1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya amani ya Syria yaanza tena

13 Aprili 2016

Duru mpya ya mazungumzo ya amani yenye lengo la kumaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Syria vilivyodumu miaka mitano sasa yameanza leo jijini Geneva

https://p.dw.com/p/1IUNz
Staffan de Mistura in Syrien Damaskus
Picha: Reuters/O. Sanadiki

Hayo yanajiri wakati kuongezeka kwa mapigano katika mkoa wa kaskazini Aleppo kukiutishia mpango tete wa kuweka chini silaha.

Mazungumzo hayo yanayosimamiwa na Umoja wa Mataifa yanalenga kuunda serikali ya mpito nchini Syria itakayofuatwa an uchaguzi mkuu wa kumaliza mzozo ambao umewauwa zaidi ya watu 270,000 na kuiacha nusu ya idadi ya watu nchini humo bila makaazi.

Hatima ya Rais Bashar al-Assad inasalia kuwa kizuizi katika mazungumzo hayo, na mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Syria Staffan de Mistura amefanya mikutano na washirika wakuu wa Assad- Iran na Urusi kabla ya kukutana leo na Kamati Kuu ya Mazungumzo inayouwakilisha upinzani, na kisha wawakilishi wa serikali baadaye wiki hii.

Kuongezeka kwa machafuko katika siku chache zilizopita kumetishia mpango wa kihistoria wa kusitisha mapigano uliosainiwa mwezi Februari – ambao unaendelea kuheshimiwa kwa kiwango kikubwa – na kuongeza shinikizo kwa mazungumzo haya, ambayo yanafuata majaribio mawili ya awali yaliyoshindikana ya kutafuta ufumbuzi wa kumaliza muwagaji damu nchini humo.

Syrien Parlamentswahlen
Uchaguzi wa bunge unaendelea katika maeneo yanayodhibitiwa na serikali nchini SyriaPicha: Reuters/O. Sanadiki

Suala jingine la mvutano wakati mazungumzo hayo yasiyo ya moja kwa moja yakianza ni uchaguzi wa bunge unaoandaliwa leo katika maeneo yanayodhibitiwa na serikali kote nchini humo. Umoja wa Mataifa hauutambui uchaguzi huo, ambao pia umepuuzwa na wapinzani wa Assad ndani na nje ya Syria wakisema sio wa haki.

Rais Bashar al Assad na mkewe Asma wamepiga kura zao mjini Damascus. Uchaguzi wa bunge nchini Syria huandaliwa kila baada ya miaka minne, na serikali inasema uchaguzi huo ni wa kikatiba na uko tofauti na mazungumzo ya amani yanayoendelea Geneva.

Mpango huo wa kuwekwa chini silaha umewezesha kupelekwa misaada ya kiutu katika maeneo yaliyoathirika na pia kupungua kwa kiasi kikubwa idadi ya vifo vya raia. Bettina Lüscher ni Msemaji wa Mpango wa Chakula Duniani - WFP "Hii itachukua wiki kadhaa, na tutaendeleza juhudi hizi, na kujaribu kuwasiliana na watu walioko katika maeneo yaliyoathirka kuona namna tunavyoweza kuyafikia. Lakini tunaendeleza operesheni hadi tutakapowafikia watu wote wanaohitaji chakula. Lakini bila shaka kwa kufanya hesabu, itachukua muda mrefu".

Wakati huo huo majeshi yanayoiunga mkono serikali yameendelea kusonga mbele katika mji wa Al-Eis unaodhibitiwa na kundi lenye mafungamano na al-Qaeda, Al-Nusra Front, na waasi washirika. Shirika linalofchunguza haki za binaadamu nchini Syria limesema kundi la Al-Nusra na waasi walipiana na vikosi hivyo na kuwawau wanajeshi 23 watiifu kwa Assad, wakiwemo wapiganaji wa Kiiran na Kiafghanistan.

Wapiganaji kama hao kutoka al-Nusra Front na kundi linalojiita Dola la Kiislamu hawashirikishwi katika mpango wa kusitisha mashambulizi. Lakini katika baadhi ya maeneo, al-Nusra inashirikiana na wanajeshi waasi wanaostahili kushirikishwa na mpango huo.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Gakuba Daniel