1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mdahalo badala ya mbinyo: Baada ya mazungumzo ya Geneva na Iran

Miraji Othman2 Oktoba 2009

Iran: sasa Uranium yake itasafishiwa Russia

https://p.dw.com/p/JwQe
Picha ya kinu cha Bushehr, kusini mwa Iran, cha kutengenezea nishati ya kinyukliyaPicha: dpa

Baada ya miaka ya malumbano kuhusu programu ya Iran ya kuwa na nishati ya kinyukliya, tangazo la jana la mshauri mkuu wa nchi hiyo kuhusu suala hilo, Saeed Jalili, lilikuwa sio la kawaida. Yaonesha kutafuata mazungumzo mazuri baada ya yale ya jana ya huko Geneva kati ya Iran na madola makuu yalio wanachama wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pamoja na Ujerumani. Sura iliojitokeza hadi sasa ni ya kutia moyo, kuliko vile ilivoweza kutarajia hapo kabla.

Mkutano huo wa mwanzo wa jana wa mshauri huyo wa Iran kuhusu masuala ya programu ya kinyukliya ya nchi hiyo ulikuwa hapo mwanzo haujawekewa matarajio makubwa, licha ya kwamba mara hii Marekani, kwa mara ya kwanza, ilishiriki kikamilifu. Pia hali ya mambo katika wakati wa karibuni ilikuwa sio nzuri, kwani Iran ilitangaza kwamba inajenga kinu kingine cha kurutubisha Uranium na pia , bila ya kujali, ilifanya majaribio ya maroketi yake ya masafa ya wastani. Hali hiyo ilifanya ile nafasi alioitoa Rais Barack Obama wa Marekani ya kufanya mdahalo na Iran kufifia zaidi.

Hata hivyo, mazungumzo ya jana ya huko Geneva yaliweza kuzituliza zile hisia za kuvunjika moyo zilizokuweko. Ilitangazwa kwamba mazungumzo ya jana yatarejewa tena mwisho wa mwezi huu wa Oktoba, na hadi wakati huo kutachukuliwa mlolongo wa hatua madhubuti. Kwa mfano, wakaguzi wa wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Kinyukliya wa huko Vienna wataweza kwenda kukikagua kinu kipya cha Iran chenye kurutubisha Uranium, au kwamba Uranium ambayo imesafishwa na Iran itapelekwa Russia kuzidi kurutubishwa.

Pindi mambo hayo yatatimizwa, basi ataadhibiwa yule yeyote ambaye mnamo siku za karibuni aliendeleza uwongo dhidi ya Iran na kutaka vikwazo zaidi viwekewe nchi hiyo. Wa mwanzo wao ni nchi za Ulaya. Warussia na Wachina walijitenga au kulipinga wazo hilo,na pia Rais wa Marekani Barack Obama aliendelea kushikilia kwamba hatarejea nyuma katika ule mpango wake wa kutaka kufanya mdahalo na Iran. Baada ya mazungumzo ya jana, rais huyo alisisitiza juu ya jambo hilo.

Yaonesha Iran imejiamulia, angalau kwa sasa. Na huo ni ukweli. Sura ya hapo kabla inaonesha inajikariri. Nayo ni kwamba Iran maisha huregeza kamba pale ule wakati wa mwisho iliowekewa kutenda jambo fulani unapokaribia. Na hivyo pia ndivyo ilivyo sasa. Hadi mwisho wa mwezi wa Septemba watu walitaka wangojee na baadae waamuwe juu ya hatua zitakazofuata. Kitisho hicho sasa hakiko. Kutafanywa mashauriano zaidi, hivyo Iran itajipatia wakati zaidi, bila ya ya hata kidogo kusogea kutoka msimamo wake wa hapo kabla.

Mwandishi: Phillip, Peter/ Othman, Miraji/ZP

Mhariri: Mohammed Abdulrahman