1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo kuhusu ujenzi wa bwawa la umeme la GERD yamekwama

Saleh Mwanamilongo
6 Aprili 2021

Mazungumzo yamekwama mjini Kinshasa baina ya Misri,Sudan na Ethiopia kuhusu ujenzi wa bwawa la umeme kwenye mto Nile.Rais wa Congo anatajia kuweko na suluhu.

https://p.dw.com/p/3rcIO
Ethiopia ilianza ujenzi wa  bwawa la Grand Renaissance litakalozalisha umeme lenye thamani  ya  dola  bilioni 4.8 mwaka 2010,kama sehemu ya mpango  wa  kupanua  uuzaji  wake  wa  nishati nje ya nchi.
Ethiopia ilianza ujenzi wa bwawa la Grand Renaissance litakalozalisha umeme lenye thamani ya dola bilioni 4.8 mwaka 2010,kama sehemu ya mpango wa kupanua uuzaji wake wa nishati nje ya nchi.Picha: DW/Negassa Desalegen

 Hadi usiku kucha,mawaziri hao wameshindwa kufikia makubaliano. Duru kutoka ikulu ya rais Tshisekedi zinasema kwamba mazungumzo yamekwama kufuatia hasa vipingamizi vya Sudan. Lakini hata hivyo hazikufafanua kuhusu hatua iliyokwamisha mazungumzo hayo.

Juhudi za diplomasia za Umoja wa Afrika

 Kwenye hafla ya ufunguzi wa mkutano huo, rais Felix Tshisekedi alizitolea mwito nchi hizo kuyapa kipau mbele maslahi ya wananchi wao. Na kuwahimiza wajumbe wote kwenye mkutano huo kufikia makubaliano ya kimsingi.

'' Tofauti kuhusu ujenzi wa bwawa la umeme la Ethiopia la Renaissance, haziwezi kuchukuliwa kama janga, bali kama fursa kwa ajili ya kuwaweka pamoja raia wetu na mwanzo mpya wa uhusiano wa mipakani na wa kikanda.'',alisema Tshisekedi.

Kulingana na ajenda ya mkutano huo wa Kinshasa,ni kwamba mawaziri hao wa mambo ya nje na wa umwagiliaji kutoka Misri,Sudan na Ethiopia watajadili masuala ya kiufundi na kisheria kuhusu ujenzi wa bwawa hilo la umeme kwenye mto Nile.

 Kabla ya mkutano huo ,Sameh Shoukry, waziri wa mambo ya nje wa Misri,aliviambia vyombo vya habari vya nchi yake kwamba mkutano huo wa Kinshasa ni wamatumaini ya mwisho katika kufikia makubaliano .

Vitisho vya Misri na Sudan 

Rais wa Misri Abdel Fattah el-Sisi na Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed Ali,mjini Cairo,Misri Juni 2018.
Rais wa Misri Abdel Fattah el-Sisi na Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed Ali,mjini Cairo,Misri Juni 2018.Picha: Imago Images/Xinhua

Mazungumzo ya awali baina ya nchi hizo tatu ,chini ya upatanishi wa Umoja wa Afrika na rais wa zamani wa Marekani Donald Trump, yalishindwa kutoa suluhu ya kudumu juu ya hatua ya Ethiopia ya kujenga bwawa kubwa la kuzalisha nishati ya umeme.

Ethiopia ilianza ujenzi wa  bwawa  hilo kwenye Blue Nile, mwaka 2010, kama  sehemu ya mpango  wa  kupanua  uuzaji  wake wa nishati nje ya nchi.

Wiki iliopita Rais wa Misri, Abdel Fattah el-Sissi alionya juu ya hali ya kutokuwa na utulivu katika eneo hilo iwapo mradi huo wa Ethiopia utaendeshwa bila ya makubaliano ya kisheria.

el-Sissi amesema hakuna anayeweza kuchukua hata tone moja la maji kutoka Misri, na kumuonya yoyote anayetaka kufanya hivyo.

Rais huyo wa Misri hata hivyo, alisema nchi yake inaunga mkono mazungumzo juu ya kutatua mzozo uliopo kabla ya Ethiopia kuendelea na mchakato wa kujaza hifadhi kubwa ya bwawa wakati wa msimu wa mvua mwaka huu. Ethiopia ilianza kujaza bwawa hilo Julai mwaka uliopita, hatua ambayo ilikosolewa vikali na Misri na Sudan.