1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mei mosi, vipi wafanyikazi walivyoiadhimisha siku hii ulimwenguni ?

Jane Nyingi/ AFPE..Picha AFP1 Mei 2009

Polisi nchini Ugiriki, watumia vitoa machozi kuwatawanya waandamanaji.

https://p.dw.com/p/HiGh
Mwandamanaji akiwa mbele ya polisi wa kuzima ghasia nchini Ugiriki.Picha: picture-alliance / dpa

Huku ulimwengu mzima ukiadhimisha siku ya wafanyikazi ulimwenguni hii leo, nchini Ugiriki polisi wamelazimika kutumia vitoa machozi kuwatawanya waandamanaji ambao waliteketeza gari moja mjini Athens. Nchini Ukraine wanaharakati wa kisiasa kutoka mrengo wa kulia na kushoto waliandamana mjini Kiev kuadhimisha siku hii ya mei mosi.

Zaidi ya watu elfu 6 walifanya maandamano ya amani katika mji mkuu wa Ugiriki, Athens kama ilivyo tamaduni yao kuadhimisha siku hii ya wafanyikazi. Hata hivyo hakukuripotiwa majeruhi au kukamatwa kwa yeyote. Zaidi ya polisi elfu 4 hata hivyo walipelekwa katika mji mkuu kushika doria ili kuzuia machafuko kutokea.


Mwezi Disemba mwaka jana Ugiriki ilishuhudia maandamano mabaya katika miongo kadhaa, yaliyochochewa na ukuaji pole wa uchumi na kuwepo kwa idadi kubwa ya vijana wasio na ajira. Kwa mujibu wa shirika la fedha duniani, IMF, idadi ya watu wasio na kazi nchini humo imeongezeka kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2004 huku ukuaji wa uchumi wake ukikaribia kusimama na huenda hata ukanywea mwaka huu wa 2009 kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka mitano.


Nchini Ukraine karibu wakomunisti elfu 2 na wafuasi wa wanasiasa wa mrengo wa kushoto walikusanyika katika mji mkuu Kiev, kwa hotuba za kila mwaka kuadhimisha sikukuu ya wafanyikazi. Karibu mita 500 kutoka mahala walipokuwa, wapinzani wao kutoka kundi dogo la wazalendo wa mrengo wa kulia pia waliandaa maandamano yao.

Wahlen in der Ukraine
Maelfu ya watu walioandamana leo katika mji mkuu wa Ukraine,KievPicha: AP


Polisi walikuwa katika eneo hilo kuhakikisha kuwa makundi hayo mawili hayakabiliani. Siku hii ya mei mosi ambayo wakati mmoja ilikuwa sikukuu muhimu katika muungano wa zamani wa Sovieti, hivi sasa inachukuliwa na Waukraine wengi kuwa siku ya mapumziko na kufanyika kwa maandamano ya makundi ya kisiasa.


Maandamano mengine kwa minajili ya siku hii pia yamefanyika nchini Ufaransa, huku yakiandaliwa na vyama vya wafanyikazi. Maafisa wa vyama hivyo wamesema wameyaitisha ili kulalamikia anavyoushughulikia uchumi rais Nicolas Sarkozy, hii ikiwa ni mara ya tatu kwa vyama hivyo kuitisha maandamano kama hayo mwaka huu.


Idadi ya watu wasiokuwa na ajira nchini Ufaransa iliongezeka kwa karibu millioni 2.5 mwezi Machi na asilimia 2.7 mwezi uliotangulia wa Februari. Idadi ya wanaotafuta kazi walio chini ya umri wa miaka 25 imeongezeka kwa asilimia 36 mwaka baada ya mwingine.


Ongezeko la watu wasiokuwa na ajira kote barani Ulaya na kwingineko limeongeza idadi ya maandamano ya siku ya leo ya wafanyikazi. Kulikuwa na mapambano makali kati ya polisi na waandamanaji hapa Ujerumani nanchini Uturuki maandamano hayo yalibadilika na kuwa ghasia.


Polisi wa kukabiliana na ghasia walitumia maji kuwatawanya waandamanaji ambao waliwarushia mawe na mabomu ya petroli yanayorushwa kwa mkono. Waandamanaji hao kisha walifanya uharibifu mkubwa kwa kuvunja vioo vya benki moja na maduka katika eneo walilokuwa wakiandamana.


Polisi wamesema wanawazuilia waandamanaji 68, huku polisi 11 wakijeruhiwa wakati wa makabiliano hayo. Mjini Berlin na Hamburg hapa Ujerumani machafuko yalitokea mapema leo na kusababisha kujeruhiwa kwa zaidi ya polisi 50 wa kuzima ghasia.

Estland Tallinn Unruhen um sowjetisches Kriegerdenkmal weiten sich aus
Polisi mjini Berlin,Ujerumani wakimzuia mwandamanaji kuzua vuruguPicha: AP

Karibu waandamanaji 200 waliwarushia polisi mawe na chupa na pia kuteketeza magari matano. Ujerumani hivi sasa inakabiliwa na hali mbaya ya kiuchumi tangu vita vya pili vya dunia.