1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya Urusi na Syria, Idlib, ni uhalifu

Saleh Mwanamilongo
15 Oktoba 2020

Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesema katika ripoti yake kuwa mashambulizi ya ndege za Urusi na Syria dhidi ya raia katika jimbo la Idlib huenda yakawa ni uhalifu dhidi ya binadamu

https://p.dw.com/p/3jy8F
Syrien Idlib Angriffe auf syrisches Rebellengebiet
Picha: picture alliance/AP/G. al-Sayed

Ripoti hiyo ya kurasa 167,iliyopewa kichwa cha '' kulenga uhai Idlib '', iliandaliwa na shirika la Human Rigths watch kufuatia mamia ya ushahidi wa picha na video za setilaiti mnamo kipindi cha Aprili 2019 na Machi 2020.

Mashambulizi hayo yaliwauwa mamia ya raia na kuwalazimisha wengine zaidi ya milioni 1.4 kuyahama makaazi yao. Shirika hilo la kutetea haki za binadamu linasema kwamba mashambulizi hayo ambayo yanafanana na uhalifu wa kivita huenda yakawa uhalifu dhidi ya ubinadamu.

Mkurugenzi mtendaji wa Human Rights watch,Kenneth Roth amesema kwamba shirika lake liliendesha uchunguzi wa mashambulizi 46 kwenye mji wa Idlib ambayo yaliwalenga raia.

'' Kwenye visa hivyo 46,wanajeshi wa Syria na Urusi walishambulia kwa maksudi taasisi au makaazi ya kiraia. Yalilenga hospitali,shule,masoko na maeneo wanakoishi raia. Na siyo kwa bahati mbaya, au kwamba walikuwa wakiwalenga wanaodhaniwa kuwa magaidi,bali kwa makusudi. Hakukuwa na kambi yeyote ya kijeshi, adui yoyote, au kitu ambacho kingesababisha mashambulizi hayo dhidi ya taasisi za kiraia. Ni uhalifu wa kivita wa dhahiri ''.

Syrien, Idlib: Luftangriff auf Schule
Raia wa Syria akitizama kipande cha roketi kilichodondoshwaPicha: picture-alliance/AA/I. Idilbi

Roth amesema kwamba lengo la kampeni hiyo ya kijeshi ya Urusi na Syria ya miezi 11, lilikuwa ni kuwafukuza raia na kugeuza maisha yao kuwa magumu kwa lengo la vikosi hivyo kukalia maeneo hayo.

 Serikali ya Urusi na Syria zimekanusha tuhuma hizo za kuwashambuliya raia kwenye eneo ambako watu milioni tatu walikimbia makwao kutokana na vita ambavyo vinadumu takriban miaka 10.

 Urusi inayounga mkono utawala wa Bachar el Assad, imesema kwamba mashambulizi yao yameyalenga makundi yenye itikadi kali na yenye ushawishi kwenye eneo hilo.

Shirika la Human Rights Watch limesema serikali ya Urusi na Syria hazikutoa majibu kuhusu ripoti hiyo. Operesheni ya kijeshi ya pamoja ya wanajeshi wa Urusi na Syiria ilisitishwa baada ya kutiwa saini kwa mkataba wa usitishwaji mapigano baina ya Uturuki na Urusi. Nchi hizo mbili zimekuwa kiunga mkono pande hasimu nchini Syria.