1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapigano Sudan Kusini yaongeza njaa

18 Oktoba 2017

Karibu nusu ya raia wa Sudan Kusini wanategemea chakula cha msaada. Tatizo hili halisababishwi tu na ukame ulioko nchini humo bali pia vya kuwania mamlaka vinavyoendelea.

https://p.dw.com/p/2m6GQ
Präsident der Republik Südsudan Salva Kiir Mayardit
Picha: imago/photothek/T. Koehler

Wanawake hasa ndiyo huathirika kutokana na njaa na machafuko.

Muda mfupi baada ya kuzuka kwa mapigano ya wenyewe kwa wenyewe Sudan Kusini mwaka 2013, Umoja wa Mataifa ulijenga kambi ya kuwahifadhi raia na kwa sasa karibu watu 200,000 wanahifadhiwa katika kambi hiyo. Kutokana na mapigano hayo, mzozo wa njaa ulizuka katika nchi hiyo.

Hannah Nyarure anasubiri chakula pamoja na wanawake wengine na mara nyingi, mama huyu amejaribu kupata msaada wa Umoja wa Mataifa akiwa na wanawe na amerudi nyumbani bila chochote.

"Hali ya usalama sio nzuri kabisa lakini ninapokuwa nyumbani kijijini kwangu naweza kupanda nafaka na mboga," alisema Nyarure.

Wapiganaji huwadhulumu wananchi vyakula vya msaada

Hata hivyo ni lazima atembee mwendo wa saa tano kuelekea katika eneo la kugawanya chakula katika kambi hiyo kila mwezi. Msimu wa mwisho wa mvua ulikuwa mfupi na Hannah Nyarure hakuweza kupanda chochote kabisa. Lakini kibaya zaidi ya ukosefu huo wa mvua ni vita visivyo na mwisho na hata kitu chochote kinapoota mashambani, wanajeshi wa serikali na waasi watakuja na kuchukua watakacho kwa nguvu.

Rebellen in Südsudan
Wapiganaji huwadhulumu wanawake chakula cha msaadaPicha: Reuters/G. Tomasevic

Hata kwa chakula cha msaada anachopata katika kambi, anadhulumiwa kiasi kikubwa.

"Kutembea njiani ukiwa na chakula sio salama lakini hatuna namna. Wapiganaji wanakichukua chakula kama kawaida na kutuachia sisi kidogo," alisema Nyarure.

Thomas Hoerz anafahamu vyema masaibu wanayopitia wanawake kama Nyarure kwa kuwa yeye ni mratibu wa chakula cha msaada kutoka Ujerumani kinachotolewa huko Bentiu.

"Iwapo tungefungua vituo vingi zaidi vya kugawa chakula, hilo lingekuwa jambo bora kwa watu hususan kwa wanawake. Lakini hilo linatuhatarisha sisi pamoja na wafanyakazi wetu," alisema Hoerz. "Kadri eneo la makaazi lilivyo dogo ndivyo ilivyo vigumu kuwahakikishia usalama wafanyakazi wetu wenyewe," aliongeza Hoerz.

Vijana wanastahili kujiondoa katika mapigano

Mwanahabari wa Sudan Kusini Parach Mach, amekuwa akiripoti kuhusiana na hali hii ya machafuko kutokea mwanzo, kuhusiana na mapigano ya kuwania mamlaka baina ya rais Salvar Kiir na aliyekuwa makamu wake Riek Machar, hadi pale yalipogeuka na kuwa mapigano ya kikabila. Mwanahabari huyu anaeleza, makundi yote yaliyojihami yamefanya uhalifu mkubwa, na kati ya wapiganaji hao mara nyingi kuna watu wanaoteseka kwa njaa.

Südsudan Frauen mit Säcke in Nimini village
Wanawake wa Sudan Kusini wakiwa wamebeba chakula cha msaadaPicha: Reuters/S. Modola

"Hawana mshahara kwa sasa. Kile wanachopata vitani ndicho hicho. Lakini hilo haliwezi kuhalalisha ubakaji na mauaji mengi yaliyofanywa na pande zote mbili," alisema Parach. "Nafikiri, uwiano wetu wa kijamii katika kipindi chote cha mapigano umevunjika kabisa. Hakuna tofauti kabisa baina ya raia wa kawaida na wapiganaji waliojihami," aliongeza mwandishi huyo.

Thomas Hoerz anayetoa misaada, anasema, mapigano ya wenyewe kwa wenyewe pamoja na njaa Sudan Kusini, ni mambo yatakayokwisha iwapo vijana watavumbua jambo jengine la kufanya badala ya vita.

"Kwa bahati mbaya hatutoi mafunzo ya kazi kwa watu walioko katika hizo kambi. Iwapo wangekuwa wamepata kuwa katika makundi ya wanamgambo," alisema Hoerz. "basi mapigano yangekuwa sio jambo wanaloliona kama njia ya kutatua mambo yao," aliongeza Hoerz.

Mwandishi:Adrian Krisch/Jacob Safari

Mhariri: Iddi Ssessanga