1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapatano-D.R Kongo-Ruanda

25 Februari 2009

mafanikio kwa rais Kabila ?

https://p.dw.com/p/H1AT

Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, anatazamiwa wiki hii kuwatuma wajumbe wake kwa mazungumzl zaidi na waasi .Hii ni baada ya kupata mafanikio kadhaa huko Mashariki mwa Kongo, ambako juu ya hivyo, yungali akikabiliwa na mitihani mingi.

Msingi wa maafikiano na Jeshi la waasi la National Congress for Defennse of the People (CNDP) ulitiwa saini Jumapili baada sehemu kubwa ya maamirijeshi wake kumpa mgongo Kiongozi wao Jamadari Laurent Nkunda.Nkunda alitiwa nguvuni ndani ya ardhi ya nchi jirani ya ruanda hapo Januari 22.

Mapatano hayo yanatazamiwa kuimarishwa na wapatanishi katika utaratibu wa amani mjini nairobi na unaweza ukachangia kurejesha amani katika jimbo la kaskazini mwa kivu huko mashariki mwa Kongo .Mkoa huo muda mrefu umekuwa shina la ugomvi katika eneo la Maziwa Makuu.

Kukamatwa kwa Jamadari Nkunda kulizusha pirikapirika nyingi za kukwamua mambo,kwavile alidhibiti eneo kubwa la nchi hii tajiri sana kwa mali ya asili.Wakati huo huo vikosi vya pamoja vya rais Kabila na vya rais Kagame wa Rwanda vilishirikiana kufanya hujuma isiowahi kuonekana kabla mwishoni mwaka jana dhidi ya waasi wa Rwanda huko mashariki.

Mafanikio ya hujuma hizo yameongoza kutokea "mapinduzi madogo" katika Maziwa makuu -hii ni kwa muujibu wa mjumbe mmoja wa kibalozi.Afisa mmoja wa Umoja wa Mataifa mjini Kinshasa, ameliambia shirika la habari la AFP kuwa ngome kubwa ya chama cha waasi cha FDLR imengolewa.

Vikosi vya Ruanda kati ya 1996-97 na tena 1998-2003 viluipigana na vikosi vya jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo vilivyoingiza majeshi ya zaidi ya nchi darzeni 1 za kiafrika katika kile kilichoitwa "vita 3 vya dunia".Vinasemekana kusababisha vifo vya hadi watu milioni 3 tukiegemea mashirika ya haki za binadamu.

Jamadari Nkunda,mtusi akiangaliwa na wengi kuwa akitumiwa na Ruanda kama turufu katika karata za siasa za maziwa makuu dhidi ya jeshi la FDLR linalojumuisha zaidi wahutu waliokimbilia Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo baada ya mauaji ya kimbari zaidi dhidi ya watutsi1994.Wakati ule ,kiasi cha watu laki 8 waliuwawa.

"Kamari alioicheza Kabila, imefanya kazi"-gazeti linaloelemea serikali " L-Observateuer"lilisema kufuatia makubaliano ya mwishoni mwa wiki yanayofungua sasa mlango wa mapatano ya amani baada ya vikosi vya Ruanda kuhama jana aridhi ya Kongo.

Pale majeshi ya Ruanda yalipotumbukia ardhi ya Kongo kupambana na waasi wa Nkunda,hasira zilipanda Ikulu mjini Kinshasa kuona maadui wa zamani wamekaribishwa rasmi katika ardhi ya Kongo.ilikua wakati ambapo mafanikio ya mradi wao si wsazi na hayajulikani.

Hakuna alietazamia majeshi ya ruanda baadae kuondoka haraka nchini Kongo.Kuna waliodai miongoni mwao afisa wa UM kuwa sherehe ya jana ya kuhama kwa vikosi vya Ruanda huko Goma, mpakani na Ruanda ni kiini macho tu.

Wachunguzi kadhaa pia wa siasa za maziwa makuu wakidai pia mazungumzo na chama cha CNDP chini ya upatanishi wa rais wa zamani wa Nigeria Olusegun Obasanjo na rais wa zamani wa Tanzania Benjamin M kapa,huenda yakachafuliwa na mzozo wa kuania uongozi katika jeshi la waasi kutokana na kutiwa nguvuni kwa Jamadari Nkunda.