika.Watu 106 waliuliwa kati kati ya mwezi wa Februari.Zaidi ya 40 mwishoni mwa februari.106 mwezi wa April,zaidi ya 200 jumanne iliyopita.Idadi ya wahanga inaonyesha kipeo cha huzuni na machungu-lakini hakuna anaeweza kuithibitisha.Katika kipindi cha chini ya miaka mitano wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam Boko Haram wameuwa watu wasiopungua 6000.Jeshi linajibu kwa kufanya mashambulio ya kulipiza kisasi yanayoangamiza maisha hata ya wale wasiokuwa na hatia na kwa namna hiyo kuzidi kupalilia uhasama.

Tume zinaundwa, na ripoti kuandikwa,majadiliano lakini hakuna.Rais Goodluck Jonathan anaamini anaweza kuwavunja nguvu Boko Haram kupitia opereshini za kijeshi.Anataka aonekane kama shujaa kabla ya uchaguzi na kiongozi mwenye kujiamini.Nigeria iliyogeuka nguvu ya kiuchumi barani Afrika ilitaka ionekane kama mshika bendera wa bara hilo.Hesabu zimethibitisha:pato la kila mkaazi mmoja katika nchi hiyo yenye wakaazi milioni 170 limepindukia mara tatu lile la Afrika kusini.Na kongamano la kiuchumi la mjini Abuja,badala ya kutoa picha ya ustawi na neema linagubikwa na mtafaruku;Kuna wanaotoa udhuru,wanaolalamika na wengine wanaozusha masuala ya ukosefu wa usalama.

Jonathan mpaka sasa hakutafuta njia ya kukutana si na familia za wahanga wa mashambulio ya kigaidi wala njia ya kuzungumza na wafuasi wa itikadi kali-mfanao kupitia wakuu wa kidini.

Mshikamano wa kimataifa angalao unawapangusa machozi wa Nigeria

Kutekwa nyara wanafunzi wa kike kati ya 200 na 300 nchini Nigeria kumeiathiri vibaya sana hadhi yake.Hasira na uchungu wa akina mama wanaoandamana tangu siku kadhaa zilizopita mjini Abuja, hazielekezwi tena dhidi ya wanamgambo hao wa itikadi kali-zinakosoa zaidi uzembe wa serikali.Kwamba ulimwengu,kutokana na mawasiliano kupitia tovuti na mitandao ya kijamii uko pamoja nao katika wakati huu mgumu,pengine ,hali hii inawapa moyo.Hata rais wa Marekani anaona analazimika kuwajibika.Kwasababu na huko pia kila siku wanigeria wanateremka majiani kudai wasichana hao waachiliwe huru.Kwamba ulimwengu umepania kusaidia kuwakomboa wasichana hao ni jambo linalowapanguza machozi japo kidogo wanigeria.

Mwandishi:Stäcker,Claus/Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Yusuf Saumu