1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yaamua kutomwadhibu mwana mfalme wa Saudi Arabia

Zainab Aziz Mhariri: Tatu Karema
27 Februari 2021

Uamuzi wa rais Joe Biden wa kutomwadhibu mrithi ya mfalme wa Saudi Arabia kwa mauaji ya mwandishi habari Jamal Khashoggi umewavunja moyo wana harakati.

https://p.dw.com/p/3q0dU
Bildkombo Joe Biden und Mohammed bin Salman

Marekani ilitoa taarifa ya kina ya kiintelijensia iliyochelewa juu ya kuhusika kwa mrithi wa mfalme Mohammed bin Salman inayobainisha kwamba mtoto huyo wa mfalme aliridhia mauaji ya Kashoggi kwenye  ubalozi wa Saudi Arabia mjini Istanbul, Uturuki mnamo mwaka 2018. Saudi Arabia imekanusha vikali madai hayo.

Hata hivyo kushutumiwa hadharani kwa mrithi huyo wa mfalme na hatua kadhaa za vikwazo dhidi ya maafisa kadhaa wa Saudi Arabia kunaonyesha mpambanuo mkubwa baina ya sera ya hapo awali ya utawala wa Donald Trump uliojaribu kumkingia kifua mtawala huyo  wa Saudi Arabia lakini nao utawala wa Biden haukuchukua hatua za kumlenga mtawala huyo moja kwa moja.

Soma Zaidi:Saudia yakanusha Bin Salman kuhusika na kifo cha Khashoggi

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken amesema utawala wa Biden unataka kurekebisha uhusiano wake na Saudi Arabia na siyo kuuvunja kwa  sababu Saudi Arabia ni mshirika wa Marekani wa muda mrefu kwenye eneo la  mashariki ya kati.

Mtafiti mchambuzi kwenye wakfu wa Washington wa masuala ya ulinzi wa demokrasia Varsha Koduyayur amesema hiyo siyo hatua kali ambayo wengi waliitarajia. Mtafiti huyo amesema hatua ya Biden inabainisha sera ya jumla ya utawala wake juu ya mfalme wa Saudi Arabia katika kusisitiza juu ya haki za binadamu, kurekebisha sera za utawala wa Trump za miaka minne iliyopita na wakati huo huo kudumisha uhusiano na Saudi Arabia.

Mwandishi wa habari wa Saudi Arabia aliyeuawa Jama Khashoggi
Mwandishi wa habari wa Saudi Arabia aliyeuawa Jama KhashoggiPicha: picture-alliance/newscom/AFP/Getty ImagesTNS

Jopo la wanaharakati la "Freedom House” la Washington limesema ni jambo la kukatisha tamaa kwamba Marekani inakataa kuchukua hatua katika msingi wa ripoti yake ya kiintelijensia na kumwekea   vikwazo mwana mfalme wa Saudi Arabia.

Mashirika ya kutetea haki za binadamu yanautaka utawala wa Joe Biden, pamoja na Umoja wa Ulaya uchukue hatua kali dhidi ya mwana mfalme wa Saudi Arabia kwa mauaji ya Jamal Kashoggi. Ripoti ya upelelezi iliyotolewa na Marekani inaashiria kwamba Kashoggi asingeuliwa bila ya Mohammed bin Salma kutoa idhini.

Malengo ya Utawala wa Biden

Utawala wa Biden una wataalamu mahiri wanaotambua kwamba Marekani inaihitaji Saudi Arabia ili kuweza  kufikia malengo yake katika mashariki ya kati. Hata hivyo maafisa 76 wa Saudi Arabia wamepigwa marufuku kuingia Marekani. Hatua hiyo ni ishara thabiti kwa viongozi wa Saudi Arabia lakini Biden amekwepa hatua kali dhidi ya Saudi Arabia licha ya kauli tupu za  kuiita Saudi Arabia kuwa ni mshirika katika mambo ya  usalama. Utawala wa Trump uliita Saudi Arabia kuwa ni mshirika wa ndani. Wakati huo huo Marekani inatambua kwamba Mohammed bin Salman atakuwamo kwenye  utawala kwa muda wa miaka mingi.

Vyanzo: AFP/RTRE/DPA