1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashoga wapinga amri ya Trump kuwazuia kulitumikia jeshi

Isaac Gamba
27 Julai 2017

Waandamanaji wamejitokeza kwa wingi katika kituo cha kusajili wanajeshi mjini New York kupinga uamuzi uliotangazwa na  Rais Donald Trump wa kupiga marufuku watu waliojibadilisha jinsia kulitumikia jeshi.

https://p.dw.com/p/2hDzO
USA - Proteste - Trump will Transgender aus Militär verbannen
Picha: Reuters/C. Allegri

Waandamanaji wamejitokeza kwa wingi katika kituo cha kusajili wanajeshi mjini New York kupinga uamuzi uliotangazwa na  Rais Donald Trump kupitia ukurasa wake wa twitter wa kupiga marufuku watu waliojibadilisha jinsia kufanya kazi  katika jeshi la nchi hiyo. Isaac Gamba anaarifu zaidi katika taarifa ifuatayo.

 Umati uliokuwa na  mamia kadhaa ulikusanyika katika kituo kinachotumika kusajili wanajeshi nchini humo katika  eneo la Time Square  wakiwa wamebeba mabango yaliyokuwa yameandikwa maandishi kupinga marufuku hiyo.

Mmoja wa waandamanji Yael Leberman alisikika akisema kuwa watu waliojibadilisha jinsia wana uwezo wa kutosha kulitumikia jeshi akidai kuwa kazi hiyo inahitaji uwezo kiakili na siyo maumbile.

Hadi sasa haijawa wazi agizo hilo lina maanisha nini hasa kwa watu wa jamii hiyo wanaolitumikia jeshi kwa sasa.

Waandamanaji kadhaa walikusanyika katika jengo la Harvey Milk Plaza lililoko San Francisco huku wakipeperusha bendera za rangi ya pinki na bluu  wakiwa na mabango yaliyosomeka " maisha ya watu waliojibadilisha jinsia sio mzigo" na kupaza sauti za kupinga amri hiyo ya Trump.

Mwanamke mmoja aliyejibadilisha jinsia aliyejitambulisha kwa jina la Layla aliueleza umati huo kuwa amechoshwa na kuambiwa  kuwa anapaswa kuwa mtu wa namna gani na kuitaka jamii ya mashoga kuwaunga mkono katika harakati zao za kupigania heshima yao.

Katika kusanyiko dogo kwenye kituo cha jamii ya mashoga kilichoko Los Angeles, Rudy  Akbarian mwanajeshi ambaye pia amejibadilisha jinsia alisema kuwa  awali alidhani taarifa hizo zinazohusiana na marufuku  hiyo ya la Rais Trump zilikua ni utani  lakini baadaye zimemuuza  baada ya kubaini kuwa ni kweli.

Amesema kuna watu ambao wanastaafu sasa jeshini, na kuna watu waliolitumikia jeshi miaka 18 ama 19 hivyo haitakuwa haki kwao  na kusisitiza kuwa  hawatakata tamaa na wataendelea kupambana.

Wanaharakati wengi wa makundi ya jamii ya mashoga nchini Marekani hawakuwahi kuamini ahadi za Rais Donald Trump wakati wa kampeni kama zitakuwa nzuri kwa upande wao lakini kwa hatua hii ya kuwapiga marufuku watu waliojibadilisha jinsia kutumikia jeshi ukiacha maamuzi mengine yanayofanywa na kiongozi huyo yakiwemo yanayohusiana na uteuzi basi yanafanya jamii hiyo imuone kuwa kwao ni adui.

USA Donald Trump
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: picture alliance/AP/E. Vucci

 Sarah Kate Ellis Rais wa kundi la wanaharakati wa kutetea haki za mashoga linalojulikana kama GLAAD amesema utawala wa Rais Donald Trump hautaacha kutekeleza sera zinazopinga haki za mashoga na hata kwenda mbali zaidi na kuwanyima wamarekani ambao ni jamii ya aina hiyo  wenye uwezo na nguvu za kutumika katika kulinda taifa lao.

Kwa upande wake chama cha Democratic kinakusudia kuzuia marufuku hiyo ya Rais Trump dhidi ya watu waliojibadilisha jinsia kulitumikia jeshi.

Wanajeshi waliojibadilisha jinsia wamekuwa wakitumika jeshini tangu mwaka jana kutokana na hatua iliyochukuliwa na waziri wazamani wa ulinzi wa Marekani Ash Carter.

Hata hivyo hatua ya Trump kusitisha sera hiyo ni ya hivi karibuni na huenda ni kali zaidi katika wimbi la hatua alizokwisha chukua tangu aingie madarakani.

Maafisa wengi wa ngazi ya juu walioteuliwa na Trump akiwemo makamu wa Rais Mike Pence, mwanasheria mkuu Jeff Sessions na waziri wa afya pamoja na huduma za kibinadamu   wana msimamo wa kupinga haki za mashoga.

Mwandishi: Isaac Gamba/ape

Mhariri: Iddi SSessanga