1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yaionya Iran

Kabogo, Grace Patricia23 Desemba 2009

Marekani imeionya Iran kuwa mwezi Desemba ni mwezi wa mwisho kwa nchi hiyo kushughulikia mpango wake wa kinuklia baada ya rais Ahmedinejad kupuuzia mapendekezo ya kimataifa.

https://p.dw.com/p/LBEh
Rais Barack Obama ametoa onyo kwa serikali ya Iran kutoa jibu kuhusu madai ya jumuiya ya kimataifa kutaka isitishe mpango wake wa kinuklia.Picha: AP

Marekani imeionya Iran kuwa mwezi Desemba ni tarehe ya mwisho kwa nchi hiyo kushughulikia mpango wake wa nyuklia, baada ya Rais Mahmoud Ahmadinejad wa Iran kupuuza pendekezo la kimataifa juu ya mpango huo. Marekani na Ufaransa zimerudia wito wake kwa Iran kuitaka ikubaliane na azimio la Shirika la Umoja wa Mataifa la za Atomiki la kusafirisha madini yake ya uranium nje ya nchi ifikapo mwishoni mwa mwaka huu ama ikabiliwe na vitisho vya kuwekewa vikwazo zaidi.

Msemaji wa Ikulu ya Marekani-White House, Robert Gibbs, amesema nchi wanachama wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Uingereza, Ufaransa, Urusi, China, Marekani pamoja na Ujerumani, wote walikuwa wakiufatilia kwa makini muda huo. Bwana Gibbs amesema anadhani jumuiya ya kimataifa imeungana pamoja katika kuliangalia suala hili. Msemaji huyo wa Ikulu ya White House amesema azimio hilo siyo tu limetolewa na rais wa Marekani Barack Obama, bali na wanachama wote wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pamoja na Ujerumani na ndio maana wako na jumuiya ya kimataifa ambapo wamekuwa wakisubiri kwa miezi kadhaa kuona kama Iran itatekeleza majukumu yake.

Awali Rais Ahmadinejad aliikataa tarehe hiyo ya mwisho na kuanzisha shinikizo kutoka mataifa ya Magharibi kuhusu hatua ya Iran kukataa kusimamisha shughuli zake za nyuklia au kukubali ukaguzi rasmi ufanywe na Shirika la Umoja wa Mataifa la nguvu za Atomiki-IAEA. Utawala wa Rais Obama umeonya kuwa muda unayoyoma kwa Iran kukubali kujihusisha kidiplomasia katika kutatua mpango wake wa nyuklia pamoja na masuala mengine. Msemaji wa wizara ya mambo ya nchi za nje ya Marekani, Philip Crowley, amesema kama ambavyo nchi ya Marekani imekuwa ikilielezea suala hilo, Rais Obama amesisitiza kuwa Marekani na washirika wake wataiangalia Iran jinsi itakavyoitikia mwito wa kimataifa ikiwa wanaelekea mwishoni mwa mwaka. Alionya kuwa mwaka ujao wa 2010 kama Iran itapaswa kuendelea na hali yake ya sasa, kutakuwa na athari za matokeo ya wao kushindwa kulishughulikia suala hilo.

Marekani itahitaji kuzishawishi Urusi na China kaucha kusita kufikiria kuiwekea vikwazo Iran. Siku ya Jumatatu mshauri mkuu wa Iran kuhusu masuala ya nyuklia, Saeed Jalili, alimueleza Waziri Mkuu wa Japan, Yukio Hatoyama, kuwa silaha za maangamizi ni kinyume na mafundisho ya dini ya Kiislamu na kwamba Iran kamwe haiwezi kutengeneza silaha kama hizo. Iran bado inasisitiza kuwa mpango wake wa nyuklia ni kwa ajili ya kuzalisha umeme. Hata hivyo Iran imekataa pendekezo la shirika la IAEA ambalo linaungwa mkono na Marekani, la kusafirisha madini yake ya uranium ya kiwango cha chini nje ya nchi kwa ajili ya kurutubishwa zaidi. Lakini Rais Ahmadinejad Ijumaa iliyopita katika mahojiano aliliambia shirika la habari la AFP kuwa nchi yake iko tayari kukubaliana na mpango huo wa kurutubisha madini ya uranium kama Marekani na mataifa ya Magharibi wataliheshimu taifa hilo la Kiislamu na kuacha kuipa vitisho.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo (AFP)

Mhariri: Miraji Othman